Wednesday 19 February 2014

Tanzania Improves Communication Link Between Mainland and Zanzibar.



Tanzania s government has switched on a new microwave link designed to improve communications between the mainland and the island of Zanzibar

The link supplements one from the main landline operatore, TTCL and was funded at a cost of US$1.6 million with support from Japan.

"We are now sure of effective communication in Zanzibar," the Minister for Communication, Science and Technology, Prof Makame Mbarawa at the inaugeration of the link.

"With this new link, people of Zanzibar will now communicate without hurdles," he said, adding that the project has been successfully completed.

Construction of the link started last year.


Source: Cellular News

Saturday 15 February 2014

Maoni ya Mzanzibari kwa Wajumbe wa Zanzibar Kwenye Bunge la Katiba

Enyi Waheshimiwa Wabunge,

Kama tunavyojua kuwa Bunge la Katiba linakaribia kuanza na nyinyi ndio munaokwenda kupeperusha bendera ya Zanzibar kwenye bunge hilo linalobeba mustakabali wa taifa hili kwa miaka mingi ijayo. Wito wangu wa kwanza kwenu ni kwamba muende mukaangalie maslahi ya nchi badala ya vyama vya siasa. Najua wito huu mumeshatolewa na wengi, na nyinyi wenyewe huwa kila mukipata nafasi munatwambia kuwa hivyo ndivyo munavyokwenda kufanya. Lakini mimi nikiwa Mzanzibari, nina wajibu pia wa kuwakumbusha tena na tena.

Ukumbi wa Bunge la Jamhuri ya Muungano ambao pia utatumika kama ukumbi wa Bunge la Katiba.
Ukumbi wa Bunge la Jamhuri ya Muungano ambao pia utatumika kama ukumbi wa Bunge la Katiba.

Jukumu lenu kubwa ni kuangalia namna madhubuti ya kutatua mfumo butu wa serikali mbili usio na mbele wala nyuma. Kwenye katiba hii, nyinyi hamuna kubwa zaidi ya hilo, maana mengine yaliyo nje ya hapo yameshaelezwa kwenye Katiba yenu ya Zanzibar.

Nendeni bungeni mukikumbuka kwamba si haki kwa Wazanzibari kuwazuilia Watanganyika kurejesha nchi yao itakayoongozwa na wao wenyewe kupitia bunge lao wenyewe, bajeti zao wenyewe na ukusanyaji wa mapato yanayotokana na jasho lao wenyewe.

Kumbukeni kuwa mfumo wa Serikali Mbili ndio umegeuka kuwa fitna baina ya jamii mbili zenye uhusiano mkubwa wa kidugu na uliodumishwa kwa misingi ya ufahamiano na heshima na sio utawala wenye malengo tafauti na azma nzima ya kuungana

Iangalieni Katiba ya Zanzibar kila mara mukiwa kwenye vikao vya bunge hilo. Ilindeni na muiheshimu. Musije mukaruhusu kuharibiwa kwa misingi ya Katiba hiyo.

Mabadiliko ya Katiba ya Zanzibar ya mwaka 2010 yameonyesha wazi kwamba Zanzibar ni nchi inayoongozwa kwa misingi ya mihimili ya serikali, bunge na vyombo vya sharia. Wakati Wazanzibari tulipoipitisha, hatukutaka kuweka kimeme katika hadhi ya Zanzibar kama nchi katika Muungano na tukaweka wazi madaraka hata ya kuigawa nchi kwa mhusika mkuu wa Serikali ya Zanzibar badala ya mfumo wa zamani wa kuomba ruhusa kwa mlango wa pili, kutoka kwa Rais wa Muungano.

Nyinyi hamuna uwezo wa kuiviza azma kama hii iliyomo kwenye Katiba yetu na ambayo iliidhinishwa na asilimia zaidi ya 60 ya wananchi. Nyinyi hamuwezi mukawa wa mwanzo kuuzuia upande wa pili kujichomoza kwa visingizo vya kuulinda Muungano. Muungano ulikuwepo na utakuwepo, pawe au pasiwe na katiba mpya, kwani misingi ya Muungano huu ni udugu na mafahamiano makubwa baina yetu, watu wa Tanganyika na watu wa Zanzibar.

Nendeni mukapinge hoja za matumizi makubwa katika Mfumo wa Serikali Tatu kwani ni dhaifu. Chukuweni data za mapato zilizokusanywa kutoka Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), Bodi ya Mapato ya Zanzibar (ZRB) na hata tafiti nyingi kutoka taasisi za ndani na nje ambazo zinaonyesha wazi mgawanyo wa mapato ya Muungano na nchi husika na hata uchangiaji wake katika shirikisho kuendana na hali halisi ya wakaazi na maeneo yao. Waulizeni wanaopinga Serikali Tatu, hivi mambo matano ya Muungano yatakuwaje ghali kuliko 32 ya sasa yenye kero lukuki?

Vunjeni hoja za kwamba wapenda Serikali Tatu ni wapenda madaraka, maana nayo pia ni potofu. Semeni kwamba Bunge la Shirikisho linalopendekezwa kwenye Rasimu ya Pili ya litakuwa na wajumbe 20 tu kutoka Zanzibar. Sasa hayo madaraka yanayopendwa na wapenda mabadiliko yako wapi, wakati leo hii Zanzibar ina takribani wabunge 100 kwenye Bunge la Muungano? Maana ubunge ni cheo na cheo ni madaraka kwa kuwa kwake na fursa za mwenye madaraka. Sasa je unapopunguza wajumbe, ni kupenda madaraka au kupunguza madaraka?

Huenda mukaambiwa kuwa hoja ni kwamba Bara nao watahitaji wabunge wao wa serikali yao. Ulizeni cha ajabu hapo ni kipi? Mbona hatujasikia kelele za kuwa Baraza la Wawakilishi, kwamba nalo pia lina gharama kwa Wazanzibari na Serikali ya Zanzibar? Wazanzibari wanalipa kodi kuigharamikia serikali, mahakama na baraza lao la wawakilishi. Waacheni ndugu zetu wa Tanganyika nao walipe kodi kwa ajili ya taasisi zao za utawala.

Urahisi wa mbili kwa tatu labda ni kwa mantiki ya hisabati tu, maana ni kweli mbili ni ndogo kuliko tatu katika mfumo wa mfuatano. Lakini kwenye suala la gharama, wasiwajie na maelezo ya mantiki ya hisabati bila ya ushahidi, kwani kwa kufanya hivyo watakuwa wanawatumieni nyinyi kuhahalisha uoza wa miaka 50, huku tukiendelea kujidanganya eti kunahitajika marekebisho madogo madogo.

Wakumbusheni historia ikiwa wameisahau. Kwamba marais waliotangulia kwa Zanzibar ni sita na kwa Muungano ni wanne. Hivi tuseme marais hao hawakuwa na hamu ya kweli ya utatuzi kwa miaka 50 hata ikawa kila mmoja anamrithisha mwenziwe kero bila ya utatuzi? Kimewashinda nini kwa muda wote huo, hata hii leo iwe rahisi kutatua hizo kero? Kwani serikali si ndio hii hii ya chama tawala, CCM?

Waonesheni ukweli ulio mbele ya macho yao lakini wasiouona. Kwamba hata ndani ya vyama vya siasa, ambavyo kikatiba ni vya Muungano, mfumo ni huu huu wa Tatu: vyama vina mwenyekiti mmoja na makamo wawili wa pande mbili, manaibu katibu wa pande. Kwa nini isiwe kwa mjengeko wa serikali?

Niwaambieni kitu kimoja, waheshimiwa wabunge wangu. Hizi kelele na khofu za gharama zinalengwa zaidi kwamba kutakuwa na rais wa pande mbili na rais wa shirikisho. Lakini wanapaswa kujua hao kuwa unapopenda boga, upende na uwa lake. Ikiwa wameutaka Muungano, wasikhofie gharama. Sisi Zanzibar, tuna wakuu wa serikali wanaotazamwa na serikali yenyewe. Sasa kwa nini iwe gharama kwa wakuu wa serikali ya Tanganyika kutazamwa na serikali yao wenyewe? Kwa nini wasiwaweke wakuu hao kuwa wachache tu wanaostahili kutokana na mamlaka na kazi zao kutazamwa na serikali ya shirikisho yenye mchango wa pande zote?

Wanaosema Zanzibar hatuwezi kuchangia Serikali Tatu, wambieni wawapeni hoja sio maneno matupu. Watumbatu hunasema “Mkono mtupu haulambwa.“ Musije mukatishwa na watu waliojivalisha majokho ya udaktari na uprofesa wa kila fani, wakawafanya kuwa mazuzu musioweza kuhoji.

Mukitaka kujuwa kuwa hao hawana hoja, angalieni upofu wa hoja yao ya mchango wa Zanzibar kwenye Muungano isivyoweza hata kuchanganuwa kwamba watu milioni 1.5 na milioni 44 ni tafauti. Kwamba uchangiaji wa Wazanzibari milioni 1.5 utakwendana na mambo matatu muhimu – idadi ya watu wetu, ukubwa wa maeneo na matumizi yetu katika taasisi husika.

Uchangiaji wa bajeti ya trilioni 400 usikutisheni. Munalotakiwa mufikiri kwanza ni kwamba kuna mantiki gani ya kupewa mapato ya 4.5% kutoka mgawo wa Muungano hata tushindwe kuchangia kwa mantiki ya namna hiyo hiyo? Waje na uthibitisho sio ngonjera zisizokwisha, maana sisi Wazanzibari tumeshachoka na kero za kujitakia. Tumechoshwa na chuki na fitna za kupandikizwa na mfumo butu wa sasa.

Wengine watawaambieni kuwa hoja ni kumuenzi Mwalimu Julius Nyerere. Waambieni basi ni bora wote warudi kwenye Vijiji vya Ujamaa na Azimio la Arusha. Waambieni warudi kwenye mfumo wa chama kimoja aliouunda. Waambieni Mwalimu Nyerere angelitunzwa zaidi kama kungeundwa serikali moja tu kwa vile ndio hasa ndoto yake na kauli mbiu yake ya “Mbili kwenda Moja”.

Watakeni wawapeni sababu za msingi za kuendelea na mfumo wa sasa, kwani sisi Wazanzibari wa wa kizazi cha leo ni watu wa kuhoji. Sisi sio wa mbembelezo wa asili za wazee wetu ikawa ndio sababu ya kukubali makosa tukayawacha yaendelee.

Pelekeni ujumbe wetu wa wazi kwenye Bunge la Katiba. Kwamba sisi Wazanzibari tumewatuma mukapitishe mfumo wa Serikali Tatu kama ulivyopendekezwa na Tume ya Jaji Warioba. Hapana shaka, mutatakiwa kuufanyia marekebisho hapa na pale kidogo, lakini kwa vyovyote hamutarudi hapa na mfumo huu wa serikali mbili ambao una kila chembechembe za watu wachache, wabinafsi, wanaofaidika nao.

Si tumeona wakati Baraza la Wawakilishi likizuia na kupinga ongezeko kubwa la mafao na mishara yao, Bunge la Muungano lilikubali ongezeko kubwa la mafao kwa wanaomaliza mihula yao? Hizi ndizo gharama tunazosema hatutaweza kuzibeba.

La mwisho kabisa, ninawanasihi kwamba nendeni mukidumisha heshima ya Zanzibar, Uzanzibari na Wazanzibari. Musije mukarogwa na mukarogeka na kirusi cha ufisadi kinachoimun’unya Tanganyika hivi sasa. Kwa mfano, kwa lipi kubwa munalokwenda hata kila mmoja kati yenu akalipwe posho ya shilingi 700,000 kwa siku? Laki saba hizo zinaweza kutumika kuwanunua na kuiuza tena Zanzibar kama ambavyo imekuwa ikichuuzwa siku nenda siku rudi.

Hapana. Nyinyi musije mukawa wachuuzi wa Zanzibar. Umma utawaona, utawalaumu. Utawahukumu.

Wakatabahu,

Farrel Foum Jr.

Thursday 13 February 2014

Makaburi ya Wakristo Mwanakwerekwe Yapo Hatarini Kutoweka....



Kumekuwepo na hujuma za makusudi za kuharibu eneo rasmi la makaburi ya kuzikia Wakristo wa Zanzibar, liliopo Mwanakwerekwe katika Wilaya ya Magharibi, Mkoa wa Mjini/Magharibi.

Ni muda mrefu sasa kumekuwepo na vitendo vya ovyo kabisa vinavyofanyika katika eneo la makaburi hayo. Vitendo hivyo sio rahisi kuviona vikifanyika katika maeneo ya makaburi ya dini zingine ambazo makaburi yao yamepakana na haya ya Wakristo.

Kama inavyoonekana kwenye picha hapo juu, kuna hujuma za kulifanya eneo hilo kama Jaa la taka, kuna watu kwa makusudi kabisa wameligeuza eneo hilo kama sehemu ya kucimbia mchanga kwa ajili ya ujenzi wa nyumba zao.

Aidha vijana na watoto wanaoishi karibu na makaburi hayo, wao wameona eneo hilo linafaa zaidi kwa kuchezea mpira, huku waakazi wengine waishio karibu wameligeuza eneo hilo kuwa barabara ya kupitishia vipando vyao juu ya makaburi, huu ni utaarabu wa pekee ambao unaweza kuonekana Zanzibar pekee hapa duniani.

Kama vile haitoshi, wapo waliogeuza makaburi hayo kama sehemu ya kupata materials kwa shughuli zao za ujenzi, ambapo ubomoa zege katika misalaba na mifuniko ya makaburi ili kupata nondo, kumegua vigae (tiles) au kuchomoa misalaba ya mbao. Zaidi sio ajabu kukutana na mifugo ikuchungwa makaburini hapo.

Wakati huu udhalilishaji wa maeneo ya makaburi ya Wakristo ukizidi kuota mizizi na kuonekana kama ni jambo la kawaida serikali imeendelea kukaa kimya tofauti na hatua wanazochukua kwa makaburi ya Waislamu.

Mwishoni mwa mwezi wa kwanza, kupitia kwenye Baraza la Wawakilishi, serikali ilisema kuwa imepanga kulitumia eneo la Kama liliopo Wilaya ya Magharibi kwa ajili ya kuzikia watu.

Mpango huo unachukuliwa kutokana na eneo la makaburi ya Waislamu yaliyopo Mwanakwerekwe kuelekea kujaa. Hata hivyo Wawakilishi hawakuwa tayali kuzungumzia udhalilishwaji na hujuma zinazofanyika katika eneo la makaburi ya Wakristo ambalo lipo jirani tu na hayo yalioadiliwa.

Upofu na ukiziwi wa serikali juu ya yale yanayoendela katika makaburi hayo, ni moja ya sababu kubwa inayowatia kiburi baadhi ya watu ambao wameamua kuyahujumu makaburi hayo ya Wakristo.

Ni vema kwa serikali kutokimbilia kutafuta maeneo mapya kabla ya kudhibiti maeneo yanayo endelea kutumika. Kwani kwa kufanya hivyo bado hawatokuwa wametatua tatizo lilipo kwenye jamii.

Ikumbukwe kuwa hatua ya kutafuta eneo jipya la Kama, imetokana na kumwegwa na kubadilishwa kwa matumizi ya eneo la makaburi ya Waislamu, ambalo awali lilikuwa na ukubwa wa hekta 80 za mraba na sasa linakaribia kuwa na hekta 25 za mraba.

Kwa upande wa Wakristo wa Unguja mjini, ipo haja ya kuendelea na wazo lililotolewa na waumini wenzetu juu ya kulizungushia ukuta eneo hilo. Viongozi wa madhehebu yote yanayotumia eneo hilo itakuwa ni jambo la msingi iwapo mtakutana na kupanga namna ya kuweza kujenga uzio ili kuifadhi makaburi hayo na eneo lililobaki.

Ni jukumu letu kwa kiasi fulani kulilinda eneo hilo pasipo kutegemea sana serikali. Hii itasaidia kulitunza eneo hilo kwa muda mrefu. Tunaweza kuangalia na kuiga mfano wa Makaburi ya Wajerumani ya pale Mwembemadema, ambayo yamedumu kwa zaidi ya miaka 150, na tunaweza vilevile kuangalia jinsi makaburi yanavyoweza kuvamiwa kama ilivotokea kwa makaburi ya Wakatoliki hapo hapo Mwembemadema, ambapo baadhi ya watu walianza kuzika kabla ya kutiwa uzio.

Kisheria, maeneo ya makaburi yamekuwa na utata mwingi. Hakuna sheria rasmi juu ya udhibiti na utunzaji wa maeneo ya makaburi, zaidi ya ile iliyotungwa baada ya Mapinduzi ikitoa uhuru wa kubadili matumizi ya makaburi baada ya kupita miaka 40. Mfano wa karibu juu ya sheria hii ni pale ilipotumika katika makaburi ya kariakoo.

Sunday 9 February 2014

Matokeo ya Uchaguzi Kiembesamaki: CUF Watafute Sababu Nyingine Mpya.



Kama ilivyo ada kila baada ya uchaguzi, vyama vishiriki vimekuwa vikitoa maoni yao juu ya mwenendo mzima wa uchaguzi kuanzia wakati wa kampeni hadi upigaji kura. Maoni ya vyama vya siasa hivyo ni juu ya ushiriki wao na namna uchaguzi ulivyokwenda halikadhalika kujipima kufanikiwa kwao ama kutofanikiwa kwao katika chaguzi husika.

Mapema mwezi huu kulifanyika uchaguzi mdogo wa kuchagua mwakilishi mpya katika Jimbo la Kiembesamaki huko Unguja, ambapo chama cha CCM kilishinda uchaguzi huo kwa kupata asilimia 76 na mgombea wake Bw. Mahmuod Thabit Kombo kutangazwa mshindi.

Chama cha CUF ambacho ndio chama kikubwa cha upinzani visiwani humo kiliambulia asilimia 18, ikiwa ni asilimia ndogo sana kulinganisha na umaarufu wake na kukubaliwa kwake visiwani humo. Hii inatoa picha mbaya kwa wafuasi wa chama hicho na inatia kichefuchefu kwa uongozi wa chama hicho. Ikumbukwe kuwa chama hicho baada ya kutoridhisha na matokea mengi ya uchaguzi visiwani humo ilifikia hatua ya kutoitambua serikali na kususia shughuli zote za kiserikali ikiwa ni pamoja na ushiriki katika Baraza la Wawakilishi.

Kwa kifupi kila mtu anajua miafaka iliyokuwa ikiundwa kila baada ya chaguzi kutokana na chama cha CUF, kupinga matokeo ya uchaguzi. Hatima ya miafaka hii ilipelekea kuanzishwa kwa serikali ya umoja wa kitaifa baada ya maafikiano na chama cha CCM.

Moja ya sababu kubwa ambayo imekuwa ikisikika tokea kurudi kwa mfumo wa vyama vingi nchini, ni ile ya uchaguzi kutokuwa huru na wa haki pamoja na kuporwa kwa demokrasia visiwani humo na chama cha CCM, zaidi lawama kwa Tume ya Uchaguzi. Sababu hizi zimekuwa zikirudiwa rudiwa kila baada ya uchaguzi na hasa katika matokeo ambayo chama cha CUF ikishindwa. Pale wanaposhinda hamna sababu hizi.

Baada ya maridhiano na kuja kwa serikali ya umoja wa kitaifa, wengi wetu tulitegemea kutosikia tena sababu hizi kutoka katika chama hicho, kwani sasa nao ni waundaji wa serikali ambayo hapo awali walikuwa wakiilalamikia. Kitendo cha katibu mkuu wa CUF Bw. Maalim Seif Hamad na Mkurugenzi wa Haki za Binadamu na Mawasiliano ya Umma wa CUF, Bw. Salim Bimani kuibuka kupinga matokeo ya uchaguzi mdogo wa Kiembesamaki kwa kauli zilezile za miaka nenda rudi kinatia shaka na kinatoa maswali mengi miongoni mwetu.

Akiwa huko Pemba Bw. Seif Sharif Hamad, amerudia kauli zake za kudai kuwa uchaguzi haukuwa huru na serikali hiyo hiyo anayoifanyia kazi imehujumu uchaguzi huo kwa kupandikiza mamluki wakati wa upigaji wa kura.

Alisema "Kama kuna wananchi wa Kiembesamaki waliokwenda kupiga kura basi hawazidi elfu moja, wengi walichukuliwa katika maeneo tafauti, kama vile Makunduchi, Mtende, Kitope na Bumbwini na wakapelekwa kupiga kura huku wakilindwa na vikosi vya serikali".

Nae Bw. Bimani alisema "Chama cha CUF kilibaini tokea mapema maandalizi ya fujo na matumizi mabaya ya nguvu za dola pamoa na vikosi vya serikali, ambavyo viliandaliwa kwa dhamira ya makusudi ya kuwapa haki waisostahiki na pia kuwanyima watu wengi haki yao ya kufanya maamuzi ya demokrasia".

Kauli hizi toka kwa viongozi hawa zinatia shaka juu ya ukweli wa malalamiko ya chama hiki kabla na baada ya kuja kwa serikali ya umoja wa kitaifa. Ni kauli ambazo zimeshazoeleka sana katika masikio ya wananchi wengi visiwani humo na nchini Tanzania kwa ujumla. Sina budi kujiuliza ni nini mafanikio ya CUF kuwepo katika serikali ilhali bado wanaendelea kuilalamikia serikali hiyo hiyo. Ni nini faida iliyopatikana kwa kuwepo na maridhiano iwapo kero ya ulalamishi wa hujuma katika chaguzi ipo pale pale?

Kwa upande mwingine nashindwa kuelewa kama viongozi hao wameshindwa kuona impact iliyotokea baada ya kuja kwa serikali ya umoja wa kitaifa kwa wanachama na wapenzi na wapiga kura wao. Je bado wanachama wao wanaona kuna umuhimu wa kushiriki katika chaguzi ambapo matokeo yake hayatoweza kubadili nafasi ya chama hicho katika kuendesha serikali? Ni kwa kiwango gani chama hiki kina maamuzi katika kuendesha serikali ya maridhiano?

Ukiangalia vyama vingine ambavyo havipo kwenye serikali ya umoja wa kitaifa kama vile TADEA, ADS, SAU na kadhalika, wao wameyapokea matokeo haya kwa mikono miwili na zaidi wameendelea kuangalia kama kumekuwepo na mafanikio katika kushii na kukubaliwa na wananchi kupitia matokeo hayo. Zaidi wameonyesha kutokuwepo na hujuma yoyote wakati wote wa uchaguzi huo tofauti na madai yaliyozoeleka ya CUF.

Bw. Ali Mohamed Ali Mwenyekiti wa TADEA amekiri kutokuwepo kwa mamluki waliopata kupia kura katika vituo vyote vya uchaguzi huo, aidha waliopiga kura ni wananchi wa Kiembesamaki. Nini nafasi ya kauli ya Bw. Hamad hapa? TADEA ni mojawapo ya vyama vilivyoshiriki chaguzi zote visiwani humo tokea kuja kwa mfumo wa vyama vingi.

Ni vema kwa wakati huu chama cha CUF, kikajiangalia upya juu ya ushawishi wake kwa wanachama wake na nafasi yake kama chama kikubwa cha upinzani visiwani humo badala ya kuja na kauli rahisi rahisi kama hizi. Muda wa kufanya hivyo wanao na ni mwingi. Zaidi wapime nafasi yao serikalini na hatima ya chama chao.