Friday 30 January 2009

Wazenj na Mashairi




PONGEZI kwake Shamhuna, pamoja na Ali Mzee
SMZedi kujikuna, na kuridhisha wazee
Shabashi na kujivuna, Zanzibar isiteketee!

Zanzibar isiteketee, vigogo kuyabaini
Mwakanjuki atutetee, nahodha wa mapinduzi
Na Salmini tuletee, salamu za uzinduzi!

Salamu za uzinduzi, kutia ghera na moyo
Kumbukeni mapinduzi, ni kombozi si uchoyo
Zanzibar si Bata Shuzi, si Lindi si Bagamoyo!

Si Lindi si Bagamoyo, Dola ya Mwinyi Mkuu
Isikatwe yake roho, Dunga ... Unguja Ukuu
Nayo Pemba si Mohoro, imefungasha na Bweju!

Kufungasha na Bweju, Mafia na huko Kilwa
Lakini hayo ni makuu, Mrima kukaripiwa
Na tudai Siku Kuu, Zanzibar kuheshimiwa!.

Wednesday 28 January 2009

Walevi Tende kumbe wapo wengi...


Ziara ya Prez Kikwete kule PBA na Zenj ambayo imemalizika hivi karibuni, imeacha maneno mengi na hasa kutokana na hotuba zake ambazo alizitoa wakati wa ziara hiyo. Huku wengi akilidhika na yale yote ambayo alihutubia katika mikutano ya hadhara na wakati wa funguzi mbalimbali wa miradi, wachache wakiongozwa na chama cha maalim wameendelea kubeza kama kawaida yao.

Kwa upande wangu ziara hiyo ilikuja katika wakati muafaka kabisa na ni baada ya sherehe za Mapinduzi ambazo zinakumbuka Mapinduzi yaliyo zaa serikali ya walio wengi visiwani humo. Mapinduzi haya yalikuja mwezi mmoja baada ya Uhuru wa mashaka uliotolewa na Waingereza kwa Waarabu wachache na jamaa zao huko visiwani zikiwaacha wananchi walio wengi katika giza la kitwana. Historia ya mapinduzi hayo kwa sasa itakuwa inafahamika vizuri kwa kila mtanzania kwani imeshapita miaka 45 tokea yatokee na kila mwaka yamekuwa yakikumbukwa. Na hivi leo anapotokea mtu ama kikundi cha watu kuhoji ama kubeza mapinduzi hayo, inafaa umtizame mara mbili mbili kama tayali ameshapata vinibu kadhaa ama la!

Mwaka jana kuna kundi ambalo linadai kuwa linahusu Uhuru wa Zenj, ambalo liliamua kuadhimisha sherehe haramu za uhuru! Mpaka sasa sijajua walikusudia nini katika maadhimisho hayo, ingawa wao walikuwa na haya ya kusema

Akizungumza na waandishi wa habari jana, Kiongozi maandalizi ya sherehe hizo, Daud Jabil Seif, alisema wameamua kuadhimisha sikukuu hiyo ili kuwaenza waasisi wa uhuru wa Zanzibar wa mwaka 1963 ambao hawakumbuliwi na serikali.


Sasa hii maana yake ni nini kama sio kuanzisha chokochoko dhidi ya Mapinduzi ya mwaka 1964. Hapana shaka kabisa huu ni ulevi wa tende toka katika mtaimbo wa kwanza. Kwa zaidi ya miaka 40 imekuwa ikielezwa maana ya mapinduzi ya Zenj na kwa nini yalifanyika na kwa nini yataendelea kudumishwa.

Walevi wengine wa tende wanajaribu kuingiza mfumo wa vyama vingi na hatima ya Mapinduzi ya Zenj. Wao huku macho yao yakiwa mekundu kutokana na ulevi wa tende na asusa za mapera mchana wa jua la utosini huku wakivuja mijasho wanasema kuwa
Lakini kauli ambayo nataka zaidi kwa leo kumhusisha nayo Rais Kikwete ni ile ya kulileta tena suala la Mapinduzi ya Zanzibar ya 1964 na kama kawaida linapotajwa suala hilo malaika huwasisimka watu. Alisema haiwezekani kabisa kuchezea Mapinduzi hayo ambayo sasa yana umri wa miaka 45.

"Kama hajipendi ajaribu…kama hajitaki ajaribu…Yote chezeeni Mapinduzi hapana…ukiyachezea Mapinduzi unawarudisha watu kwenye utumwa, unawarudisha watu kwenye utwana. Hili liliondoka Januari 12, 1964 na halitarudi tena….haiwezekani."



Hiyo ndio kauli aliyoitoa Rais Kikwete ambayo inanifanya nijiulize masuala chungu nzima na hasa kuhusisha kauli hiyo na suala zima la demokrasia na ushiriki wa kisiasa hapa Zanzibar.


Mlevi huyu amesahau kuwa vyama vingi vimekuja baada ya Mapinduzi na vimeidhinishwa na Baraza la Wawakilishi ambalo ndio utunga sheria kwa serikali ya mapinduzi. Hapana shaka mlevi huyu ambae ni mwandishi wa makala kadhaa, bado ana faida za tende na kusahau kuwa Chama chochote cha siasa ambacho kitashindwa kuyatambua mapinduzi ya Zenj hakina nafasi ya kutawala huko Zenj. Maalim na madevu yake alijaribu mara kadhaa na joto lake ameliona na sasa amefyata mkia. Hata hivyo sio rahisi kuaminika kwani jamaa wale walipelekewa tu taarifa za Mapinduzi hivyo hawajui uchungu wake... Na Wengi wanajua kuwa Uchungu wa mwana aujuae mzazi

Pamoja na mambo mengine Prez JK aliwaambia waziwazi wale wote ambao wanabeza maendeleo ya SMZ na JMT katika visiwa hivyo ni sawa na walevi wa tende, kauli ambayo naona inawafaa sana maruuni hao.

Wednesday 14 January 2009

Tukiwa bado kwenye wiki ya Sherehe za Mapinduzi



Wakati tuneendelea kujadili hotuba ya Mhe Prez wa Zenj wakati wa shehere za miaka 45 ya Mapinduzi na yale yote yaliyojili katika sherehe hizo,ambapo kama kawaida yamezua mazungumzo marefu sana sehemu mbalimbali hapa duniani...

Leo hebu tuangalie jina la mtaa maarufu wa Darajani, Jina hili limetokana na kuwepo na daraja katika eneo hilo. Zaidi daraja hilo lilikuwa limepambwa na taa za umeme na kulifanya kuvutia sana na kupitika hata wakati wa usiku. Kumbukumbu za kuwepo na taa hizo inakwenda nyuma mwanzoni mwa miaka ya 1900.

Hali ya sasa hapo darajani inasikitisha sana, umaridadi wake umepotea na imekuwa ni kadhia tu kupita katika mtaa huo sio mchana wala usiku. Eneo la darajani ambalo limepakana na barabara ya Benjamin Mkapa(greek road), kwa sasa halina taa na linategemea taa zenye mwanga hafifu toka kwenye maduka na makontena,huku yakiongezewa nguvu na kandiri za wauza vitambaa.

Kama kawaida sababu tele za kujaza pakacha la mkaa zinaweza kutolewa kutokana na uchakavu wa eneo hilo, pasipo kutoa hatua madhubuti ambazo zinaweza kuchukuliwa japo kuboresha eneo hilo maarufu kwa biashara.

Labda tuwasubiri Agha Khan wakimaliza kukarabati soko la chakula la jioni, labda watawakumbuka wauza vitambaa wa hapo darajani. Maanake sio Manispaa ya Mji wala hao wenye Mamlaka ya Hifadhi na Uendelezaji wa Mji Mkongwe wenye nia na uwezo wa kuboresha eneo hilo.

Thursday 6 November 2008

"Migogoro ya Kisiasa katika SMZ"- Hayo ni Mavuno...

Hivi karibuni Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Kiongozi, alinukuliwa akisema kuwa migogoro ya kisiasa katika SMZ imekuwa chanzo cha ucheleweshaji wa mipango ya maendeleo ya wananchi wake. Kauli hii sio ngeni miongoni mwa wananchi wa visiwa vya Zenj hali kadhalika kwa maelfu ya watendaji wa vyombo mbalimbali ya SMZ. Migogoro inayozungumziwa na Mhe. huyo ni matokeo ya sera za umimi na uwale zilizozaliwa wakati Visiwa hivyo vilipoanza kuingia katika mfumo wa vyama vingi mapema katika miaka ya tisini.

Siasa katika vyombo vya SMZ ilikuwa ni kwa manufaa ya chama tawala, hii ni kwa watendaji wote kuanzia wa ngazi za chini hadi za juu. Kila mfanyakazi aliaminika kuwa ni mwanachama wa chama tawala na ameajiliwa ili kutekeleza sera za chama. Hii ilikuwa inadhibitisha na ushirika wa asasi za SMZ katika shughuli za kichama ambapo ilifikia hatua za kufunga ofisi kabla ya muda wake ili kutoa nafasi kwa wafanyakazi kushiriki katika mikutano ya hadhara ya chama tawala. Nahisi katika kipindi hicho hadi sasa ni shurti uwe mwanachama wa chama tawala kabla ya makablasha yako ya uombaji kazi kujadiliwa.

Hata hivyo kuingia kwa mfumo wa vyama vingi kulibadilisha mtazamao wa wafanyakazi kuhusu umuhimu wa kuwa katika chama tawala ili kuendelea kuwatumikia wananchi. Mabadiliko haya yaliguza wafanyakazi katika ngazi zote. Wafanyakazi wa ngazi za juu ambao wengi walikuwa katika nyadhifa zingine chamani, huku wakipata misukumo toka chamani, bila kujijua walianza kupandikiza mbegu mbaya mno ndani ya vyombo vya SMZ.

Katika moja ya mikutano ya kampeni ya 1995 Kiongozi wa ngazi ya juu chamani na katika SMZ alitamka maneno ya kejeli mno kwa watendaji wa SMZ ambao wamehusu kisiwa cha pili. Hotuba yake hiyo ilijukuwa imejaa ubaguzi na shutuma nyingi kwa wafanyakazi na wananchi toka katika kisiwa cha pili haikuweza kujenga bali ilikuwa ndio mwanzo wa migogoro katika Idara zote za SMZ, ambapo Mhe. Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri kiongozi anazungumzia.

Nakumbuka siku mbili baada ya hotuba ile, mmoja wa mfanyakazi katika idara ya kutoa huduma ambae alikuwa ni rafiki yangu aliniambia kuwa pamoja na kuwa na mapenzi ya muda mrefu na chama tawala lakini maneno yaliyozungumzwa na kiongozi huyo ni matusi makubwa kwao watokao kisiwa cha pili, hivyo anajitoa rasmi katika chama tawala, na yupo tayali kwa lolote ambalo litamtokea kwa hatua hiyo yake.

Mbaya zaidi, baada ya hotuba hiyo wafanyakazi wengi waliohusu kisiwa cha pili ambao walionyesha mapenzi tofauti walijikuta wakipoteza kazi zao, wengine wakinyanyaswa na kutegwa kwa sababu za kisiasa tu na tena kwa sababu ya SMZ kuunganisha siasa na serikali.

Haya aliyozungumza Mhe. Waziri hayana kificho, kwani katika moja ya miafaka ilikubalika kuwarudisha makazi wale wote ambao walifukuzwa kazi kwa tofauti za kisiasa. Ni wajibu wake iwapo anataka kuona migogoro hiyo inakwisha kuchukua hatua za vitendo katika kuona kuwa siasa katika Idara za SMZ zinawekwa kando, ikiwa ni pamoja na kuwarudisha wale wote ambao walitimiliwa kwa ajili ya mitazamo yao ya kisiasa. Kwa upande wa ajila mpya zisiangalie siasa bali uwezo wa mfanyakazi.

Zaidi Mhe anatakiwa kuona kuwa utengano katika idara za SMZ unakwisha ili kuweza kuongeza kasi ya kutoa huduma na kuleta maendeleo kwa wananchi wa visiwa hivyo.