Thursday 10 February 2011

HARUSI TRADE FAIR 2011 - MAONYESHO YA HARUSI 2011



Maonyesho ya Harusi kufanyika Dar.
Wadau wa Harusi kukutanishwa Dar
Siku tatu za Maonyesho ya Harusi Diamond Jubilee
Maandalizi ya Maonyesho ya Harusi 2011 yapamba moto Dar



Maandalizi ya maonyesho ya pili ya Harusi Tanzania ‘Harusi Trade Fair 2011’, yanayotarajiwa kuanza tarehe 1- 3 mwezi ujao katika ukumbi wa Diamond Jubilee yanaendelea vizuri , huku yakiwa yanajumuisha wataalamu waliobobea katika nyanja zote zinazohusiana na suala zima la Harusi.

Muaandaaji na msimamizi wa maonyesho haya makubwa ya Harusi Tanzania, Mustafa Hassanali amesema kuwa “maonyesho ya mwaka huu yatakuwa makubwa, mazuri na yenye kuvutia zaidi ya mwaka uliyopita, na tunatazamia kuyafanya yawe maonyesho makubwa zaidi kwa ukanda huu kwa miaka ijayo”

Nukuu zinasema kuwa, maonyesho ya mwaka huu tayari yameshawavutia zaidi ya washiriki 32 , wakiwemo washiriki wa maonyesho yaliyopita na wapya.

Maonyesho ya Harusi ya mwaka 2011, ni maonyesho ambayo uboreshaji wake umevuka kutoka siku mbili za maonyesho hadi siku tatu kwa mwaka huu, huku likiongezewa na kujumuisha vionjo vingi zaidi.

“Harusi ni tukio zuri, ambalo hutokea mara moja tu, huku likiunganisha familia na jamii pamoja, hivyo nia yetu ni kuwapa maharusi mahitaji yao yoote muhimu kwa pamoja na kwa wakati mmoja, na maonyesho haya ndio sehemu muafaka kwa hilo” alisema Mustafa Hassanali.

Maonyesho haya ya Harusi ambayo hufanyika kila mwaka, huwaleta pamoja wahusika wote wa mambo ya Harusi katika kujenga na kutengeneza mtandao wa kimafanikio baina yao, na ndio maana maonyesho haya yamekuwa ni ya kwanza na ya aina yake Tanzania, ambapo kwa mwaka huu yatapambwa na vitu kama keki, maua, wapiga picha, magauni ya Harusi, bila kusahau mengi na yenye ubunifu katika Harusi.

Gabriel Makupa wa ‘GRM Production’, ambae ni mmoja wa washiriki wa mwaka huu wa maonyesho haya alisema kuwa, wamekuwa na wakati mzuri kibiashara, hali iliyosababishwa na ushiriki wao katika maonyesho haya kwa mwaka uliyopita.

“tumekuwa na wakati mzuri kibiashara, hii imetusaidia kujenga mtandao mzuri kibiashara, tulitangaza huduma zetu vilivyo, na hii ndo sababu ya sisi kushiriki tena mwaka huu” alisema Gabriel wa GRM, kampuni inayojihusisha na upigaji picha katika maharusi.

“makampuni yajitokeze kutangaza huduma zao mwaka huu katika maonyesho haya, ni nafasi nzuri, kwani tumeshapata makampuni 32 mpaka sasa yatakayoshiriki mwaka huu, idadi ambayo inaongezeka kila siku, “ alisema Mustafa Hassanali.

Mmoja wa washiriki wa mwaka huu wa maonyesho kutoka ‘Karibu Holiday’, kampuni inayoshughulika na maandalizi ya fungate kwa maharusi na mapumziko binafsi nchini, Bw. Susai Nathan alisema kuwa, maonyesho ya mwaka huu ni njia mbadala ya kutangaza huduma zao mpya zenye ubora maalum kwa fungate, mahususi kwa maharusi au watakaofunga ndoa katika miezi hii mitatu ijayo.

Haya ni maonyesho ya siku tatu ambayo yana mengi, na si yakukosa kushiriki ama kuhudhuria kwa maharusi, familia, na wale wote wanaohusika na kamati za Harusi, ili kujionea na kujua mengi yahusuyo Harusi na mahitaji yake.


Kwa maelezo zaidi tembelea hapa

No comments: