Sunday 31 December 2006

Mahakama za Zenj na Matatizo ya Ubabe

Mahakama za zenj katika ngazi zote kuanzia mahakama ya wilaya hadi mahakama kuu ya rufaa zimekuwa zikukutana na wababe ambao hupinga maamuzi ya mahakama hizo kwa muda mrefu sasa.

Tukio la hivi karibuni huko Kibeni katika mkoa wa Kaskazini linathibitisha kuwa maamuzi mengi ya mahakama yamekuwa hayakubaliwi na wanajamii na hasa yale ambayo yamekuwa yakihusisha ujenzi wa nyumba.

Zipo kesi nyingi kuhusu migogoro ya ardhi katika Zanzibar, kesi hizi nyingi zimetokana na kutokuwepo na uwazi katika sheria ya ardhi ya mwaka 1985. Kwa ufupi ardhi yote ya Zanzibar ni mali ya serikali na sio vipando katika ardhi hiyo. SMZ ndio yenye jukumu la kupanga na kugawa ardhi visiwani humo, na kutoa umiliki wa ardhi kwa mtu binafsi, taasisi, mashirika n.k

Kwa upande mwingine serikali hiyo hiyo imekuwa ikitambua baadhi ya hati miliki za ardhi ambazo zilitolewa kabla ya mapinduzi ya Zanzibar(1964) mwa madai kuwa ardhi hizo hazikuwahi kutaifishwa na kuwa mali ya serikali au zimetiwa wafku hivyo serikali haiwezi kuzitaifisha...! Sasa unaposema kuwa ardhi yote ya Zanzibar ni mali ya serikali huku ukijua kuwa sio kweli maana yake ni nini? ka si kupotosha ukweli na kujenga mazingira ya dhuluma!

Matatizo mengine ambayo yanachangia kuwafanya wananchi kuwa wababe dhidi ya maamuzi ya serikali na vyombo vyake, ni kutojulikana kwa wigo za kiutawala visiwani humo. Haijulikani ni wapi ardhi ya serikali inaanzia na wapi inaishia, hata hizo wizara zimekuwa kimya kuelimisha wananchi juu ya suala zima la ardhi.. Wananchi wameachwa kwenye giza huku watawala wakijua hilo pasipo kufanya lolote za ya kukurupuka pale yanapotokea matatizo ya ardhi kwa kutoa amri kubwa kubwa.

Ubabe wa wananchi katika kupinga Hukumu za Mahakama umetokea huko Shakani katika wilaya ya Magharibi mkoa wa Mjini/Magharibi na sasa zimehamia katika mkoa wa Kaskazini. Hii yote ni kwa sababu SMZ imeshindwa kusimamia sheria zake. Iwapo serikali hiyo ingekuwa wazi na hasa kwenye eneo la ardhi lenye migogoro mingi, hapana shaka kusingekuwepo na matatizo haya ya baadhi ya watu kukejeri na kupuuza amri za mahakama.

Kingine watendaji wa SMZ, kwa kujua mapungufu ya serikali wamekuwa ndio mashawishi wakubwa wa kuwepo kwa migongano ya ardhi. Aina hii ya undumilakuwili inatisha na inapaswa kufanyiwa kazi

Friday 29 December 2006

Watanzania wanapokutana

Mwaka huu unaokwisha kuwekuwepo na matukio mbalimbali yaliyoweza kukutanisha watanzania toka zaidi ya mji mmoja.. hapa chini ni mojawapo ya matukio hayo

Monday 25 December 2006

Zenj na visa vya ardhi mwaka huu....

Mwezi wa tatu 2006
Kuna kauli moja iliwahi kutolewa na rais wa awamu ya nne katika SMZ kuwa Zanzibar ni "Njema na kila atakae kuja basi anakaribishwa" Kutokana na kauli hiyo Zanzibar ilishuhudia mabadiliko ya nguvu katika sekta zote kuanzia ya kibiashara,kijamii na kadhalika. Mamia ya watu walianza kufanya biashara wageni wakiongezeka na kuufanya mji wa zanzibar kuwa mdogo kutokana na msongamano wa watu.
Kuingia kwa awamu ya tano kulishuhudiwa na mabadiliko makubwa zaidi,mabadiliko haya zaidi yalikuwa katika kuendeleza ardhi ya zanzibar. Hapa inabidi tukumbuke kuwa ardhi yote ya Visiwa vya Zanzibar ni mali ya serikali. Hivyo ili uweze kuendeleza ardhi hiyo ni shurti uwe na hati ya kumiliki ardhi hiyo toka serikalini. Katika awamu ya tano kulikuwa na wimbi kubwa la ujenzi wa nyumba za kuishi na mahoteli, kutokana na kuwa serikali ndio mmiliki wa ardhi kwa kiasi kikubwa ilishindwa kukidhi maombi mengi ya viwanja. Hili likawa ni tatizo kubwa na tena kubwa sana. Hadi mwaka huo tayali mji wa zanzibar ulikuwa unafuata mapendekezo ya mastertplan ya wachina ya mwaka 1982 iliyotiliwa nguvu na sheria ya upimaji miji na ardhi ya mwaka 1985.
Master plan hiyo iliongeza ukubwa wa mji wa zanzibar na ilikuwa imeshatenga maeneo ambayo serikali ilitakiwa kuyaendeleza aidha kwa kujenga nyumba au kugawa ardhi hiyo kwa wananchi wanaotaka kujenga nyumba. Hilo halikufanyika na kama lilifanyika basi ni kwa kiwango kidogo sana. Maeneo hayo yaliyopimwa na kuonyeshwa kwenye master plan ni pamoja na eka tatu ambazo zilitolewa na serikali ya awamu ya kwanza na ya pili kwa lengo la kuwapatia wananchi wa visiwa hivyo sehemu za kulima. Katika awamu hizo wananchi wengi walikuwa wanaishi katika maeno ya umbali wa maili tano kuzunguka mji.
Eka tatu karibu zote zilikuwa nje ya mji na ziliguswa na master plan. Kutokana na mabadiliko ya kiuchumi na mahitaji makubwa ya ardhi kwa ajili ya ujenzi, eka tatu taratibu zilianza kujengwa. Ilikuwa ni kazi ya ziada kujenga katika eka hizo ukizingatia kuwa ardhi ni mali ya serikali. Hata kupitia Mambo msige ambao wao pia wanatoa hati ya kumiliki mali, wananchi waliona huko ndiko kwepesi kwa kupata hati ya kumiliki ardhi.Hivyo wananchi walianza kujenga misingi ya nyumba katika heka hizo na baadae kuziuza na serikali kupitia idara yake ya mambo msige kuidhinisha na kuthibitisha uuzaji na uendelezaji wa ardhi hiyo ambayo awali ilikusudiwa kuwa ni ya kilimo.
Vita kati ya idara za serikali ukaanza taratibu kati ya idara ya Ardhi na Idara ya Mambo msige, huku serikali kuu ikikaa kimya. Leo katika kusoma gazeti nimekutana na kauli ya Waziri wa Waziri wa Maji, Ujenzi na Ardhi Bw. Mansour Yussuf Himid akisema kuwa smz itabomoa nyumba zote zilizojengwa kwenye eka tatu. Kauli hii kwa kweli imenitisha mno. Na ni kauli nzito sana kwa waelfu ya wakaazi wa Visiwa hivyo. Kwani kwa namna moja ama nyingine watakaoadhirika na bomoabomoa hiyo ni wengi, na ni kuanzia kwenye mahoteli yote ya kitalii yaliyojengwa baada ya mwaka 1985, viwanda na maelfu ya nyumba za kuishi.
Tutabomoa nyumba zilizojengwa kwenye ardhi za ekari tatu
zilizotolewa kwa
wananchi baada ya Mapinduzi,’’ alisisitiza Waziri
.

http://www.ippmedia.com/ipp/nipashe/2006/03/16/62186.html

Mapema mwezi wa nne 2006

Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imeagiza nyumba zote zilizojengwa katika vyanzo vya maji zibomolewe na watendaji wa serikali waliotoa vibali vya ujenzi walipe fidia hizo. Zaidi hapa..http://www.ippmedia.com/ipp/radio1/2006/04/14/64264.html

Mwezi wa nne 2006

Hatimae Waziri Kiongozi wa SMZ amebadili kauli yake juu ya ulipwaji wa fidia kwa nyumba zitakazobomolewa kwenye vyanzo vya maji.Sasa wale waliojenga nyumba hizo hawatalipwa fidia tena.... Zaidi ametupa lawama kwa watendaji wa SMZ kwa kuwa wavivu na mwenye upungufu mkubwa wa kiuwezo katika utendaji wa kazi zao...

Chanzo:http://www.ippmedia.com/ipp/nipashe/2006/04/17/64424.html

Shirika la Meli Zanzibar: Kulikoni?

Imelipotiwa hivi karibuni kuwa Meli ya Mv Maendeleo ilishindwa kuendelea na safari yake kuelekea Pemba ikiwa inatokea Zanzibar. Tatizo lilikuwa ni kuzimika kwa injini yake. Kabla ya kuanza kwa safari hiyo, injini ya meli hiyo ilishindwa kuwaka, hata baada ya kuwaka safari ya kwenda Pemba haikukamilika kwani meli hiyo ilisimama na kubidi kulaza abiria wote ndani ya meli hiyo umbali mfupi tokea katika Bandari ya Malindi Zanzibar.
Kushindwa kuendelea kwa safari hiyo kulizua kero kubwa kwa abiria ambao licha ya kutofika safari yao, iliwalazimu kulala ndani ya meli hiyo katika mazingira magumu, huku hali ya bahari ikiongeza ugumu wa kukesha katika chombo hicho.
Shirika la Meli la Zanzibar ni mojawapo wa mashirika yanayotoa huduma ya usafiri baharini katika visiwa vya Zanzibar, aidha zaidi ya kusafirisha abiria wanahudumia pia usafirishaji wa mizigo na mafuta ya magari. Shirika hilo ndio kongwe katika usafiri wa baharini na lenye vyombo vikubwa.
Tokea kuanzishwa kwake limekuwa tegemeo kubwa kwa usafiri, kabla ya kuingia kwa mashirika binafsi katika sekta hiyo. Hata hivyo mafanikio yake yamekuwa ni kidogo au pengine kutokuwepo kabisa. Shirika hilo limeshauza baadhi ya meli zake, lakini haijawahi kuongeza meli nyingine yoyote licha ya kuendeshwa kibiashara. Meli zake zote ni mbovu na pamoja na kutumia gharama kubwa kuzifanyia matengenezo bado zimekuwa zikiendelea kuwa mbovu na mbovu zaidi.
Meli zake za abiria zote mbili yaani Mv Mapinduzi na Mv Maendeleo zimeshawahi kuzuiwa kuingia katika Bandari ya Dar es Salaam kutokana na kushindwa kukamilisha taratibu za kiusalama zinazohusu vyombo vya baharini. Hata hivyo zimekuwa zikiruhusiwa tena kuingia katika bandari hiyo kwa sababu ambazo hata mimi sijaweza kuzifahamu. Zaidi ya kutokuwa na mfumo unaotakiwa wa usalama meli hizo zimechakaa na kuchoka hasa upande wa injini zake. Hazina uwezo wa kufanya safari kwa miezi mitatu mfululizo pasipo kuharibika injini zake.
Uchakavu wa meli hizo unatokana na kutumika kwa muda mrefu na kwa upande mwingine ni kutokana na hujuma zinazofanywa na wafanyakazi wa meli hizo. Kuna hujuma nyingi zinazofanywa na wafakazi hao kuanzia kuuza kwa vipuli hadi mafuta ya meli hizo. Vitendo hivi ufanyika bila kificho na kwa ushirikiano miongoni wa wafanyakazi hao.
Zaidi Shirika hilo baada ya kufanya kazi kwa miaka zaidi ya arobaini na mbili, inawapasa sasa watuonyeshe mafanikio yao kwa kuweza kuwa na vyombo vya uhakika. Miaka chini ya kumi iliyopita Mv Maendeleo iliwahi kukodishwa, na ilikuwa ikifanya kazi vizuri tu, mara baada ya muda wa kukodishwa kwisha meli hiyo imeshindwa kuwa nzima tena. Na kabla ya kukodishwa ilikuwa mbovu. Sasa ni swala la kujiuliza kwanini meli hiyo iliweza kufanyakazi vizuri ilipokodishwa na kwanini inashindwa kufanya kazi chini ya shirika lenyyewe...
Kulikoni?

Saturday 9 December 2006

Athari za Wizara kung'ang'ania madaraka....

Wakati mamilioni ya Watanzania leo hii wanasherekea siku ya uhuru wa Tanganyika, Huko Zanzibar, suala la uchafuzi wa Mazingira limechukua sura mpya. Hii ni baada ya wizara ya maji, ujenzi, nishati na ardhi kutangaza kuwa hapatakuwa na ruhusa kwa mwekezaji kujenga hoteli pasipo kuwa na water treatment plant na sehemu ya kuchomea taka ngumu ( incinerator).

Tatizo la utupaji wa taka ngumu na taka maji katika ukanda wa hoteli za kitalii na hasa maeneo ya mashariki na kaskazini ya kisiwa hicho yapo kwa muda mrefu sasa. Hoteli nyingi kubwa na ndogo zimekua zikitupa taka zao kwa njia wanazojua wao wenyewe. Kuna hoteli ambazo zimekuwa zikitupa taka ngumu moja kwa moja baharini, wengine kuzichimbia ardhini na wapo waliokuwa wanazichoma sehemu ya mbali toka katika maeneo yao. Hali kadhalika taka maji zimekuwa zikitupwa moja kwa moja baharini na kwenye maeneo ya karibu na bahari.

Matatizo ya kukosekana kwa mfumo wa utupaji wa taka na hasa nje ya halmashauri ya manispaa ua zanzibar, yamechangiwa kwa kiasi kikubwa na baadhi ya wizara kung'ang'ania madaraka na hasa kwenye maeneo nyeti ya ardhi na uwekezaji. Kimsingi Mamlaka ya Maji huko visiwani inashughulika na usambazaji wa maji safi tu katika visiwa hivyo, huku jukumu la maji taka likiwa chini ya halimashuri ya manispaa ya zanzibar..ambayo ina eneo dogo tu la utawala. Zaidi hata katika eneo hilo dogo la kiutawala, haina sauti kisheria juu ya usimamiaji wa maji taka katika hoteli ambazo zimejengwa ndani ya Manispaa hiyo. Vyombo vinavyohusika hapo ni ZIPA na Idara ya Upimaji na Mipango Miji. Cha kushangaza hata Idara ya Mazingira imekuwa ikiwekwa pembeni mno kuhusu shughuli nyingi za uendelezaji wa ardhi katika visiwa hivyo.

Baada ya Miaka kumi na sita ya uendelezaji wa Mahoteli ya kitalii katika fukwe za visiwa hivyo pasipo na mfumo wowote wa utunzaji wa mazingira, athari zake sasa zimeanza kuoneka wazi. Hoteli hizo hazina mfumo wowote wa kusafisha maji taka kabla ya kuyamwaga baharini na hakuna sehemu maalumu ya utupaji wa taka ngumu katika maeneo ya hoteli hizo. Kila mwenye hoteli anafanya chochote atakachoweza katika kutupa taka zake.

Haya yote yametokana na baadhi ya wizara kung'ang'ania kila kazi, Kwa mfano jukumu la Idara ya Mazingira katika uwekezaji na katika suala zima la maendeleo hasa katika sekta ya ujenzi halijulikani. ZIPA ikishirikiana na Idara ya Mipango Miji/Vijiji wameshindwa kuonyesha ni kwa nanma gani taka zinazozalishwa kila siku katika mahoteli hayo zitakavyoweza kuhifadhiwa, kutupwa au kutumika tena, na mbaya zaidi haijulikani ni mamlaka ipi inayoshughulikia maji taka nje ya Manispaa ya zanzibar.

Iwapo ZIPA na Idara ya Mipango Miji/Vijiji ndio wanaochukua kodi za uanzishwaji wa mahoteli ya kitalii inawapasa wawajibike na kupanga mfumo unaoeleweka ukusanyaji na utupaji wa wa taka katika Maeneo ya hoteli. Ushirikishwaji wa mamlaka za serikali za mitaa katika maeneo hayo pamoja na idara ya mazingira lazima utazamwe upya.