Wednesday 15 April 2009

Zenj kuondokana na mafuta ya kwenye Rambo




Japo mtaalamu wa uchunguzi wa kuwepo kwa mafuta katika visiwa vya Zenj alisema mafuta katika visiwa hivyo hayatoshi kwa uchimbaji wa kibiashara, Wawakilishi walimjibu kuwa hata kama ni kidogo kwa ujazo wa kinibu, mafuta hayo ni kwa ajili ya Wazenj na watagawana hivyohivyo! Mbaya zaidi kwa mtaalamu huyo kupendekeza kuwa mafuta hayo yawe chini ya Muungano, jambo ambalo lilizua jambo lingine kwa mahasimu wa siasa visiwani humo kukaa pamoja na kupinga kwa nguvu zote kauli ya mtaalamu huyo aliyejikusanyia vijisenti kadhaa baada ya kukamilisha ripoti yake.

Kadhia ya upitikanaji wa mafuta visiwani humo imekuwa ya muda mrefu licha ya kuwepo kwa vituo vya kutosha kwa ajili ya uuzaji wa mafuta hayo. Watumia vyombo wanajua usumbufu mkubwa wanaoupata wakati bidhaa hiyo adimu inapokosekana visiwani humo.Kiasi cha kufikia kununua mafuta vichochoroni tena yaliyohifadhiwa katika maplastiki na vifuko vya Rambo.Usumbufu huu hauishii kwa wenye vyombo tu bali utambaa na kuenea kwa kila mwananchi wa visiwa hivyo kwa namna moja ama nyingine.

Kauli ya Waziri Mansoor Yusuf Himid katika suala la mafuta aliyoitoa hivi karibuni, inabainisha wazi kuwa serikali ya muungano wa tz(SMT)kupitia shirika lake la TPDC limekuwa likifanya uchunguzi na utafutaji wa mafuta katika visiwa vya Zenj kinyume na makubaliano ya ndoa...Muungano wa Tanganyika na Zenj. TPDC kwa zaidi ya miaka kumi sasa imekuwa ikiingia mikataba na kampuni za uchunguzi wa mafuta katika maeneo ya kujidai ya visiwa hivyo kana kwamba suala la mafuta ni la Muungano. Wawakilishi kwa upande wao walisimamia kidete kuzuia TPDC kunusanusa uwepo wa mafuta katika visiwa hivyo, huku wananchi wa visiwani wakisuburi kwa hamu kujua ubavu wa SMZ dhidi ya SMT.
Waziri Mkuu wa SMT Mizengo Pinda, kwa kuona kuwa kuna tatizo hapo amekubaliana na Waziri Kiongozi wa SMZ Nahodha kuwa mafuta katika Zenj yafanyiwe uchunguzi na wazenj wenyewe na kuweza kuyachimba wao wenyewe hata kama ni kidogo kwa kuweza kujipaka mwilini kwa siku mbili tu. Ingawa kaurusha mpira kwenye Bunge la Jamhuri ya Muungano ili kutoa kauli ya mwisho juu ya mstakabala wa mafuta.

Kinachoshangaza hapo ni kwanini suala hili lipelekwe kwenye Bunge ilhali Bunge hilo haliyawahi kukaa hata siku moja na kusema kuwa mafuta ni suala la muungano? zaidi ya watendaji wa SMT kwa utashi wao binafsi kuliingiza suala hili ndani ya Muungano! Hiki ni kichekesho kikubwa katika kadhia za Muungano huu!

Kinachofurahisha ni jinsi gani SMZ mara hii ilivyoweza kukataa kuburuzwa na SMT. Kuna mambo mengi ambayo SMZ imekuwa ikipelekweshwa mbio na kuna mengi ambayo yamekuwa yakiingizwa kwenye SMT pasipo kuwashirikisha wazenj, ambapo uhambulia taarifa tu kuwa jambo fulani lipo kwanye Muungano!

Ili kulinda na kuendeleza Muungano huu ni vema kwa SMT kuacha tabia yake ya muda mrefu ya kujichukulia uwamuzi pasipo kuwashirikisha wenzao wa SMZ. Ni vema wakakumbuka kuwa Muungano huu ulifikiwa kwa makubaliano ya nchi mbili tena kwa mambo kadhaa na sio sahihi kuongeza mambo mengine bila ridhaa ya upande pili. Hali kadhalika SMT waache kujisahau kuwa wana nafasi sawa na SMZ katika hatima ya muungano huu na hivyo ni vema wakawa na heshima!

Tuesday 7 April 2009

Leo ni siku ya Karume


Watanzania leo wanaungana na ndugu zao wa Zenj katika siku hii muhimu ya kumbukumbu ya A.Karume rais wa kwanza wa Zanzibar na Muasisi wa Muungano wa Tanganyika na Zanzibar.

Wednesday 25 March 2009

Huu Ndio Wakati Muafaka wa Kumiliki gari la Waziri wa SMZ


Mara kadhaa nimewahi kuandika juu ya ubabe wa SMZ dhidi ya Mahkama za Zenj, zaidi ya SMZ hata wananchi wakati mwingine wamekuwa na ubabe dhidi ya maamuzi ya Mahkama za Zenj. Kumekuwepo na hukumu mbalimbali kila siku, ila zinazonipa mashaka ni zile hukumu za kesi za madai. SMZ kama mhimili wa Mahkama imekuwa kwa mara kadhaa ikishitakiwa katika kesi za madai kutoka na ubabe wake wa kushindwa kufuata sheria zake.

Kesi nyingi ambazo SMZ na asasi zake zimekuwa zikijikuta matatani zinatokana na matatizo ya ardhi na madeni yanayotokana na huduma mbalimbali wanazoomba kufanyiwa na hatimae kushindwa kulizipia. Mwaka 2006 niliwahi kuandika jinsi gani Mahakama za Zenj zinapoonja ubabe wa SMZ na wananchi wake kiasi cha mtu kujiuliza iwapo utakuwa na matatizo ambayo yanahitaji haki kutendeka utakimbilia wapi!

Mwaka huo wa 2006 kulikuwa na kesi mbili za muda mrefu ambazo zilipata hukumu yake, lakini zikakutana na ubabe wakati wa utekelezaji wake, kama inavyoelezwa kwa kirefu chini ya bandiko la "Mahakama za Zenj na Matatizo ya Ubabe"

SMZ kwa kujua au kwa makusudi kabisa imekuwa ikipuuza madai mengi ya wananchi wake dhidi ya asasi yake. Nakumbuka kesi nyingi katika hili lakini moja iliyonivutia ni ile ya asasi moja ya SMZ kuibeza amri ya Mahkama kuhusu uvunjaji wa mabanda ya biashara ili kupisha ujenzi wa soko katika eneo la Mwanakwerekwe.

Wengi wa wananchi wamekuwa na madai mbalimbali na wanapokimbilia katika vyombo vya SMZ ili kupata suluhisho, uvunjika moyo jinsi wanavyosumbuliwa na inahitaji moyo wa ziada kwenda Mahakamani ambako ni sawa na kumpa Nyani kesi ya Ngedere. Binafsi nimekuwa nikipigwa tarehe zaidi ya miaka tisa kwa madai ya haki yangu ambayo niliingia mkataba na SMZ.

Hatua ya Mahakama Kuu kupiga mnada magari ya SMZ kwa kushindwa kulipa deni lake la matengenezo ya ikulu ndogo huko Pemba ni ya kuungwa mkono sana. Amri hii iwapo itafanikiwa itakuwa ya kuigwa na kupigiwa mfano. Moja ya mali ambayo inaweza kupigwa mnada ni gari la Mh. Waziri ambae wizara yake inahusika moja kwa moja na kushindwa kufuata taratibu za kuheshimu mikataba. Nategemea jeshi la polisi visiwani humo kusimamia vizuri ushikwaji wa mali hizo za SMZ na hatimae kupigwa mnada. Hii inaweza kuondoa usingizi mzito kwa watendaji wa SMZ kuhusu kuheshimu mikataba wanayoingia.

Tuesday 24 March 2009

Agha Khan na Mji Mkongwe....

Agha Khan Development Network kwa zaidi ya miaka kumi sasa imekuwa ikifanya ukarabati mkubwa katika baadhi ya Majengo ya Mji Mkongwe wa Zanzibar. Na hivi karibuni walikuwa katika hatua za mwisho mwisho za kukamilisha ukarabati wa Forodhani Park.
Leo nitaangalia majengo mawili, nikianzia na Stone Town Culture Centre maarufu kama Old Dispensary ambalo ni mojawapo ya majengo yaliyofanyiwa ukarabati na AKDN baada ya kutupwa na SMZ. Aidha jengo lingine lililolembewa na SMZ ni Extelcom, ambalo leo hii kuingia ndani ya jengo hilo inabidi uwe nazo mfukoni.

Old Dispensary.

Jengo hili ujenzi wake ulikamilika mwaka 1894 chini ya ushauri wa kihandisi toka Uingereza. Michoro na mafundi wa jengo hili ni kutoka India ambako ndipo alipotoka mwenye jengo Bw. Tharia Topan ingawa hakuweza kuona kukamilika kwa ujenzi wa jengo hilo.

Mjane wa Topan aliweza kuendeleza ujenzi na baadae kuliuza. Lengo la Topan lilikuwa kujenga shule na zahanati, ambapo mmiliki wa mwisho wa jengo hilo aliweza kufanya sehemu ya chini ya jengo hilo kuwa zahanati na sehemu ya juu kuwa sehemu ya makaazi yake. Huu ndio ukawa mwanzo wa jina maarufu la Old Dispensary.

Miaka 70 baadae jengo hilo likawa tupu, na kuendelea kuwa tupu huku likiendelea kuchakaa na kuharibika ni hadi pale Agha Khan walipopewa ruhusa ya kulifanyia ukarabati ili kunusuru ufundi mkubwa uliotumika katika ujenzi huo kupotea na hasa nakshi zake za kihindi.


Miaka 100 baadae Agha Khan waliweza kupata kibali cha ukarabati wa jengo hilo, zaidi walipewa mkataba mpya wa kukodishwa jengo hilo na SMZ chini ya muda maalumu. Pichani hapo juu ni old dispensary baada ya kufanyiwa ukarabati mkubwa .


Extelcom
Jengo lingine ambalo lilikuwa chini ya SMZ na kuachwa bila aina yoyote ile ya usimamizi hadi pale walipotokea tena agha khan na kuamua kuligeuza toka ofisi hadi kuwa hoteli ya kitalii. Sasa jengo hili linajulikana kama Serena Inn