Thursday 6 November 2008

"Migogoro ya Kisiasa katika SMZ"- Hayo ni Mavuno...

Hivi karibuni Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Kiongozi, alinukuliwa akisema kuwa migogoro ya kisiasa katika SMZ imekuwa chanzo cha ucheleweshaji wa mipango ya maendeleo ya wananchi wake. Kauli hii sio ngeni miongoni mwa wananchi wa visiwa vya Zenj hali kadhalika kwa maelfu ya watendaji wa vyombo mbalimbali ya SMZ. Migogoro inayozungumziwa na Mhe. huyo ni matokeo ya sera za umimi na uwale zilizozaliwa wakati Visiwa hivyo vilipoanza kuingia katika mfumo wa vyama vingi mapema katika miaka ya tisini.

Siasa katika vyombo vya SMZ ilikuwa ni kwa manufaa ya chama tawala, hii ni kwa watendaji wote kuanzia wa ngazi za chini hadi za juu. Kila mfanyakazi aliaminika kuwa ni mwanachama wa chama tawala na ameajiliwa ili kutekeleza sera za chama. Hii ilikuwa inadhibitisha na ushirika wa asasi za SMZ katika shughuli za kichama ambapo ilifikia hatua za kufunga ofisi kabla ya muda wake ili kutoa nafasi kwa wafanyakazi kushiriki katika mikutano ya hadhara ya chama tawala. Nahisi katika kipindi hicho hadi sasa ni shurti uwe mwanachama wa chama tawala kabla ya makablasha yako ya uombaji kazi kujadiliwa.

Hata hivyo kuingia kwa mfumo wa vyama vingi kulibadilisha mtazamao wa wafanyakazi kuhusu umuhimu wa kuwa katika chama tawala ili kuendelea kuwatumikia wananchi. Mabadiliko haya yaliguza wafanyakazi katika ngazi zote. Wafanyakazi wa ngazi za juu ambao wengi walikuwa katika nyadhifa zingine chamani, huku wakipata misukumo toka chamani, bila kujijua walianza kupandikiza mbegu mbaya mno ndani ya vyombo vya SMZ.

Katika moja ya mikutano ya kampeni ya 1995 Kiongozi wa ngazi ya juu chamani na katika SMZ alitamka maneno ya kejeli mno kwa watendaji wa SMZ ambao wamehusu kisiwa cha pili. Hotuba yake hiyo ilijukuwa imejaa ubaguzi na shutuma nyingi kwa wafanyakazi na wananchi toka katika kisiwa cha pili haikuweza kujenga bali ilikuwa ndio mwanzo wa migogoro katika Idara zote za SMZ, ambapo Mhe. Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri kiongozi anazungumzia.

Nakumbuka siku mbili baada ya hotuba ile, mmoja wa mfanyakazi katika idara ya kutoa huduma ambae alikuwa ni rafiki yangu aliniambia kuwa pamoja na kuwa na mapenzi ya muda mrefu na chama tawala lakini maneno yaliyozungumzwa na kiongozi huyo ni matusi makubwa kwao watokao kisiwa cha pili, hivyo anajitoa rasmi katika chama tawala, na yupo tayali kwa lolote ambalo litamtokea kwa hatua hiyo yake.

Mbaya zaidi, baada ya hotuba hiyo wafanyakazi wengi waliohusu kisiwa cha pili ambao walionyesha mapenzi tofauti walijikuta wakipoteza kazi zao, wengine wakinyanyaswa na kutegwa kwa sababu za kisiasa tu na tena kwa sababu ya SMZ kuunganisha siasa na serikali.

Haya aliyozungumza Mhe. Waziri hayana kificho, kwani katika moja ya miafaka ilikubalika kuwarudisha makazi wale wote ambao walifukuzwa kazi kwa tofauti za kisiasa. Ni wajibu wake iwapo anataka kuona migogoro hiyo inakwisha kuchukua hatua za vitendo katika kuona kuwa siasa katika Idara za SMZ zinawekwa kando, ikiwa ni pamoja na kuwarudisha wale wote ambao walitimiliwa kwa ajili ya mitazamo yao ya kisiasa. Kwa upande wa ajila mpya zisiangalie siasa bali uwezo wa mfanyakazi.

Zaidi Mhe anatakiwa kuona kuwa utengano katika idara za SMZ unakwisha ili kuweza kuongeza kasi ya kutoa huduma na kuleta maendeleo kwa wananchi wa visiwa hivyo.

Wednesday 8 October 2008

Mbolea ya Mboji katika mjadala


Waalimu wawili wakuu wa shule ya Msingi za Kahama na Kirumba pamoja na Mwalimu toka shule ya msingi Isenga, wakifuatana na Mratibu wa Mradi wa Tampere - Mwanza wametembelea chuo cha TAMK Tampere kujadili maendeleo ya mradi wa utengenezaji wa mbolea katika shule zao jioni ya leo. Pichani Waalimu hao wakitoa maelezo juu ya mradi huo ambao kwa ufupi umekuwa ni wa mafanikio makubwa.

Aidha wanafunzi wa TAMK walipata kutoa shukrani zao juu ya ushirikiano mkubwa wakati wa uanzishaji wa mradi huo wa aina yake wenye lengo la kuwashirikisha wanafunzi katika utengenezaji wa mboji.



Hadi sasa shule zote tano ambazo zipo kwemye mradi huu zimefanikiwa kuzalisha mbolea hiyo, huku shule ya msingi ya Isenga ikiwa tayali imeanza kutumia mbolea hiyo kwa upandaji wa miti katika shule yao. Mwalimu toka Isenga alisema kuwa mafanikio hayo yameanza kuvuka mipaka ya shule hiyo kwa baadhi ya wakaazi wa karibu na shule hiyo kuanza kutengeneza mbolea ya mboji.

Mipango ya baadae ni kuendelea kutoa elimu ya utengenezaji wa mboji kwa shule nyingi zaidi katika Jiji la Mwanza. Aidha kutoa nafasi kwa wanafunzi na wananchi wa jiji hilo kupitia vikundi kazi kutembelea jiji la Tampere ili kutoa ujuzi wao wa kutengeneza mbolea kwa wakaazi wa jiji la Tampere. Hii itakuwa ni nafasi nzuri zaidi kwao, kwani matumizi ya artificial fertilizer yanategemewa kupungua kwa kasi katika nchi ya Finland kutokana na kuongezeka kwa bei yake kwa kiwango cha asilimia 300.

Kwa upande wa TAMK wanafunzi wameonyesha kulidhika sana na mradi huo kiasi kwamba idadi ya wanafunzi wanaotegemewa kwenda kwenye awamu ya pili ya mradi huo imeongezeka. Hii ni changamoto kwa Jiji la Mwanza kuandaa shughuli nyingi kadili ya idadi ya wanafunzi hao ili kuweza kunufaika vema na utaalamu wao.

Tuesday 30 September 2008

Idd Mubaraka


Napenda kuwapa mkono wa idd wadau wote wa blog hii. Sikukuu njema

Monday 29 September 2008

Wanafunzi na Mazingira...Case: Mwanza





Mazingira ya shule ya Msingi Igoma. Shule hii ina klabu ya mazingira ya wanafunzi na moja ya kazi zake ni kutunza mazingira ya shule hiyo.




Wanafunzi wa shule ya Msingi Kirumba wakiandaa shimo kwa ajili ya utengenezaji wa mbolea kwa taka za jikoni. Klabu ya Mazingira katika shule hiyo hujishughulisha na usafishaji wa mazingira katika kata yao ya Kirumba.


Uandaji wa mashimo kwa ajili ya kutengeneza mboji kutokana na taka za jikoni, katika shule ya Msingi Isenga