Showing posts with label Flash blood. Show all posts
Showing posts with label Flash blood. Show all posts

Sunday 14 September 2008

Madawa ya kulevya na Zenj...Watoto matatani!




Matumizi ya madawa ya kulevya huko Zanzibar sasa yamechukua sura mpya ambayo ni mbaya sana na ya kutisha katika historia ya matumizi ya madawa hayo Visiwani humo. Athari za mwanzo kwa jamii ya visiwa hivyo ilikuwa ni pamoja na kuvunjika kwa ndoa, umalaya na wizi. Hatua ya sasa ni kuambukiza watoto wadogo virusi vya ukimwi kwa kuwachoma sindano zenye damu isiyo salama. Huu ni unyama wa aina yake kutokea huko visiwani.

Hadi kufikia mwaka 2001, Zanzibar ilikuwa tayali imepata umaarufu mkubwa wa kuwa bandari ya kupitishia madawa ya kulevya. Umaarufu huu ulisadikiwa kufunika hata umaarufu wa soko la watumwa uliotokea miaka mia mbili iliyopita. Ukuuaji wa biashara ya ya madawa ya kulevya katika Zanzibar ulikwenda sambamba na uporomokaji wa bei ya karufuu katika soko la dunia na kupanda chati kwa biashara ya utalii.

Awali, Zanzibar ilikuwa ni pepo ya wasafiri watumiao Bangi. Hii ilitokana na urahisi mkubwa wa kupatikana kwa bangi visiwani humo. Taratibu madawa mengine ya kulevya yalianza kuingia visiwani na kufikia kilele katika miaka ya tisini.

Zanzibar kuwa pitisho kubwa la madawa ya kulevya katika ukanda wa Afrika ya Mashariki, kunahusishwa sana na mabadiliko ya ya kiutawala huko Afrika ya Kusini, ambapo utawala wa kibaguzi ulifikia kikomo. Ulinzi mkali katika bandari ya Mombasa baada ya ulipuaji wa balozi za USA huko Nairobi na Dar es Salaam ni sababu nyingine inayotajwa ya Zanzibar kuwa kimbilio la kupitishwa kwa madawa hayo. Aidha ubinafishwaji wa Uwanja wa ndege wa Zanzibar katika miaka ya mwishoni ya tisini umetajwa kuchangia kwa kiasi kikubwa kukua kwa upitishaji wa madawa hayo katika Zanzibar.

Matumizi ya madawa ya kulevya yamekuwa yakienda pamoja na uongezekaji wa maambukizi ya virusi vya ukimwi. Hii hasa kwa wale wanaojidunga sindano. Uchunguzi unaonyesha kuwa asilimia 46 ya watumiaji wa madawa hayo hushare sindano, huku zaidi ya asilimia 50 wakifanya ngono (group sex na anal sex) ili kupata madawa hayo. Baadhi ya vijana huweza kutumia hadi US$ 240 kwa mwezi kupta madawa hayo.

Matumizi ya sindano yaliweza kuingia katika sura mpya katika miaka ya hivi karibuni, baada ya kuongezeka kwa watumiaji wasio kuwa na uweo wa kununua madawa hayo. Njia maarufu ya "flash blood" iligunduliwa ambapo mtumiaji wenye nazo mfukoni, hujidunga sindano yenye heroin, na akimaliza kijidunga ufyonza damu yake kutumia sindano hiyohiyo na kumpatia asie na uwezo damu yake ilichanganyika na heroin(diluted). Mchanganyiko huu uweza kumpatia nishai asiye kuwa na uwezo wa kununua herion.

Hali ya sasa ni mbaya mno kama si ya kutisha. Kwani watumiaji wa madawa hayo sasa hupita mitaani na kuwachoma sindano watoto wadogo, sindano hizo ni zile ambazo wanatoka kuzitumia kwa madawa yao ya kulevya, hivyo kuwepo na uwezekano mkubwa wa kuwapatia watoto hao maambukizi ya virusi vya ukimwi. Huu ni unyama mkubwa kabisa katika historia ya matumizi ya madawa hayo pamoja na ugonjwa wa ukimwi visiwani hapo. Kwa ufupi wazazi wengi wapo katika hali ya hofu na hasa wale wanoishi katika mitaa yanye vijana wengi wa kubembea, aidha kwa watoto ni adha kubwa mno kwao kwani inabidi kukaa ndani tu kwa usalama wao...