Tuesday 4 October 2016

Ashauri Mahari Ilipiwe Kodi ...



MWALIMU wa somo la biashara katika skuli ya sekondari ya Chasasa Wete Pemba Ali Hamad Nondo, amezishauri Mamlaka ya Mapato Tanzania ‘TRA’ na Bodi ya Mapato Zanzibar ‘ZRB’ kuchukua kiwango cha fedha (VAT) kwenye vyeti vya ndoa, ikiwa ni njia nyengine ya kukuza pato la taifa.

Alisema hata mahari nayo yamekuwa yakipanda siku hadi siku, na wakati wa kufungishwa kwa sunna hiyo, hutolewa cheti cha ndoa baada ya maharia kulipwa, hivyo ni yema kukawa na kiwango cha fedha kinachoingia serikalini.

Mwalimu huyo, ametoa ushauri huo alipokuwa akichangia mada kadhaa kwenye semina ya siku moja ya kuelezea umuhimu wa kulipa kodi, kwa wanafunzi na waalimu wa skuli hiyo.

Alisema kama bado TRA na ZRB hawachukua ‘VAT’ kwenye cheti cha ndo, wakati umefika sasa kufanya hivyo, maana kwenye taratibu hizo huwepo kwa cheti cha ndoa kutoka mamlaka za kiserikali.

“Mimi nauliza kwenye cheti cha ndoa kuna VAT, kama jawabu hakuna sasa anzisheni hiyo, ili mfuko wa serikali ukuwe, maana nayo mahari yanapanda kila siku’’,alishauri.

Akijubu hoja hiyo, Afisa Uhusiano wa Bodi ya Mapato Zanzibar ‘ZRB’ Khamis Makame Mohamed, alisema kwa sasa wao hawakusanyi hata shilingi moja kwenye cheti cha ndoa, ili kama jamii ikiridhia ni jambo jema.

“Hili ni jambo jema, sisi tutalichukua na kulifikisha kwa wenzetu, lakini kwa sasa pamoja na mahari kuonekana kupanda juu, lakini hatuna kodi, maana kwanza ni jambo la kiimani linataka ufafanuzi wa kina”,alieleza.

Nae Afisa Elimu kwa walipa kodi kutoka Mamlaka ya Mapato Tanzania TRA ofisi ya Zanzibar, Saleh Haji Pandu, alisema kwa sasa mamlaka hiyo, inakusanya ushuru wa forodha na kodi ya mapato pekee na wala sio kwenye cheti cha ndoa.

Mapema akizungumza kwenye semina hiyo, Afis huyo wa elimu kwa walipa kodi, aliwataka wanafunzi na waalimu hao kuwa wa mwanzo kuwadai risiti za bidhaa wafanya biashara mara wapato huduma.

“Nyinyi muwe mabalozi kwa wafanyabiashara kwamba mkishanunua bidhaa msisite kuwataka wawape risiti, maana kama hakutoa huyo ni ehemu ya kukwep kuliopa kodi.

Wakichangia mada kadhaa kwenye semina hiyo, washiriki hao walipendekeza iwepo taasisi moja pekee ya kukusanya kodi ili kuwapungizi usumbufu wafanyabiashara.

Mwanafunzi Yasseir Hamad Ali, alisema itakuwa jambo la busara kama kutakuwa na chombo kimoja cha kukusanya kodi ili iwarahisishie wanaopaswa kulipa kodi moja kwa moja.

Semina kama hiyo juzi walifanyiwa waandishi wa habari na wafanyabiashara kwa lengo la kukuza uwelewa wa ulipaji kodi kupitia TRA na ZRB.
………………………………..