Tuesday 9 January 2007

Alijenga Baba na kamalizia Mtoto

Leo Wazenj na Watz wanasherekea siku ya Mapinduzi ya Zanzibar ukiwa ni mwaka wa 43. Mapinduzi hayo ambayo lengo lake kubwa ilikuwa kuwapa weusi wengi madaraka ya kujitalawa.

Tokea Mapinduzi kumeshapita awamu zaidi ya sita za uongozi wa ngazi ya juu kabisa visiwani humo, nikiwa na maana marais wa serikali ya mapinduzi, maarufu kama SMZ. Kila awamu iliingia na mambo yake waliyoona ni muhimu kwa wakati wao, zaidi kila awamu inakumbukwa kwa mazuri na mabaya waliyofanya.

Awamu ya kwanza ilikuwa na lengo la kuwawezesha wananchi walio wengi kuwa na maisha bora. Na hii ilithibitishwa na ujenzi wa nyumba bora katika kila pande ya kisiwa hicho. Juhudi za ujenzi huo zilifanyika kwa pamoja kati ya serikali na wananchi. Yaani wote walishiriki kikamilifu katika ujenzi wa nyumba tena wakitumia kila kitu katika kufanikisha azma ya serikali kuwapatia maakazi bora. Utaratibu uliotumika ni kuvunja nyumba ndogo ndogo zilizojengwa kiholela na kujenga nyumba kubwa za ghorofa. Mfano ni majengo ya Forodhani. Kwa upande mwingine nchi za ulaya nazo hazikuwa nyuma kuona wakaazi wa kisiwa hicho wananufaika, Ujerumani nao wakajenga nyumba za maendeleo katika mtaa wa Kikwajuni ambazo zilikuwa na kila kitu ambacho kinahitajika kwa maisha bora.

Awamu iliyofuata ikaona ni vema kuwa na nyumba nzuri vijijini vilevile, hivyo nayo ikajikita katika kujenga nyumba za vijiji huku wao wakitoa mafundi na vifaa vya ujenzi na wananchi wakifyatua matofali. Vijiji vikajengwa na wananchi wakahamia.

Awamu mbili zikapita pasipo kujishughulisha kabisa na masuala ya ujenzi wa nyumba, licha ya kuwepo na matatizo na kasoro nyingi katika ujenzi wa nyumba katika awamu zilizopita. Mojawapo ya matatizo ni kutomalizika kwa ujenzi wa Nyumba za Michenzani na baadhi ya nyumba za vijiji kukosa wakaazi. Aidha matatizo mabaya ya matumizi ya nyumba hizo na uchakavu wa nyumba. Mbaya zaidi ni kwa wale ambao walivunjiwa vibanda vyao kupisha majengo hayo waliendelea kusota pasipo kujua ni lini watanufaika na nyumba bora.

Awamu ya tano iliingia na aina mpya ya ujenzi wa nyumba, ambao uliitwa nyumba za mkopo nafuu, lengo likiwa ni ujenzi wa nyumba za kisasa kwa kuwauzia wananchi hasa wafanyakazi wa SMZ ambao wengi wao walikuwa hawana nyumba. Serikali ya Uchina ikajitutumua na kujenga nyumba za mkopo nafuu. Kasheshe ikaanza wakati wa ugawaji wa nyumba hizo, malengo yakapindishwa na waliopata wakapata na waliokosa wakakosa, malalamiko yakazidi na serikali kama kawaida yake ikaendelea kutoa ahadi kuwa zitajengwa zingine. Zaidi awamu hii ikachungulia na kule kwenye mabaki ya ujenzi wa nyumba za Michenzani. Wakajipanga na kumalizia block moja, wanainchi wakapata nyumba, kama vile haitoshi kukawepo na malalamiko kuwa nyumba nyingi wamepewa watu toka kisiwa cha pili.

Kuingia kwa awamu ya sita kukabadili kidogo sura ya ujenzi wa nyumba, wao wakaona ni bora kumalizia majengo ya Michenzani na kuwapa wale waliovunjiwa nyumba zao karibu miaka therathini na ushee! Wakawata watu hao kuwa wavumilivu kwani serikali haina fedha za kutosha ila nyumba zitamaliziwa.
Hapa sio kama zamani ambapo wananchi walishiriki ujenzi wa nyumba hizo. Sasa ikawa ni kazi ya serikali pekee kumalizia nyumba hizo. Pengine wananchi walishachoka kuisaidia serikali yao. Sijui.

Umaliziaji wa nyumba za Michenzani utakuwa ni furaha ya pekee kwa Rais Aman Abeid Karume. Kwani nyumba hizo zilijengwa na baba yake ambae alikuwa ndio rais wa kwanza wa SMZ. Pengine Karume ameshawishika kumalizia nyumba hizo ili kukamilisha ndoto za baba yake ambae alitaka kuona kuwa wananchi wake wanaishi katika nyumba zilizo bora kabisa. Aidha ni kuondoa kero za wale ambao walivunjiwa nyumba zao kwa mategemo ya kuishi kwenye nyumba bora, na kujikuta wakisubiri kwa zaidi ya miaka arobaini.

Mwisho napenda kuipongeza SMZ kwa kufikisha miaka 43.

Sunday 31 December 2006

Mahakama za Zenj na Matatizo ya Ubabe

Mahakama za zenj katika ngazi zote kuanzia mahakama ya wilaya hadi mahakama kuu ya rufaa zimekuwa zikukutana na wababe ambao hupinga maamuzi ya mahakama hizo kwa muda mrefu sasa.

Tukio la hivi karibuni huko Kibeni katika mkoa wa Kaskazini linathibitisha kuwa maamuzi mengi ya mahakama yamekuwa hayakubaliwi na wanajamii na hasa yale ambayo yamekuwa yakihusisha ujenzi wa nyumba.

Zipo kesi nyingi kuhusu migogoro ya ardhi katika Zanzibar, kesi hizi nyingi zimetokana na kutokuwepo na uwazi katika sheria ya ardhi ya mwaka 1985. Kwa ufupi ardhi yote ya Zanzibar ni mali ya serikali na sio vipando katika ardhi hiyo. SMZ ndio yenye jukumu la kupanga na kugawa ardhi visiwani humo, na kutoa umiliki wa ardhi kwa mtu binafsi, taasisi, mashirika n.k

Kwa upande mwingine serikali hiyo hiyo imekuwa ikitambua baadhi ya hati miliki za ardhi ambazo zilitolewa kabla ya mapinduzi ya Zanzibar(1964) mwa madai kuwa ardhi hizo hazikuwahi kutaifishwa na kuwa mali ya serikali au zimetiwa wafku hivyo serikali haiwezi kuzitaifisha...! Sasa unaposema kuwa ardhi yote ya Zanzibar ni mali ya serikali huku ukijua kuwa sio kweli maana yake ni nini? ka si kupotosha ukweli na kujenga mazingira ya dhuluma!

Matatizo mengine ambayo yanachangia kuwafanya wananchi kuwa wababe dhidi ya maamuzi ya serikali na vyombo vyake, ni kutojulikana kwa wigo za kiutawala visiwani humo. Haijulikani ni wapi ardhi ya serikali inaanzia na wapi inaishia, hata hizo wizara zimekuwa kimya kuelimisha wananchi juu ya suala zima la ardhi.. Wananchi wameachwa kwenye giza huku watawala wakijua hilo pasipo kufanya lolote za ya kukurupuka pale yanapotokea matatizo ya ardhi kwa kutoa amri kubwa kubwa.

Ubabe wa wananchi katika kupinga Hukumu za Mahakama umetokea huko Shakani katika wilaya ya Magharibi mkoa wa Mjini/Magharibi na sasa zimehamia katika mkoa wa Kaskazini. Hii yote ni kwa sababu SMZ imeshindwa kusimamia sheria zake. Iwapo serikali hiyo ingekuwa wazi na hasa kwenye eneo la ardhi lenye migogoro mingi, hapana shaka kusingekuwepo na matatizo haya ya baadhi ya watu kukejeri na kupuuza amri za mahakama.

Kingine watendaji wa SMZ, kwa kujua mapungufu ya serikali wamekuwa ndio mashawishi wakubwa wa kuwepo kwa migongano ya ardhi. Aina hii ya undumilakuwili inatisha na inapaswa kufanyiwa kazi

Friday 29 December 2006

Watanzania wanapokutana

Mwaka huu unaokwisha kuwekuwepo na matukio mbalimbali yaliyoweza kukutanisha watanzania toka zaidi ya mji mmoja.. hapa chini ni mojawapo ya matukio hayo

Monday 25 December 2006

Zenj na visa vya ardhi mwaka huu....

Mwezi wa tatu 2006
Kuna kauli moja iliwahi kutolewa na rais wa awamu ya nne katika SMZ kuwa Zanzibar ni "Njema na kila atakae kuja basi anakaribishwa" Kutokana na kauli hiyo Zanzibar ilishuhudia mabadiliko ya nguvu katika sekta zote kuanzia ya kibiashara,kijamii na kadhalika. Mamia ya watu walianza kufanya biashara wageni wakiongezeka na kuufanya mji wa zanzibar kuwa mdogo kutokana na msongamano wa watu.
Kuingia kwa awamu ya tano kulishuhudiwa na mabadiliko makubwa zaidi,mabadiliko haya zaidi yalikuwa katika kuendeleza ardhi ya zanzibar. Hapa inabidi tukumbuke kuwa ardhi yote ya Visiwa vya Zanzibar ni mali ya serikali. Hivyo ili uweze kuendeleza ardhi hiyo ni shurti uwe na hati ya kumiliki ardhi hiyo toka serikalini. Katika awamu ya tano kulikuwa na wimbi kubwa la ujenzi wa nyumba za kuishi na mahoteli, kutokana na kuwa serikali ndio mmiliki wa ardhi kwa kiasi kikubwa ilishindwa kukidhi maombi mengi ya viwanja. Hili likawa ni tatizo kubwa na tena kubwa sana. Hadi mwaka huo tayali mji wa zanzibar ulikuwa unafuata mapendekezo ya mastertplan ya wachina ya mwaka 1982 iliyotiliwa nguvu na sheria ya upimaji miji na ardhi ya mwaka 1985.
Master plan hiyo iliongeza ukubwa wa mji wa zanzibar na ilikuwa imeshatenga maeneo ambayo serikali ilitakiwa kuyaendeleza aidha kwa kujenga nyumba au kugawa ardhi hiyo kwa wananchi wanaotaka kujenga nyumba. Hilo halikufanyika na kama lilifanyika basi ni kwa kiwango kidogo sana. Maeneo hayo yaliyopimwa na kuonyeshwa kwenye master plan ni pamoja na eka tatu ambazo zilitolewa na serikali ya awamu ya kwanza na ya pili kwa lengo la kuwapatia wananchi wa visiwa hivyo sehemu za kulima. Katika awamu hizo wananchi wengi walikuwa wanaishi katika maeno ya umbali wa maili tano kuzunguka mji.
Eka tatu karibu zote zilikuwa nje ya mji na ziliguswa na master plan. Kutokana na mabadiliko ya kiuchumi na mahitaji makubwa ya ardhi kwa ajili ya ujenzi, eka tatu taratibu zilianza kujengwa. Ilikuwa ni kazi ya ziada kujenga katika eka hizo ukizingatia kuwa ardhi ni mali ya serikali. Hata kupitia Mambo msige ambao wao pia wanatoa hati ya kumiliki mali, wananchi waliona huko ndiko kwepesi kwa kupata hati ya kumiliki ardhi.Hivyo wananchi walianza kujenga misingi ya nyumba katika heka hizo na baadae kuziuza na serikali kupitia idara yake ya mambo msige kuidhinisha na kuthibitisha uuzaji na uendelezaji wa ardhi hiyo ambayo awali ilikusudiwa kuwa ni ya kilimo.
Vita kati ya idara za serikali ukaanza taratibu kati ya idara ya Ardhi na Idara ya Mambo msige, huku serikali kuu ikikaa kimya. Leo katika kusoma gazeti nimekutana na kauli ya Waziri wa Waziri wa Maji, Ujenzi na Ardhi Bw. Mansour Yussuf Himid akisema kuwa smz itabomoa nyumba zote zilizojengwa kwenye eka tatu. Kauli hii kwa kweli imenitisha mno. Na ni kauli nzito sana kwa waelfu ya wakaazi wa Visiwa hivyo. Kwani kwa namna moja ama nyingine watakaoadhirika na bomoabomoa hiyo ni wengi, na ni kuanzia kwenye mahoteli yote ya kitalii yaliyojengwa baada ya mwaka 1985, viwanda na maelfu ya nyumba za kuishi.
Tutabomoa nyumba zilizojengwa kwenye ardhi za ekari tatu
zilizotolewa kwa
wananchi baada ya Mapinduzi,’’ alisisitiza Waziri
.

http://www.ippmedia.com/ipp/nipashe/2006/03/16/62186.html

Mapema mwezi wa nne 2006

Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imeagiza nyumba zote zilizojengwa katika vyanzo vya maji zibomolewe na watendaji wa serikali waliotoa vibali vya ujenzi walipe fidia hizo. Zaidi hapa..http://www.ippmedia.com/ipp/radio1/2006/04/14/64264.html

Mwezi wa nne 2006

Hatimae Waziri Kiongozi wa SMZ amebadili kauli yake juu ya ulipwaji wa fidia kwa nyumba zitakazobomolewa kwenye vyanzo vya maji.Sasa wale waliojenga nyumba hizo hawatalipwa fidia tena.... Zaidi ametupa lawama kwa watendaji wa SMZ kwa kuwa wavivu na mwenye upungufu mkubwa wa kiuwezo katika utendaji wa kazi zao...

Chanzo:http://www.ippmedia.com/ipp/nipashe/2006/04/17/64424.html