Tuesday 23 January 2007

Nungwi : Ukahaba, Nguo fupi na Ulevi hauna nafasi..

Linapokuja suala la ukahaba, Kijiji cha Nungwi huko Zanzibar kimekuwa mbele kukanya tabia hizo wazi wazi. Wamejaribu kutumia njia mbalimbali ikimemo maandamano, risala na kutimia viongozi wao katika kukemea tabia hiyo, hali hiyo ni tofauti kidogo na mjini Zanzibar ambapo makundi ya vijana hujichukulia sheria mkononi kuwahadhibu makahaba na wale wavao nguo fupi.
Hatua iliyochukuliwa mwanzoni mwa wiki hii na Kamati ya Maadili na Maendeleo katika kijiji cha Nungwi ya kutunga sheria ndogo ya kudhibithi uvaaji nguo fupi, ukahaba na ulevi inathibitisha ni kwa jinsi gani wanakijiji hicho hupenda kupita katika njia zinazokubalika katika kutoa kero zao.
Nikirudi nyuma na kuangalia kile kinachodaiwa kuwa ni ukahaba na mambo mengine yanayokwenda tofauti na maadili ya wakaazi wa Nungwi, yalianza mara baada ya kijiji hicho kukaribisha hoteli za kitalii. Kabla ya kuja kwa hoteli za kitalii kijiji hicho kilikuwa ni maarufu kwa uundaji wa majahazi na shughuli za uvuvi.
Miaka ya tisini ambayo ilikuwa ni ya mabadiliko makubwa katika sekta ya utalii visiwani huko, Waakazi wa Nungwi walishuhudia maandamo ya kinamama kupinga kuwepo kwa wanawake na wasichana toka mkoani Tanga ambao walidaiwa kuwepo huko kwa lengo la kufanya ukahaba. Wakinamama hao walidai wadada hao toka Tanga wamekuwa wakiwarubuni waume zao na kufanya nao mapenzi kwa pesa na kusababisha hali ngumu katika nyumba zao. Waliendelea kwa kusema uwepo wao hapo kutasababisha kuongezeka kwa ukimwi na kupolomoka kwa maadili. Hivyo waliwataka akinadada hao kuondoka mara moja kijijini mwao. Hatua yao hiyo ambayo iliungwa mkono na Mkuu wa Mkoa wa Kaskazini, ilizusha mjadala mrefu kuhusu nafasi ya Wabara katika visiwa hivyo. Zaidi ilionekana kuwa Watz bara wanazuiwa kutumia haki yao ya msingi ya kwenda popote pale ndani ya Tanzania pasipo bughuza. Hata hivyo maandamano hayo yalishuhudia kuongezeka kwa Watanga ambao sasa walihamia mjini na vijiji vingine vyenye hoteli za kitalii.
Nungwi hawakuishia hapo, wakanyosha vidole kwa wageni wengine ambao ni wafanyakazi wa mahoteli kwamba wanavaa nguo fupi na suruali za kubana. Kipindi hicho wafanyakazi wengi katika hoteli za kitalii huko walikuwa ni wananchi toka Kenya.
Hatua za Kamati hiyo ya kutunga sheria ndogo ndogo za kudhibiti uvaaji wa nguo fupi na ukahaba, ni hatua nzuri katika kulinda maadili yao. Hata hivyo kuna vitu kadhaa vya kujiuliza juu ya uhalali wa sheria hizo ndogo ndogo na hasa katika kuzisimamia na utekelezaji wake. Kimsingi kuhusu uvaaji wa nguo fupi, kamati hiyo inawataka wale wote wavaao nguo fupi kuvaa vazi la Kizanzibari. Vazi la kizanzibari kwa ufahamu wangu ni kuvaa kanga zaidi ya mbili, huku ukiwa umefunika sehemu zote za mwili na kuachia sura tu. Sheria hii inaweza isikubalike kwa wengi wa wafanyakazi katika hoteli hizo ambao sio wenyeji wa zanzibar.
Na iwapo vazi la kizanzibari ni kama lile la kuvaa baibui na hijabu yake, basi sheria hiyo itakuwa inalenga zaidi maadili ya kidini kuliko maadili ya kizanzibari, na itakuwa sio kosa kuhoji kauli ya serikali ya kusema kuwa nchi hiyo si ya kidini. Na kwanini wananchi ambao sio wa dini fulani washurutishwe kuvaa baibui?
Ofisi ya Mkuu wa wilaya ya Kaskazini ambayo ndio imepelekewa sheria hizo ili izibaliki, kabla ya Sheha na Wajumbe wake kuanza kucharaza viboko hadharani kwa dada zetu, itabidi iipitie vizuri sheria hizo kabla ya kuziruhusu kutumika. Lengo ni kuona haki sawa kwa waakazi wa kijiji hicho na kisiwa cha zanzibar kwa ujumla, inazingatiwa.

Sunday 21 January 2007

Mstakabala wa Soko la Usiku....

Wengine wamediriki kusema ni mojawapo wa kivutio cha watalii wawepo Zanzibar, huku wengine wakisema ni sehemu nzuri ya kwenda jioni iwapo huitaji kupika, na vijana wakipasha kuwa ni sehemu nzuri ya kukutana na marafiki wapya! Hiyo sio sehemu nyingine yoyote bali ni bustani ya Forodhani. Soko la chakula na vinywaji baridi wakati wa usiku.
Kwa miaka mingi eneo la bustani ya Forodhani limekuwa likitumika kwa shughuli mbalimbali, ikiwemo ya soko la lachakula kuanzia jioni hadi usiku. Jioni eneo hilo hilo hutumika kwa ajili ya michezo hasa mpira wa miguu na kuogelea. Muda wa maghahalibi ukifika eneo hilo hugeuka na kuwa soko. Miaka ya karibuni matumizi katika eneo hilo yamezidi kuongezeka, siku hizi asubuhi hadi usiku eneo hilo hutumika na wauza vinyago na batiki. sehemu nyingine hutumika kwa madereva kupumzika wakati wakisubiri wateja wao... hasa watalii.
Upanukaji wa matumizi ya eneo hilo kumeleta uharibifu mkubwa wa mazingira ya bustani hiyo. Aidha wingi wa watu watumiao bustani hiyo umezidi sana kiasi cha bustani hiyo ya Forodhani kuchakaa kwa kasi kubwa. Pamoja na kuzidiwa huko na wingi wa watumiaji bustani hiyo imeendelea kutumika kwa shughuli kupishana kutokana na muda wa siku, yaani asubuhi eneo linatumika hivi, mchana vile na usiku namna hii. Na inapotekea shughuli maalumu basi hutavutiwa muda muufaka ili isije kera shughuli zingine, na hasa soko la chakula....!
Uharibifu wa kwanza kuonekana katika bustani hiyo, ulitokana na wauzaji wa vyakula katika eneo hilo kuanza kupika ndani ya bustani. Hali ya bustani ikawa ni mbaya sana, hadi kufikia kufungwa. Baada ya kuafikiana na Manispaa ya Zanzibar, wafanyabiashara wa usiku walikubali kurejea mtindo wao wa awali wa kutopika katika bustani. Zaidi ni kuja na vyakula ambavyo vimekwisha pikwa tokea majumbani mwao. Tatizo lao likawa limepatiwa dawa.
Kwenye mikusanyiko ya watu hapakosi kadhia zake, wenye vipando hasa pikipiki, vespa na magari madogo, wakaona ni vema kuingia na vyombo vyao ndani ya bustani hiyo. Sijui ni nini hasa kilichopelekea watu hao kufanya hivyo. Vijia ndani ya bustani ambavyo vilikuwa ni maalumu kwa watembeao kwa miguu vikavamiwa na vyombo, haikuchukua muda navyo vikachoka. Mamlaka kama kawaida ikachukua hatua. Mara hii ikawa ni kuvipiga marufuku vyombo vyote ndani ya bustani.
Uchovu wa bustani hiyo sasa ukawa upo wazi kwa kila mtu kuuona, pasipo kujali kama ni mtaalamu au la.. Wanjanja vilevile wakaona hilo huku wakijua mapungufu ya mamlaka husika katika kutengeneza bustani hiyo. Wajanja hao wakatoa masharti yao ili kuweza kurejesha madhali nzuri ya bustani hiyo, ambayo sasa ilikuwa ni mojawapo ya vivutio vya utalii katika kisiwa cha Zanzibar. Sharti lao kubwa walitaka wapewe eneo la kufanyia biashara ndani ya bustani hiyo, aina ya biashara yao ni mgahawa. Bila ajizi Mamlaka husika wakatoa nafasi, Mgahawa ukajengwa na bustani ikafanyiwa matengenezo kidogo sana. Mgahawa ukashamiri na bustani ikaendelea kuharibika.
Bustani hiyo ina bahati ya kusimamiwa na zaidi ya Idara tatu kubwa za serikali, Kuna Manispaa ya Zanzibar, ipo Mamlaka ya Hifadhi na Uendelezaji wa Mji Mkongwe na Idara ya Mipango Miji. Mamlaka hizi zote zimekuwa zikishindana katika kusimamia bustani hiyo, na hasa linapokuja suala la uendelezaji wa bustani hiyo. Mamlaka ya Hifadhi na Uendelezaji Miji Mkongwe, chini ya sheria ya mwaka 1994, imekuwa ikidai ndie muhusika mkuu, huku Manispaa chini ya sheria ya mwaka 1995 nayo ikidai inapaswa kusimamia eneo hilo. Idara ya Mipango miji ikiendelea kutumia sheria yake ya mwaka 1985, imekuwa ikitaka kuhusishwa kwa kila kitu ndani ya bustani hiyo.
Idara hizo kila mmoja kwa wakati wake ilijaribu kupanga ni kwa namna gani eneo hilo litaweza kurudishwa katika hali yake hasa kimazingira. Manispaa kupitia Mpango wa Mji Endelevu waliona ni vema kufanyia matengenezo bustani hiyo. Lengo kubwa la Mji endelevu ni kuwashirika wadau wote wa bustani hiyo katika matengenezo ya bustani. Hii ni kwa sababu waliamini kwa kuwashirikisha wadau patakuwepo na uendelevu wa bustani. Mamlaka ya hifadhi na uendelezaji wao walikubaliana na Agha Khan kuifanyia matengenezo bustani hiyo na zaidi kuipanua. Wakati taasisi hizi mbili zikijadili nani afanye matengenezo, Ofisi ya Mkuu wa Mkoa ikaibuka na ufadhili toka kwa asasi ya Mke wa Rais wa Zanzibar(Karume) kuwa wapo tayali kuanza kuifanyia matengenezo bustani hiyo, chini ya maelekezo ya Manispaa.
Mamlaka ya hifadhi na uendelezaji mji mkongwe, wakaona iwapo watabariki matengenezo hayo watakuwa wanakwenda kinyume na Agha Khan, ambao wanampango wa muda mrefu wa kutengeneza bustani hiyo na kisha kuigawa upya. Hivyo wakashindwa kutoa idhini ya matengenezo. Manispaa ambao hukusanya mapato katika eneo hilo, wakaanza kufanya matengenezo kwa kasi ya konokono kupitia mfuko wa Mji endelevu, huku wakisikilizia ni nani ambae atapewa baraka zote kati ya Agha khan na asasi ya mke wa rais.
Hayo yakiendelea kwa upande wangu napenda kuwashauri kuwa uwamuzi wowote ambao utatolewa basi uwashirikishe moja kwa moja wadau wa eneo hilo. Matengenezo hayo yawe ni kwa faida ya wadau wa eneo, ambao wapo hapo kila siku. Na iwapo watashirikishwa katika matengenezo na kuhakikishiwa kuendelea kufanya biashara katika bustani hiyo, watakuwa na uchungu iwapo wataona bustani hiyo itaharibika, kwani kwa kushiriki kwao katika matengenezo ni njia mojawapo ya kuwafanya waithamini eneo hilo na kulienzi.

Thursday 18 January 2007

SMZ yafanya kweli

Kwa muda mrefu mifuko ya plastic nyepesi imekuwa ikitumika kwa wingi katika visiwa vya Zanzibar, kuja kwa mifuko hiyo kulitokana na kisiwa hicho kuwa kivutio cha pekee cha biashara katika afrika ya mashariki katika ile miaka ya tisini mwanzoni... Matumizi ya mifuko hiyo ilikuwa ni kwa bidhaa mbalimbali, aidha mteja hakupaswa kulipia chochote kwa ajili ya bidhaa yake kutiwa ndani ya mifuko hiyo.
Umaarufu wa mifuko hiyo ikashika kasi kiasi kwamba ikiwa sio lazima tena kwenda sokoni au dukani ukiwa na kikapu au mkoba. Umaarufu huo ukaongezeka hadi kufikia kwenye vyakula, sasa ikawa ukienda kununua mbatata za urojo huna haja ya kwenda na chombo chako kwani mifuko ya plastiki ipo. Ukishindwa kumaliza biriani yako hotelini, huna shaka kwani mifuko ya plastiki ipo, iwapo chakula kwenye sherehe au shughuli za misiba kikabaki na ukataka kwenda nacho nyumbani, mifuko ya plastiki ilikuwa ni karibu kuliko chombo chochote kile.
Wenye kuishi kwenye nyumba za ghorofa nao wakaja na udhuru wao, kuwa maji ni ya shida na kamwe hajafiki kwenye ghorofa zao! hivyo kuwafanya wapate shida kubwa linapokuja suala la kujisaidia iwe haja kubwa au ndogo. Njia mbadala ya karibu ikawa ni kutumia mifuko hiyo ya plastiki kukamilisha haja zao, na baade kuitupa chini.
Watumiao vyombo vya moto nao hawakuwa nyuma katika kutumia mifuko hiyo. Chombo kiliendeshwa hadi kwisha mafuta, baada ya hapo mtu hukimbilia kituo cha kuuzia mafuta na mfuko wake wa plastiki. Baada ya kuuziwa mafuta ya kuyatia chomboni mfuko hulembewa mbali pasipo kujali lolote.
Miaka ikaenda na ustawi wa mifuko ya plastiki ukashamiri, sasa ikawa kila baada ya hatua mbili utembeapo kwa miguu unakanyaga mifuko iliotupwa ya plastiki. Bustani, baraza na viunga vyote vikajaa uchafu wa mifuko ya plastiki. Kelele za mji kuwa mchafu zikapamba moto na Halmashauri ya Mji ikaonekana haifanyi kazi yake ipasavyo.
Serikali ikaliona hilo, semina, kongamano na warsha zikafanyika ili kujua athari za mifuko hiyo, Halmashauri kwa upande wake ikatunga sheria ndogo ya kudhibiti matumizi ya mifuko, ambayo haikuwahi kufanya kazi hata siku moja.
Baada ya miaka kumi na ushee sasa, serikali imeona na kuamua kulivalia njuga tatizo la mifuko ya plastiki nyepesi, na ni baada ya kuja na sheria kali dhidi ya matumizi ya mifuko hiyo. Ikiwa ni pamoja na kutumikia kifungu cha miezi sita jela au faini ya dola za kimarekani 2000.00.
Matumizi ya mifuko hiyo kwa zaidi ya miaka kumi kumesababisha uharibifu mkubwa wa mazingira ya kisiwa hicho pamoja na bahari ya Hindi. Ikumbukwe kuwa Taka maji ambazo huchanganyika na mifuko hiyo humwagwa kwenye bahari pasipo kuwepo na mchujo wowote ule, hivyo kuwepo na uharibifu wa maisha katika bahari.
Wafanyabiashara kwa upande mmoja wamekuwa mstari wa mbele kupinga kupigwa marufuku kwa utumiaji wa mifuko mepesi ya plastiki kwa kigezo cha serikali kupoteza mapato ilhali mazingira yakitetekemea. Uwamuzi wa serikali ni wa kuungwa mkono kwa dhati kuanzia kwa wananchi hadi kwa wafanyabiashara, kwani unalengo muhimu wa kuhifadhi na kutunza mazingira ya kisiwa chetu!

Tuesday 9 January 2007

Alijenga Baba na kamalizia Mtoto

Leo Wazenj na Watz wanasherekea siku ya Mapinduzi ya Zanzibar ukiwa ni mwaka wa 43. Mapinduzi hayo ambayo lengo lake kubwa ilikuwa kuwapa weusi wengi madaraka ya kujitalawa.

Tokea Mapinduzi kumeshapita awamu zaidi ya sita za uongozi wa ngazi ya juu kabisa visiwani humo, nikiwa na maana marais wa serikali ya mapinduzi, maarufu kama SMZ. Kila awamu iliingia na mambo yake waliyoona ni muhimu kwa wakati wao, zaidi kila awamu inakumbukwa kwa mazuri na mabaya waliyofanya.

Awamu ya kwanza ilikuwa na lengo la kuwawezesha wananchi walio wengi kuwa na maisha bora. Na hii ilithibitishwa na ujenzi wa nyumba bora katika kila pande ya kisiwa hicho. Juhudi za ujenzi huo zilifanyika kwa pamoja kati ya serikali na wananchi. Yaani wote walishiriki kikamilifu katika ujenzi wa nyumba tena wakitumia kila kitu katika kufanikisha azma ya serikali kuwapatia maakazi bora. Utaratibu uliotumika ni kuvunja nyumba ndogo ndogo zilizojengwa kiholela na kujenga nyumba kubwa za ghorofa. Mfano ni majengo ya Forodhani. Kwa upande mwingine nchi za ulaya nazo hazikuwa nyuma kuona wakaazi wa kisiwa hicho wananufaika, Ujerumani nao wakajenga nyumba za maendeleo katika mtaa wa Kikwajuni ambazo zilikuwa na kila kitu ambacho kinahitajika kwa maisha bora.

Awamu iliyofuata ikaona ni vema kuwa na nyumba nzuri vijijini vilevile, hivyo nayo ikajikita katika kujenga nyumba za vijiji huku wao wakitoa mafundi na vifaa vya ujenzi na wananchi wakifyatua matofali. Vijiji vikajengwa na wananchi wakahamia.

Awamu mbili zikapita pasipo kujishughulisha kabisa na masuala ya ujenzi wa nyumba, licha ya kuwepo na matatizo na kasoro nyingi katika ujenzi wa nyumba katika awamu zilizopita. Mojawapo ya matatizo ni kutomalizika kwa ujenzi wa Nyumba za Michenzani na baadhi ya nyumba za vijiji kukosa wakaazi. Aidha matatizo mabaya ya matumizi ya nyumba hizo na uchakavu wa nyumba. Mbaya zaidi ni kwa wale ambao walivunjiwa vibanda vyao kupisha majengo hayo waliendelea kusota pasipo kujua ni lini watanufaika na nyumba bora.

Awamu ya tano iliingia na aina mpya ya ujenzi wa nyumba, ambao uliitwa nyumba za mkopo nafuu, lengo likiwa ni ujenzi wa nyumba za kisasa kwa kuwauzia wananchi hasa wafanyakazi wa SMZ ambao wengi wao walikuwa hawana nyumba. Serikali ya Uchina ikajitutumua na kujenga nyumba za mkopo nafuu. Kasheshe ikaanza wakati wa ugawaji wa nyumba hizo, malengo yakapindishwa na waliopata wakapata na waliokosa wakakosa, malalamiko yakazidi na serikali kama kawaida yake ikaendelea kutoa ahadi kuwa zitajengwa zingine. Zaidi awamu hii ikachungulia na kule kwenye mabaki ya ujenzi wa nyumba za Michenzani. Wakajipanga na kumalizia block moja, wanainchi wakapata nyumba, kama vile haitoshi kukawepo na malalamiko kuwa nyumba nyingi wamepewa watu toka kisiwa cha pili.

Kuingia kwa awamu ya sita kukabadili kidogo sura ya ujenzi wa nyumba, wao wakaona ni bora kumalizia majengo ya Michenzani na kuwapa wale waliovunjiwa nyumba zao karibu miaka therathini na ushee! Wakawata watu hao kuwa wavumilivu kwani serikali haina fedha za kutosha ila nyumba zitamaliziwa.
Hapa sio kama zamani ambapo wananchi walishiriki ujenzi wa nyumba hizo. Sasa ikawa ni kazi ya serikali pekee kumalizia nyumba hizo. Pengine wananchi walishachoka kuisaidia serikali yao. Sijui.

Umaliziaji wa nyumba za Michenzani utakuwa ni furaha ya pekee kwa Rais Aman Abeid Karume. Kwani nyumba hizo zilijengwa na baba yake ambae alikuwa ndio rais wa kwanza wa SMZ. Pengine Karume ameshawishika kumalizia nyumba hizo ili kukamilisha ndoto za baba yake ambae alitaka kuona kuwa wananchi wake wanaishi katika nyumba zilizo bora kabisa. Aidha ni kuondoa kero za wale ambao walivunjiwa nyumba zao kwa mategemo ya kuishi kwenye nyumba bora, na kujikuta wakisubiri kwa zaidi ya miaka arobaini.

Mwisho napenda kuipongeza SMZ kwa kufikisha miaka 43.