Monday 3 September 2007

Zenj Watatoa Lini Miss Tz......?



Mshindi wa Miss Tz mwaka huu amewasha moto mkubwa kwa wadau wa urembo wa huko bara, ikiwa ni pamoja na mamiss kadhaa waliopita. Moto huo ambao kuzimika kwake ni songombindo unatokana na madai kuwa miss huyo hana asili ya Utz bara, ukinondoni n.k Usishangae sana kusema Utz bara, kwani huko visiwani hakuna mambo ya Umiss, na nina shangaa huyo mdosi...sori huyo miss kuitwa Miss Tz wakati Warembo wa Zenj hawakushiriki mashindano hayo...

Mara ya mwisho kwa kumbukumbu zangu, warembo wa marashi ya karafuu walishiriki mashindano hayo wakati yakidhaminiwa na fegi za aspen.. sijui bado zipo au la! manake fegi hizo zimeadimika sana mitaani.

Awali ya yote inaonekana kuwa Watz wameshindwa kabisa kuficha makucha yao ya kibaguzi kwa kupiga kelele kwa mdosi huyo mzalendo kutwaa taji hilo. Mimi binafsi sishangai sana, kwani ile dhambi ambayo ipo visiwani huku, imeweza kuvuka bahari na kutua huko Bongo...Tz bara.

Iwapo kungekuwpo na Miss Zenj basi yoyote yule ambae angebahatika kutwaa taji hilo, angechunguzwa kuwa ana asili ya wapi...! Kama ni kutoka kisiwa cha pili basi angeitwa ni mpemba, na iwapo angekuwa anakaa Ng'ambo iliyo karibu na Mji mkongwe basi wangesema ni Mngazija, zaidi iwapo angekuwa na chongo basi moja kwa moja angeitwa ni mnyamwezi( mtu yoyote toka bara).

Utamaduni wa kuangalia mtu ana asili ya wapi upo muda mrefu katika visiwa hivi, kiasi kwamba umeleta kujitenga kimakaazi kwa watu... Tabia hii huko bara haikuwepo huko zamani, lakini sasa naona inaingia kwa kasi kubwa. Sijui inaashiria kitu gani, kwani, huko bara waasia wamekuwa wakishika dhamana kubwa kubwa katika kuongoza nchi pasipo mashaka wala malalamiko yoyote. Leo hii kupatikana kwa miss mdosi wa kitz imekuwa nongwa!

Iwapo tulikuwa tukitembea vifua mbele kupinga ubaguzi wa rangi miaka ile, iweje leo tutoe machozi kwa mtz wa kiasia kutwaa taji la Utz? Au ile dhambi toka Zenj tayali imeshaanza kuingia huko bara? Tuliwahi kuonywa kuwa dhambi ya ubaguzi ni mbaya sana, eti ni sawa na kula nyama ya binadamu, kwani hutoishia kuionja tu, bali utaendelea kuila tu!... Mwakani Watz watahoji ni kwanini Mass wanatoka Kinondoni, au kwa nini wamiss wanatoka katika kabila fulani kila mara... Dhambi hiyo itaendelea tu!

Wazenj mara nyingi wamekuwa wakisoma mifano imara ya Tz bara katika suala zima la kuishi bila kujali huyu anatoka wapi au ana asili ya wapi... Iwapo leo hii mmefikia hatua hii, basi mnapoelekea sio kuzuri kabisa. Mfano wa karibu upo huku visiwani!

Thursday 30 August 2007

Wednesday 29 August 2007

Kauli ya Nahodha ina Walakini

Waziri Kiongozi wa Zenj, ambae yupo mkoani Ruvuma ametoa kauli ya kusisitiza kuwa, Elimu ndio njia pekee ya kuwaletea maendeleo wakazi wa Mkoa huo,kutokana na mkoa huo kukosa Umeme wa kuhaminika na kuwa na barabara mbovu. Msisitizo wa kauli hiyo aliutoa kwa kufananisha ukuaji wa kasi wa uchumi wa Singapore na udodoraji wa maendeleo ya mkoa huo na Tanzania kwa ujumla.

Kauli hii ina utata mkubwa kwani elimu pekee haiwezi kuleta maendeleo yoyote iwapo njia zingine za kuleta maendeleo zitakuwa zimebanwa kwa wananchi. Mkoa wa Ruvuma unasifika kwa kuzalisha Mahindi, Kahawa, Tumbaku,Alizeti na mazao mengine. Kabla ya mwaka 1984, usafiri wa kwenda huko ulitegemea zaidi njia ya anga (ATC).Usafiri wa barabara ulikuwa ni wa usumbufu mkubwa na uliweza kuchukua muda mrefu kufika mkoani. Kufunguliwa kwa barabara ya Makambako - Songea katika kiwango cha lami, kulitoa fursa kubwa kwa mkoa huo kuvuma katika uzalishaji wa Mahindi. Barabara hii haikuja kutokana na elimu ya waakazi wa huko bali ni kutokana na umuhimu mkubwa wa taifa kupata Mahindi na Kahawa toka mkoani huko.

Mkoa wa Ruvuma kwa miaka mingi umekuwa ukitegemea umeme wa nguvu ya jenereta, ambao licha ya kuwa ni ghali kuuendesha, upatakanaji wake umekuwa ni wa kimgao kwa zaidi ya miaka ishirini sasa. Sasa hapa sijui elimu ya aina gani inatakiwa ili mkoa huo uunganishwe kwenye gridi ya taifa, ambayo inapita katika mikoa ya jirani zake.

Nimeshindwa kuelewa kauli ya Nahodha, kati ya kuwa na elimu na uwewezeshaji wa miundo mbinu na uchumi wa mkoa husika. Kwa mfano majumba ya michenzani huko Zenj hayakujengwa kwa kuwa waakazi wa zenj wote walikuwa ni wajuzi wa ujenzi. Yalijengwa kwa sababu uchumi wa Zenj kipindi hicho ulikuwa unaruhusu, na viongozi kwa kushirikiana na wananchi waliona upo umuhimu wa kufanya hivyo.

Kwa mkoa wa Ruvuma kuwaambia kuwa tatizo lao la umeme litatatuka kwa kuwa na elimu na sawa na kuwaondoa njiani tu...

Tuesday 21 August 2007

Wadau



Altune na Kibunango

Umbeya Wenye Manufaa...

Hatua ya mradi wa Usimamizi wa Uhifadhi na Mazingira ya Ukanda wa Pwani "MACEMP" kanda ya Zenj kuanzisha mpango wa kuwafanya wavuvi kuwaripoti kwa siri wavuvi haramu ni mzuri kwa lengo la kuwajua wavuvi haramu. Hatua hii imechukuliwa ili kudhibiti uvuvi haramu ambao kwa kiasi kikubwa wamekuwa wakiharibu mazingira ya baharini, pamoja na kuhatarisha maisha ya viumbe wa baharani.

Lengo kubwa la mradi huo ni kuhifadhi na kutunza mazingira ya pwani kwa kuondoa umaskini wa wavuvi. Malengo yao kwa kiasi fulani yamefanikiwa kupitia kwa kamati mbalimbali za wavuvi katika kisiwa hicho. Mradi huo umeshatoa boti,ndege,mikopo na nyavu kwa kamati mbalimbali ili kuondoa tatizo la uvuvi haramu huku ikikuza kipato cha wavuvi hao.

Hata hivyo pamoja na utoaji wa vifaa hivyo, tatizo la uvuvi haramu limekuwa likiendelea. Kuendelea kwa tatizo hilo kwa upande mwingine ni kuonyesha kuwa mradi huo bado kuwafikia wadau wote katika sekta ya uvuvi. Zaidi kuna tatizo ndani ya kamati za uvuvi ambao wamelalamikiwa na mradi kwa kuvujisha siri za mikakati ya kudhibiti uvuvi haramu.

Mradi huu ili kuwa endelevu unapaswa kuangalia tena malengo yake, na njia ambazo wanatumia kuwafikia wadau wake. ushirikishwaji wa kamati hizo za uvuvi na wavuvi wenyewe. Iwapo mojawapo wa malengo ni kuondoa umaskini wa wavuvi, hapana shaka basi wawatafutie au kuwaelekeza jinsi ya kupata soko la uvuvi wao(soko la ndani na nje), uhifadhi endelevu wa maeneo yanayotumika kwa uvuvi, maana na athari za uvuvi haramu.
Kutoa vifaa pekee sio njia ya kuweza kufanikisha kuondoa uvuvi haramu na hata umaskini wa wavuvi hao.

Ipo mifano mingi ya miradi ambayo ilipewa vifaa vingi kwa miradi hiyo lakini ikashindwa kuendelea na kuishia kufa baada ya muda mfupi. Hii ilitokana na wadau kutojiona kuwa wapo ndani ya miradi hiyo, na kujenga tabia kuwa maendeleo ya miradi hiyo sio yao bali ni ya serikali au watoa miradi hiyo.

Iwapo mradi wa MACEMP watataka mradi huu uwe endelevu, inawabidi kuangalia ni njia gani ambayo wataweza kuitumia kuhakikisha kuwa wadau wao wanajua umuhimu wa mazingira ya bahari ambalo ndio shamba lao la kuwaingizia kipato. Inawabidi wawafikie hadi wale wavuvi wa chini kabisa,zaidi ya kuishia kwenye kamati na wale wavuvi wanaojulikana huko vijijini. Zaidi ya kuwafikia itawabidi kuwapa elimu tosha ambayo itawafanya wathamini na kutambua umuhimu wa mradi huo kuwa upo kwa ajili ya kuwaondolea umaskini huku mazingira ya bahari na viumbe vyake yakiwa salama.

Sunday 19 August 2007

TV Zanzibar(TVZ): Jionee mwenyewe walivyochoka

Pamoja na kushikilia rekodi ya kuwa kituo cha kwanza cha television ya rangi katika Afrika ya Mashariki kama sio Afrika, Television hiyo imekuwa ikirudi nyuma kimaendeleo kila kukicha. Sababu za kuanguka kimaendeleo zinajulikana sana, kwani zimekuwa zikisikika kila siku masikioni mwetu, toka kwa Viongozi wa Kisiasa hadi kwa Watendaji wa kituo hicho.

Lengo la bandiko hili si kuzungumzia uchakavu wa Majengo au vyombo vya kurushia matangazo ya tv hiyo, bali ni kuzungumzia muundo wa web site yao, ambayo umeniacha hoi bin taabani.

Tovuti ya kituo hicho kikongwe unakatisha tamaa, na haina uhusiano wowote wa moja kwa moja na shughuli za kila siku za kituo hicho. Zaidi Tovuti hiyo ni kama imewekwa kuhifadhi baadhi ya hotuba za Rais na Waziri kiongozi wa Zenj. Pengine ingependeza zaidi iwapo tovuti hiyo ingekuwa ni ya Ikulu au ya Ofisi ya WK!

Sijui ni kazi ya Mkurugenzi au Afisa Uhusiano au Mwangalizi wa ofisi kusimamia update za tovuti hiyo. Kwa yoyote ambae anahusika basi ameshindwa kabisa kuelewa ni kwa nini TV huwa na tovuti, au ndio hadithi ile ile ya vyombo vya SMZ kujipendekeza zaidi kwenye Ofisi za Wakubwa wao, na kusahu kushughulikia maendeleo ya Ofisi zao!

Kwa ufupi ni aibu kubwa na ni kituko kikubwa kama si kioja kwa TVZ kuiweka hewani tovuti yao. Kama walikuwa hawajawa tayali kuweka tovuti, wangeweza tu kushikiria domain yao bila ya kuirusha hewani kitu ambacho hakina uhusiano wowote na shughuli zao za kiutendaji, hata historia yao. Zaidi hiyo Elimu kwa Televisheni naona bado kufikiwa au kufanyiwa kazi

Wednesday 15 August 2007

Mbinu za Kizenj za Kusafirisha Mizigo...



Moja ya mambo niliyo yaona huko UK ni jinsi wazenj wanavyojitahidi kusafirisha malundo ya vitu vilivyotumika toka UK kwenda Zenj... Mazagazaga hayo ni kuanzia mafriji, mavideo(VHS), maprinter, mamonitor, makomputer, majiko ya umeme /gasi mabafu, vyoo, n.k.




Makontena ya size ya futi 40 ndio maalufu katika kusafirishia mazagazaga hayo.. ambayo mengine yapo katika hali mbaya sana kutumika zaidi ya kufaa kwa kutupwa tu.



Leo hii tuangalie jinsi ya kusafirisha magari matano katika kontena la futi 40......






















Wednesday 8 August 2007

Safarini Suomi...

Baada ya kuona Vituko kibao vya wazenj hapa Uk... takribani kwa miezi minne sasa, Nageuza safari na kurudi kijiweni huku nikiwa na rundo la vituko vya wazenj hapa uk... tokea wazungu wa unga, hadi vitangi, wasomi na wafanyabiashara, wazazi hadi wajane... ili mradi ni vituko kede kede.. nikipata nafasi nitakuwa nawapasha baadhi ya vituko vyao...

Thursday 14 June 2007

Mahakama Kuu ni Kimeo....

Nimewahi kuandika kuhusu mashaka makubwa ya mahakama za zenj katika mabandiko yaliyopita, leo hii kumeibuka kadhia nyingine ambayo hapana shaka ipo kwa muda mrefu tu huko zenj..

Imeripotiwa kuwa mahakama za zenj, hasa Mahakama Kuu haina majaji wa kutosha hivyo kukosa hadhi ya kuitwa Mahakama Kuu kwa mujibu wa katiba ya visiwa hivyo. Tatizo la Majaji huko visiwani lipo kwa muda mrefu sana, ingawa kuna wakati smz ilijitia kifua mbele kwa kukodisha majaji toka nje ya visiwa hivyo(Mapopo).

Kwa mwananchi wa kawaida hawezi kuamini kuwa Visiwa hivyo havina majaji, kwani wao mtu yoyote afanyae kazi mahakamani basi ni jaji, kama ilivyokuwa katika hospitali zao kwa wafanyakazi wote huitwa ni madokta.

Pengine ujuha huu wa kushindwa kutofautisha mgawanyiko wa ngazi za wafanyakazi, upo ndani ya vibosile wa SMZ kiasi cha kujisahau kuwa hawana Majaji wa kutosha kuendesha kesi lukuki katika Mahakama Kuu. Udhaifu wa mahakama za zenj na hasa katika watendaji wake umekuwa ni gumzo kubwa katika kipindi hiki, wakati kuna fufunu ya uteuzi wa Jaji Mkuu mpya wa Tanzania,

Ukiachana na hayo ambayo yanatia kichefuchefu, Mahakama ya Mkoa wa Mjini Magharibi ina Mahakimu watatu tu, ambao kwa maneno mengine ndio Mahakimu wa Mikoa yote ya Zanzibar! kwani sio siri kuwa sijawahi kusikia Hakimu wa Mikoa mengine minne wakitajwa, licha ya kesi walizohukumu kuripotiwa...! Hao Mahakimu wa wilaya wapo kwa hesabu ya vidole, na wengi wao wapo katika Mahakama za wilaya ya Mjini na ile ya Magharibi... Nasikia huko Pemba kuna mahakama ya Mkoa vilevile, hata hivyo Hakimu wake kutwa yupo Vuga!

SmZ kupitia kwa ofisi ya mwanasheria mkuu wa serikali wanapaswa kuja na suluhisho la kudumu kuhusu kadhia hii, na sio kila siku kuwa ni watetezi wa uchovu wa SMZ. Iwapo wao ndio wanasimamia Mahakama na sheria zake, basi hawana budi kuwa na mipango madhubuti ili kuona kuwa vyombo vya haki visiwani humu vimekamilika kwa mujibu wa sheria na katiba ya visiwa hivyo. Kitendo cha kuwaondoa Wapopo katika Mahakama zetu kilikuwa kizuri kwa manufaa ya watu na uchumi wetu unaodorola, aidha ipo haja basi ya ofisi hiyo kupanda Jahazi hadi bara ili kupata Majaji wenye kujua sheria zetu na maadali ya Mtanzania.

Friday 8 June 2007

'Ongezeko la Uzaaji UK' Wazenj Hawako Nyuma....

Imeripotiwa kuwa kumekuwepo na ongezeko kubwa la uzaaji hapa UK, ikiwa ni ongezeko kubwa kwa miaka 26. Ongezeko hilo la uzaaji, limechangiwa na wahamiaji miongoni mwao wakiwa ni wazenj.

Moja kati ya watoto watano wanaozaliwa hapa, amezaliwa na mhamiaji, hivyo kufanya ongezeko la asilimia kumi kwa mwaka kwa watoto wanaozaliwa na wahamiaji. Mwaka 2006 walizaliwa watoto 669,531 kwa wastani wa kila mzazi wa 1.87 huku wahamiaji wakizaa asilimia 21.9 ya watoto wote waliozaliwa mwaka 2006. Wahamiaji wengi ni kutoka nchi za ulaya ya mashariki, wengi wao wakiwa ni Wapoland. Zaidi kumekuwepo na ongezeko kubwa watoto toka kwa wanawake wa Pakistan, India, Afrika na Mashariki ya Kati. Wachunguzi wa mambo wanasema tokea mwaka 1997 (labour ilipoingia madarakani) kiasi cha wahamiaji milioni 1.5 wamehamia UK.[1]

Wanawake wengi toka Zenj hawapo nyuma katika suala la uzaaji, wengi wa wanawake hao ni kinamama wa nyumbani. Nilipojaribu kuulizia zaidi kuhusu uzaaji huo wa kasi, wengi wao walisema ni kutokana na mafao mazuri ambayo hutolewa na serikali ya hapa, hivyo kutokuwa na wasiwasi juu ya malezi na usomeshaji wa watoto hao tofauti na kama ingekuwa huko Zanzibar, ambapo jukumu lote lipo kwa mzazi pekee..!



1.Source: Daily Mail, June 8 2007.

Saturday 19 May 2007

Madeleine wa Zenj

Wengi wetu sasa tunajua kutoweka kwa Madeleine, mtoto wa miaka minne, raia wa Uingereza aliyetoroshwa huko Ureno yapata siku kumi na sita sasa. Vyombo vya habari na hasa vya hapa UK vimekuwa vikitoa maendeleo ya sakata hilo katika kila habari zao. Hivyo kuweza kuwafikia watu wengi kadiri iwezekanavyo. Leo wakati Fainali ya Kombe la FA, kati ya Man Utd na Chelsea, video ya dakika nne ya Madeleine inategemewa kuonyeshwa.Hivyo kuweza kutazamwa na watu zaidi ya nusu bilioni duniani kote.

Huko Zenj kuna mtoto wa kike wa miaka kumi na sita ameripotiwa kutoroshwa na mwalimu wake yapata miezi mitatu sasa. Jeshi la polisi visiwani humo limeomba kusaidiwa na jeshi la polisi la kimataifa(interpol) katika kumtafuta mtoto ambae jina lake ni Maryam Farid Said.

Tofauti ya Maryam na Madeleine ni kubwa sana, Madeleine ni mtoto mdogo sana asiejua hili na lile, wakati Maryam ni msichana mkubwa ambae anajua nini anafanya. Cha kusisimua zaidi ni kuwa Maryam hii ni mara yake ya pili kutoroshwa na wanaume.

Msichana huyo ambae alikuwa ni mwanafunzi wa shule ya binafsi ya bweni huko Bububu Zanzibar ana undugu na Rais wa Tanzania Jakaya M. Kikwete hivyo kuweka utoroshwaji wake kuwa wa mvuto zaidi. Polisi wa visiwani hapo wanashuku kuwa mtoto huyo atakuwa ametoroshwa na mwalimu wake ambae ni raia wa Uganda.

Iwapo mtoto huyo akipatikana, wazazi wake ambao sasa wanamtafuta, itabidi wamkalishe kikao mtoto huyo, kwani hii ni mara ya pili kutoroshwa hivyo kujenga hofu juu ya tabia yake kwa ujumla. Hapana shaka kuwa mtoto huyo anashirikiana na hao wanao mtorosha hivyo kufanya utafutaji wake kuwa mgumu zaidi. Zaidi nawatakia kila la heri Wazazi wa mtoto huyo katika jitihada za kumtafuta mwanao. Hali kadhalika wanachi ambao kwa namna moja ama nyingine ambao watakuwa na habari yoyote ya kuweza kupatika kwa mshichana huyo watoe ushirikiano wao kwa kutoa taarifa katika vyombo husika.