Thursday 15 February 2007

Sasa ni Disco...!

Katikati ya mwaka jana(2006)SMZ ilipigia marufuku matumizi ya simu za mkononi kwa wanafunzi wote wa shule za Msingi na Sekondari kwa madai kuwa, simu hizo zinachangia kwa kiasi kikubwa kwa wanafunzi kushiriki katika vitendo vya ngono, aidha wanafunzi hao wamekuwa wakipoteza muda mrefu kuandika meseji na kupokea simu wawapo darasani na katika maeneo ya shule.

Sasa SMZ imenyoshea mkono Disco kuwa imesababisha kwa wanafunzi wengi kufeli mtihani wa kidato nne wa mwaka jana. Hivyo ni marufuku kwa mwanafunzi yoyote wa shule ya msingi na sekondari kwenda Disco!

Hatua ya kupiga marufuku kwa wanafunzi kwenda kwenye madisco na kumbi za starehe zimepokelewa kwa mitazamo tofauti na waakazi wa visiwa hivyo, ambapo Disco na mojawapo ya sehemu ndogo tu ya Starehe zinazopatina kwenye visiwa hivyo.

Wanafunzi wengi wanakwenda katika madisco wakati wa sikukuu za Idd ambazo huwa ni mara mbili kwa mwaka, Madisco mengine yanayovuta wanafunzi wengi ni kama tamasha la Mwaka Kogwa ambalo hufanyika mara moja kwa mwaka na Tamasha la nchi za Majahazi. Zaidi wanafunzi huonekana kwenye maonyesho ya Muziki wa Kizazi Kipya. Madisco yote haya hufanyika kuanzia saa za maghalibi hadi usiku wa saa nne.

Katika kuona kuwa wanafunzi wa Visiwa hivyo wanafanya vizuri SMZ imo katika mipango ya kutenganisha wanafunzi kwa kuweka shule za jinsia moja tu. Mpango huu umeshaanzishwa kwa baadhi ya shule visiwani humo kwa lengo la kuwafanya wanafunzi hao wasome na kufaulu na sio kutongozana.

Mwaka jana Visiwa hivyo vilishuhudia amri ya kuwataka wanafunzi wa chuo cha "Zanzibar University College" kutochanganyikana(wanaume na wanawake) wakati wa kujisomea usiku, kwa madai kuwa chuo kimezagaa na kondomu zilizotumika!

Hatua za SMZ kutaka kuona kunakuwepo na matokeo mazuri ya mitihani kwa wanafunzi wake zichukuliwe kufuatana na mapendekezo kadhaa yaliyokwisha kutolewa huko nyuma. Kwanza SMZ imekwisha shauriwa mara kadhaa kuhusu kubadilisha mitaala yake ili iendane na ya Tanzania bara. Hata hivyo hadi sasa SMZ wanaonekana kuwa bado kuwa tayali kufuta pendekezo hilo, licha ya kujua manufaa yake kwa wanafunzi na wanakisiwa hicho kwa ujumla. Kinacho zuia kutofuatwa kwa pendekezo hilo hadi leo hakijulikani. Zaidi ni kwa serikali hiyo kuibuka na viamri vya ajabu ajabu kila kukicha! Kitendo cha kupiga marufuku marufuku hizi husababisha kuwafanya wanafunzi kuwa watukutu zaidi.

Kwa upande mwingine Wazazi nao wanapaswa kushirikishwa katika kila hatua ya maendeleo ya wanafunzi wanapokuwa shuleni na majumbani. SMZ inapaswa kushirikiana na wazazi kuona ni kwa kiwango gani wataweza kuongeza bidii ya wanafunzi katika masomo yao. Malezi bora kwa mwanafunzi husaidia kwa kiasi kikubwa kwa mwanafunzi kuwa na bidii katika masomo yake.

UNCEF wanathibitisha hilo kwa kuwa hata nchi zenye utajili mkubwa iwapo wanafunzi wake wanakosa malezi bora matokeo ni kufanya vibaya shuleni.

http://news.bbc.co.uk/2/hi/uk_news/6359363.stm