Saturday 19 May 2007

Madeleine wa Zenj

Wengi wetu sasa tunajua kutoweka kwa Madeleine, mtoto wa miaka minne, raia wa Uingereza aliyetoroshwa huko Ureno yapata siku kumi na sita sasa. Vyombo vya habari na hasa vya hapa UK vimekuwa vikitoa maendeleo ya sakata hilo katika kila habari zao. Hivyo kuweza kuwafikia watu wengi kadiri iwezekanavyo. Leo wakati Fainali ya Kombe la FA, kati ya Man Utd na Chelsea, video ya dakika nne ya Madeleine inategemewa kuonyeshwa.Hivyo kuweza kutazamwa na watu zaidi ya nusu bilioni duniani kote.

Huko Zenj kuna mtoto wa kike wa miaka kumi na sita ameripotiwa kutoroshwa na mwalimu wake yapata miezi mitatu sasa. Jeshi la polisi visiwani humo limeomba kusaidiwa na jeshi la polisi la kimataifa(interpol) katika kumtafuta mtoto ambae jina lake ni Maryam Farid Said.

Tofauti ya Maryam na Madeleine ni kubwa sana, Madeleine ni mtoto mdogo sana asiejua hili na lile, wakati Maryam ni msichana mkubwa ambae anajua nini anafanya. Cha kusisimua zaidi ni kuwa Maryam hii ni mara yake ya pili kutoroshwa na wanaume.

Msichana huyo ambae alikuwa ni mwanafunzi wa shule ya binafsi ya bweni huko Bububu Zanzibar ana undugu na Rais wa Tanzania Jakaya M. Kikwete hivyo kuweka utoroshwaji wake kuwa wa mvuto zaidi. Polisi wa visiwani hapo wanashuku kuwa mtoto huyo atakuwa ametoroshwa na mwalimu wake ambae ni raia wa Uganda.

Iwapo mtoto huyo akipatikana, wazazi wake ambao sasa wanamtafuta, itabidi wamkalishe kikao mtoto huyo, kwani hii ni mara ya pili kutoroshwa hivyo kujenga hofu juu ya tabia yake kwa ujumla. Hapana shaka kuwa mtoto huyo anashirikiana na hao wanao mtorosha hivyo kufanya utafutaji wake kuwa mgumu zaidi. Zaidi nawatakia kila la heri Wazazi wa mtoto huyo katika jitihada za kumtafuta mwanao. Hali kadhalika wanachi ambao kwa namna moja ama nyingine ambao watakuwa na habari yoyote ya kuweza kupatika kwa mshichana huyo watoe ushirikiano wao kwa kutoa taarifa katika vyombo husika.

Wednesday 16 May 2007

Wazenj wa UK na Vituko Vyao...

Nilipofika hapa UK yapata mwezi sasa, nilikuwa na hamu kubwa ya kukutana na watz wanaishi huku, zaidi kuonana wa Wazenj wa huku ili niweze kubadilishana nao mawazo kuhusu vituko, vioja na kadhia kadha wa kadha za huko Zenj.
Well haikuwa kazi kubwa kabisa kuwatafuta wazenj, kwani nilipofika mwenyeji wangu alikuwa ametingwa sana na kazi zake za kila siku, hivyo alinitaka radhi kuwa hataweza kunipikia chakula cha jioni. "nikahisi sasa ndio kuna kulala na njaa" Hata hivyo alinitoa hofu kuhusu kupata kwa msosi, kwa kuniambia kuwa tayali ameshatoa oda ya msosi, ambao anahisi kuwa utanifaa na kunikumbusha huko bongo, na hasa katika soko la usiku la chakula huko Zenj(Forodhani).
Muda si mrefu tokea kuingia ndani kwa mwenyeji wangu, chakula cha jioni kikaletwa! MMhm nikaamini maneno yake, kwani ulikuwa ni msosi ambao nimeukasa kwa muda mrefu sasa... Chapati, samaki waliokaangwa kwa viuongo rukuki vya kisiwani, mchuzi mzito maandanzi, na mazagazaga mengine kibao.. ile harufu yake ilipofika puani mwangu, mate kibao yalijaa mdomoni. Baada ya kufakamia msosi ule wa jioni, mwenyeji wangu aliniambia kuwa umetoka kwa Wazenj ambao wao wamefungua mgahawa bubu wa kupika vyakula kwa order.
Asubuhi yake niliamua kuingia mitaani kuangalia hili na lile, baada ya kutembea tembea bila dira maalumu nilijikuta naingia kwenye sehemu ya kukatia nywele. Hapo niliamua kupunguza nywele zangu. Hata hivyo kulikuwa na watu wengi, hivyo nikabidi kusubiri. Vinyozi walikuwa kama wanne hivi wakiendelea na kazi zao... baadae walianza kuongea kwa lugha ya kiswahili yenye rafudhi ya mwambao, nikahisi hapana shaka watakuwa ni Wazenj, hivyo nikajiweka sawa kuwasikiliza. Hata nafasi ya kunyolewa ilipopatikana nilikaribishwa kwa lugha ya Kiingereza... mimi nikajibu kwa lugha ya Kiswahili. Nikanyolewa huku tukiongea hili na lile na hasa mambo ya Zenj. Nilipomaliza nikawauliza sehemu ambayo ninaweza kukutana na Watz wengi kwa wakati mmoja. Wakanielekeza.
Ni jioni, nikaamua kwenda kutembelea sehemu ambayo nitakutana wa Watz wengi kwa wakati mmoja. Ni baa maridadi kabisa na ya kisasa. Nilipoingia ndani ilikuwa imejaa watu kibao wa kila rangi. Baa ya kuchukua bia yangu, nikaanza kutafuta sehemu nzuri ya kukaa. Nikaona bora nokae karibu na meza moja iliyokuwa imejaa weusi kibao amboa walionekana wakifurahia vinywaji vyao ipasavyo. Nilipoangalia vizuri meza hiyo nikaona kuna kijana ambae niliwahi kuishi nae Malaysia ambae ni Mzenj. Nikamwita na kumkumbusha, kwani alionekana kunisahu. Baada ya kunikumbuka alinikaribisha kwa furaha tele kwenye meza yao. Akanitambulisha kwa rafiki zake, ambapo niligundua kuwa wote ni kutoka Zenj...Baada ya glass mbili hivi nikamuuliza kama kuwa Watz wa bara katika baa hiyo. Akanionyesha kwa kidole kuwa wamekaa kule... Well nikamwambia wacha nikawasalimu nao pia.
Baada ya kukaa kwa Wabongo kwa muda kadhaa nikahisi kuwa kuna kitu kinaendelea kati ya Wazenj na Wabongo... kwani ninapotoka sijawahi kuona utengano wa aina hii. Well sijui ni nani aliyeanzaa. Ila kwa haraka haraka nikahisi kuwa ni Wazenj ambao walikuwa na vituko ambavyo vimepelekea kuwepo na utengano huu... Hata hivyo nitazidi kuchimbachimba ili nijue vituko vyao.....

Thursday 19 April 2007

Uchafuzi wa Mandhari ya Bwawani Hotel

Bwawani Hotel ndio hotel pekee ambayo SMZ inaweza kujisifia kwa namna ilivyojengwa na huduma ambazo zinatolewa na hoteli hiyo. Hotel hii ilijengwa katika miaka ya 70, ikiwa na vyumba 118 kwenye jengo la ghorofa nne. Ipo umbali wa kilometa nane toka uwanja wa ndege na ni mwendo wa dakika tano toka bandarini.

Pamoja na vitu vingine vinavyopatikana katika hotel kubwa, hotel hii ina viwanja wa Tennis ndani na nje, swimming pool ya ndani, ukumbi wa michezo( game room) na bwawa zuri upande wa mbele ya hotel hiyo.

Leo ningependa kuzungumzia juu ya bwawa la hoteli hiyo, ambapo pengine ndio lililo zaa jina la Hotel Bwawani. Bwawa ambalo hadi hoteli inakamilika katika miaka ya sabini, ujenzi wake ulikuwa bado kukamilika, hivyo kuto toa madhari halisi ya hoteli hiyo.

Katika miaka ya themanini, wakati SMZ ikiwa inajichanganya kuamua kufuata mfumo gani wa serikali za mitaa, toka serikali za majimbo, kulijitokeza wawekezaji ambao waliona kuwa upo umuhimu wa kuendeleza bwawa hilo. Katika kipindi hicho tayali madhari ya bwawa hilo ilikuwa ni ya kuchukiza zaidi kuliko kuvutia. Majani maji yalikuwa yakiongezeka kwa kasi kubwa.

Mapendekezo yaliyotolewa na wawekezaji wa miaka hiyo ya themanini ni kuhamisha bandari ya yatch iliyopo kwenye bandari ya Malindi hadi kwenye bwawa hilo, kujenga ofisi ya Meja wa Halmashauri ya Mji wa Zanzibar(Town Hall) katika kingo za bwawa hilo, toka katika Ofisi ya Halmashauri ya Mji katika barabara ya Benjamin Mkapa. Ofisi hiyo ya Meya licha ya kuwa na ukumbi wa mikutano ya Madiwani, pia ungekuwa na club ya yatch zinazotia nanga Kisiwani hapo toka sehemu mbalimbali hapa duniani.

Wazo hili lilipo pelekwa kwenye vyombo vya SMZ lilitupwa kando, licha la kuwa wazo bora kabisa katika kipindi hicho hadi leo na mpaka kesho. Kwani kinachoendelea katika bwawa hilo hivi sasa ni uchafu mtupu. Kwa upande mwingine iwapo wazo hili lingefanyika katika siku zile, matatizo ya kisaikolojia yanayowakuta Madiwani na Meya wao sasa yasingekuwepo. Kuwachanganya Meya na Madiwani wake katika jengo moja na Watendaji wa Manispaa ya Zanzibar kumesababisha kuwepo na miingiliano ya kiutendaji kila siku katika Manispaa hiyo.

Ukiachana na adha za madiwani hao, bwawa hilo ni makaazi ya ndege watokao kaskazini ya dunia wakati wa msimu wa baridi huko kaskazini, hivyo iwapo bwawa hilo lingeendelezwa na kutuzwa vema tungeweza kujifunza mengi kuhusu ndege hao na zaidi kingekuwa ni mojawapo wa kivutio cha utalii. Lakini hili nalo halipo ndani ya mawazo ya watendaji wa SMZ!

Kumekuwepo na mawazo mengi toka serikalini na katika Halmashauri ya Mji juu ya kuendeleza bwawa hilo. Lakini yote kwa upande mmoja ni kuchakaza tu bwala hilo au kuliondoa kabisa.

Katika miaka ya tisini msikiti(Msikiti Mabluu) ambao uliondolewa ili kupisha ujenzi wa bwawa hilo, ulijengwa upya. Ujenzi wa msikiti huo ulikuwa ni kutoa mfano wa mradi mpya wa ujenzi wa nyumba katika muda mfupi. Ujenzi wa msikiti ulikamilika ndani ya siku saba na siku ya nane ukatumika. Mawazo ya ajabu ajabu yakazidi kumiminika, moja wa Mameja alipendekeza kuwa sehemu yenye magugu maji ijazwe kifusi ili kupatikane nafasi ya kuweka makontena ya biashara! Meya mwengine alikuja na wazo kuwa bwawa hilo litumike kuwa jaa kuu la taka.
Pengine waliokuwa wanajitahidi kuliweka bwawa hilo katika hali ya usafi ni wafungwa, ambao kila mwaka kwa mamia hupita hapo kukata magugu maji.

Miaka ya elfu mbili Waziri kiongozi alitoa amri ya wafanyabiashara wa vinyago na batiki wapewe eneo hilo kwa biashara zao, agizo likatekelezwa na madhari ikazidi kuwa mbaya. Hata hivyo kutokana na kuwepo kwa msikiti wauza vinyago walijikuta wakiondolewa hapo.

Ukarabati wa kusuasua wa Bandari ya Malindi umeligeuza tena bwawa hilo kuwa sehemu ya kuhifadhia makontena ya bandarini, hiyo kuendelea kuchafua bwawa na zaidi hata kuziba madhari nzuri ya mbele ya hoteli hiyo. SMZ inadai kuwa uwekaji wa makontena katika eneo hilo ni wa muda tu, na hata bandari itakapokamilika makontena hayo yataondolewa. Cha kujiuliza hapo jee vifusi na michanga iliyojazwa katika bwawa ili kutoa ya uwekaji wa makontena yataondolewa au utakuwa ni mwanzo wa kuzaliwa wazo jingine la kutokomeza bwawa hilo?

Kwa maoni yangu wazo lilitolewa katika miaka ya themanini ya kukamilisha ujenzi wa bwawa na ujenzi wa ofisi ya Meya pembeni ya bwawa hilo, lilikuwa ni wazo pekee ambalo lingeweza kulinusuru bwawa hilo kuwa kichaka cha mawazo duni ya viongozi wa SMZ. Aidha kungesaidia kuendeleza bwawa hilo na kuwa sehemu ya kuvutia kabisa katika eneo la Mji Mkongwe zaidi ya Forodhani.

Wednesday 11 April 2007

Tindikali kwa wauza kilaji Zanzibar

Sijui kisiwa kitaendelea vipi katika sekta ya Utalii kama wauzaji vinywaji vikali wataendelea kuteswa namna hii haya mambo yakuchanganya maswala ya kidini na uchumi hayana maendeleo yoyote Somalia mfano.




Wakala mwingine wa pombe amwagiwa tindikali

2007-04-10 10:28:44
Na Mwinyi Sadallah,Zanzibar

Wakala mwingine wa kusambaza pombe Zanzibar, Bw. Chadalal Javed, amemwagiwa tindikali usoni, muda mfupi baada ya kufungua duka lake lililoko mtaa wa Empire mjini hapa.

Kamanda wa Polisi mkoa wa Mjini Magharibi Bw. Bakar Khatib Shaaban alithibitisha kutokea kwa tukio hilo. Tukio hilo lilitokea jana saa 3:00 asubuhi.

Alisema kwamba mfanyabishara huyo mwenye asili ya Asia, alivamiwa na mtu asiyejulikana, muda mfupi baada ya kufungua duka lake.

``Ghafla mfanyabiashara huyo alimwagiwa kemikali na kumjeruhi sehemu za usoni na tayari amepelekwa jijini Dar es Salaam kwa matibabu zaidi,`` alisema Kamanda Bakari.

Alisema kuwa wakati tukio likitokea, mfanyabiashara huyo alikuwa dukani na mkwewe wakijiandaa kutoa huduma kwa wateja wao.

Alisema hata hivyo, polisi hawakufanikiwa kuchukua sampuli za kemikali iliyotumika, kwa vile baada ya tukio kutokea, wahusika waliharibu mabaki ya kemikali hiyo.

Kamanda Bakari alisema kwamba iwapo wangefanikiwa kupata mabaki ya kemikali hiyo, wangeweza kupeleka kwa Mkemia Mkuu kujua aina ya kemikali iliyotumika.

``Hatufahamu, aina ya kemikali iliyotumika,lakini tunaendelea na uchunguzi kwa kuwa mtu aliyefanya uhalifu huo alifanikiwa kukimbia baada ya tukio,`` alisema Kamanda Bakari.

Mfanyabiashara huyo anamiliki duka la Scorch Store, ambalo linatumika kusambaza pombe Zanzibar katika mahoteli ya kitali, baa na watumiaji wa rejareja Zanzibar.

Kamanda Khatib alisema hilo ni tukio la pili kutokea kwa wamiliki wa maduka ya pombe. Alisema mwezi uliopita mfanyabiashara mwenye asili ya Kiasia, Bw. Kirikti Mandala, alimwagiwa tindikali akiwa dukani kwake eneo la Michenzani.

Alisema kwamba katika tukio hilo watu wawili walihojiwa na polisi, lakini hadi sasa hakuna mtu aliyefikishwa Mahakamani kuhusiana na tukio hilo.

Hivi karibuni baadhi ya wanaharakati wa dini, wamekuwa wakilalamika kuongezeka kwa idadi ya baa katika manispaa ya Zanzibar, kitendo ambacho wanasema ni kinyume na mila na utamaduni wa Mzanzibari.

Mwezi uliopita wanaharakati hao, waliandamana kupinga ongezeko hilo la idadi ya baa katika mji wa Zanzibar, lakini hawakutoa takwimu za ongezeko hilo.

* SOURCE: Nipashe