Wednesday 16 May 2007
Thursday 19 April 2007
Uchafuzi wa Mandhari ya Bwawani Hotel
Pamoja na vitu vingine vinavyopatikana katika hotel kubwa, hotel hii ina viwanja wa Tennis ndani na nje, swimming pool ya ndani, ukumbi wa michezo( game room) na bwawa zuri upande wa mbele ya hotel hiyo.
Leo ningependa kuzungumzia juu ya bwawa la hoteli hiyo, ambapo pengine ndio lililo zaa jina la Hotel Bwawani. Bwawa ambalo hadi hoteli inakamilika katika miaka ya sabini, ujenzi wake ulikuwa bado kukamilika, hivyo kuto toa madhari halisi ya hoteli hiyo.
Katika miaka ya themanini, wakati SMZ ikiwa inajichanganya kuamua kufuata mfumo gani wa serikali za mitaa, toka serikali za majimbo, kulijitokeza wawekezaji ambao waliona kuwa upo umuhimu wa kuendeleza bwawa hilo. Katika kipindi hicho tayali madhari ya bwawa hilo ilikuwa ni ya kuchukiza zaidi kuliko kuvutia. Majani maji yalikuwa yakiongezeka kwa kasi kubwa.
Mapendekezo yaliyotolewa na wawekezaji wa miaka hiyo ya themanini ni kuhamisha bandari ya yatch iliyopo kwenye bandari ya Malindi hadi kwenye bwawa hilo, kujenga ofisi ya Meja wa Halmashauri ya Mji wa Zanzibar(Town Hall) katika kingo za bwawa hilo, toka katika Ofisi ya Halmashauri ya Mji katika barabara ya Benjamin Mkapa. Ofisi hiyo ya Meya licha ya kuwa na ukumbi wa mikutano ya Madiwani, pia ungekuwa na club ya yatch zinazotia nanga Kisiwani hapo toka sehemu mbalimbali hapa duniani.
Wazo hili lilipo pelekwa kwenye vyombo vya SMZ lilitupwa kando, licha la kuwa wazo bora kabisa katika kipindi hicho hadi leo na mpaka kesho. Kwani kinachoendelea katika bwawa hilo hivi sasa ni uchafu mtupu. Kwa upande mwingine iwapo wazo hili lingefanyika katika siku zile, matatizo ya kisaikolojia yanayowakuta Madiwani na Meya wao sasa yasingekuwepo. Kuwachanganya Meya na Madiwani wake katika jengo moja na Watendaji wa Manispaa ya Zanzibar kumesababisha kuwepo na miingiliano ya kiutendaji kila siku katika Manispaa hiyo.
Ukiachana na adha za madiwani hao, bwawa hilo ni makaazi ya ndege watokao kaskazini ya dunia wakati wa msimu wa baridi huko kaskazini, hivyo iwapo bwawa hilo lingeendelezwa na kutuzwa vema tungeweza kujifunza mengi kuhusu ndege hao na zaidi kingekuwa ni mojawapo wa kivutio cha utalii. Lakini hili nalo halipo ndani ya mawazo ya watendaji wa SMZ!
Kumekuwepo na mawazo mengi toka serikalini na katika Halmashauri ya Mji juu ya kuendeleza bwawa hilo. Lakini yote kwa upande mmoja ni kuchakaza tu bwala hilo au kuliondoa kabisa.
Katika miaka ya tisini msikiti(Msikiti Mabluu) ambao uliondolewa ili kupisha ujenzi wa bwawa hilo, ulijengwa upya. Ujenzi wa msikiti huo ulikuwa ni kutoa mfano wa mradi mpya wa ujenzi wa nyumba katika muda mfupi. Ujenzi wa msikiti ulikamilika ndani ya siku saba na siku ya nane ukatumika. Mawazo ya ajabu ajabu yakazidi kumiminika, moja wa Mameja alipendekeza kuwa sehemu yenye magugu maji ijazwe kifusi ili kupatikane nafasi ya kuweka makontena ya biashara! Meya mwengine alikuja na wazo kuwa bwawa hilo litumike kuwa jaa kuu la taka.
Pengine waliokuwa wanajitahidi kuliweka bwawa hilo katika hali ya usafi ni wafungwa, ambao kila mwaka kwa mamia hupita hapo kukata magugu maji.
Miaka ya elfu mbili Waziri kiongozi alitoa amri ya wafanyabiashara wa vinyago na batiki wapewe eneo hilo kwa biashara zao, agizo likatekelezwa na madhari ikazidi kuwa mbaya. Hata hivyo kutokana na kuwepo kwa msikiti wauza vinyago walijikuta wakiondolewa hapo.
Ukarabati wa kusuasua wa Bandari ya Malindi umeligeuza tena bwawa hilo kuwa sehemu ya kuhifadhia makontena ya bandarini, hiyo kuendelea kuchafua bwawa na zaidi hata kuziba madhari nzuri ya mbele ya hoteli hiyo. SMZ inadai kuwa uwekaji wa makontena katika eneo hilo ni wa muda tu, na hata bandari itakapokamilika makontena hayo yataondolewa. Cha kujiuliza hapo jee vifusi na michanga iliyojazwa katika bwawa ili kutoa ya uwekaji wa makontena yataondolewa au utakuwa ni mwanzo wa kuzaliwa wazo jingine la kutokomeza bwawa hilo?
Kwa maoni yangu wazo lilitolewa katika miaka ya themanini ya kukamilisha ujenzi wa bwawa na ujenzi wa ofisi ya Meya pembeni ya bwawa hilo, lilikuwa ni wazo pekee ambalo lingeweza kulinusuru bwawa hilo kuwa kichaka cha mawazo duni ya viongozi wa SMZ. Aidha kungesaidia kuendeleza bwawa hilo na kuwa sehemu ya kuvutia kabisa katika eneo la Mji Mkongwe zaidi ya Forodhani.
Posted by Kibunango at 15:24 5 comments
Wednesday 11 April 2007
Tindikali kwa wauza kilaji Zanzibar
Sijui kisiwa kitaendelea vipi katika sekta ya Utalii kama wauzaji vinywaji vikali wataendelea kuteswa namna hii haya mambo yakuchanganya maswala ya kidini na uchumi hayana maendeleo yoyote Somalia mfano.
Wakala mwingine wa pombe amwagiwa tindikali
2007-04-10 10:28:44
Na Mwinyi Sadallah,Zanzibar
Wakala mwingine wa kusambaza pombe Zanzibar, Bw. Chadalal Javed, amemwagiwa tindikali usoni, muda mfupi baada ya kufungua duka lake lililoko mtaa wa Empire mjini hapa.
Kamanda wa Polisi mkoa wa Mjini Magharibi Bw. Bakar Khatib Shaaban alithibitisha kutokea kwa tukio hilo. Tukio hilo lilitokea jana saa 3:00 asubuhi.
Alisema kwamba mfanyabishara huyo mwenye asili ya Asia, alivamiwa na mtu asiyejulikana, muda mfupi baada ya kufungua duka lake.
``Ghafla mfanyabiashara huyo alimwagiwa kemikali na kumjeruhi sehemu za usoni na tayari amepelekwa jijini Dar es Salaam kwa matibabu zaidi,`` alisema Kamanda Bakari.
Alisema kuwa wakati tukio likitokea, mfanyabiashara huyo alikuwa dukani na mkwewe wakijiandaa kutoa huduma kwa wateja wao.
Alisema hata hivyo, polisi hawakufanikiwa kuchukua sampuli za kemikali iliyotumika, kwa vile baada ya tukio kutokea, wahusika waliharibu mabaki ya kemikali hiyo.
Kamanda Bakari alisema kwamba iwapo wangefanikiwa kupata mabaki ya kemikali hiyo, wangeweza kupeleka kwa Mkemia Mkuu kujua aina ya kemikali iliyotumika.
``Hatufahamu, aina ya kemikali iliyotumika,lakini tunaendelea na uchunguzi kwa kuwa mtu aliyefanya uhalifu huo alifanikiwa kukimbia baada ya tukio,`` alisema Kamanda Bakari.
Mfanyabiashara huyo anamiliki duka la Scorch Store, ambalo linatumika kusambaza pombe Zanzibar katika mahoteli ya kitali, baa na watumiaji wa rejareja Zanzibar.
Kamanda Khatib alisema hilo ni tukio la pili kutokea kwa wamiliki wa maduka ya pombe. Alisema mwezi uliopita mfanyabiashara mwenye asili ya Kiasia, Bw. Kirikti Mandala, alimwagiwa tindikali akiwa dukani kwake eneo la Michenzani.
Alisema kwamba katika tukio hilo watu wawili walihojiwa na polisi, lakini hadi sasa hakuna mtu aliyefikishwa Mahakamani kuhusiana na tukio hilo.
Hivi karibuni baadhi ya wanaharakati wa dini, wamekuwa wakilalamika kuongezeka kwa idadi ya baa katika manispaa ya Zanzibar, kitendo ambacho wanasema ni kinyume na mila na utamaduni wa Mzanzibari.
Mwezi uliopita wanaharakati hao, waliandamana kupinga ongezeko hilo la idadi ya baa katika mji wa Zanzibar, lakini hawakutoa takwimu za ongezeko hilo.
* SOURCE: Nipashe
Posted by Al tunez at 21:19 2 comments
kibunango
Asante kwa kunikaribisha katika blog hii matata yenye jicho katika vihoja vitokeavyo kisiwani Unguja , napenda kwanza kukutakia safari njema uingereza, na vilevile kutoa ahadi yakujitahidi kucompose as many articles as possible tuko pamoja.
Guidance
Posted by Al tunez at 19:02 2 comments
Safarini Uingereza
Wapenzi wa kona hii ya Vituko vya Zenj, napenda kuwataarifu kuwa nitakuwa safarini Uingereza kuanzia mwishoni mwa wiki hii..
Kwa miezi kadhaa ijayo nitakuwa na blog tokea jiji la London. Zaidi itakuwa jambo la msingi iwapo nitaweza kukutana na wanablog wa Uingereza...na watanzania wengine ambao ni wapenzi wa blog..
Posted by Kibunango at 12:30 3 comments
Tuesday 6 March 2007
Uchovu wa SMZ kwenye masuala ya Umiliki wa Ardhi...
Moja ya matatizo makubwa ya SMZ yapo kwenye masuala ya umiliki wa ardhi. Serikali hiyo ina migogoro mingi kuhusu umiliki na uendelezaji wa ardhi licha ya kuwa na sheria ya Mipango miji/vijiji na Ardhi ya mwaka 1985, Baraza la Manispaa ya mwaka 1995 na Mamlaka ya Hifadhi na Uendelezaji wa Mji Mkongwe ya mwaka 1994.
Sheria hizo zote hapo juu zinasimamia uendelezaji na umiliki wa ardhi, aidha Halmashauri za wilaya nazo kwa upande mwingine zimekuwa zikisimamia uendelezaji wa ardhi. Serikali kuu kupitia kwa Masheha wao nao wamekuwa wakijishughulisha katika masuala ya ardhi.
Katika Mahakama zote visiwani humo kumejaa kesi nyingi za madai ambazo zinahusiana na matatizo ya ardhi.
Leo kanisa la Anglikana huko Zanzibar limekumbushia kadhia yao ya kunyang'anywa ardhi yao na kufanyia mabadiliko ya matumizi. Kimsingi eneo ambalo lina mgogoro ni shule ya msingi Mkunazini ambayo kabla ya mwaka 1964 ilikuwa inamilikiwa na kanisa hilo.
Kinachoshangaza ni hatua ya SMZ kupitia wizara zake kuendelea kubadilisha kinyamela matumizi ya eneo hilo toka eneo la shule na Ibada kuwa eneo la biashara, kwa kuruhusu ujenzi wa maduka katika eneo hilo.
Miaka ya tisini kanisa hilo liliwahi kuomba ruhusa ya kukarabati uzio wa eneo hilo ambao ulikuwa unazama taratibu. Uzio huo unaanzia upande wa mbele ya shule hiyo mkabala na barabara ya Benjamini Mkapa. Kibali cha ujenzi wa uzio huo kilichukua muda mrefu hadi kupatikana. Na kiliweza kupatikana baada ya kanisa hilo kutoa malalamiko mengi kuhusu urasimu wa vyombo vya SMZ.
Ucheleweshaji wa upatikanaji wa Kibali cha Matengenezo ya Ukuta wakati ule sasa ninaweza kuuelewa vizuri. Inaoneka Watendaji wa SMZ walishaona kuwa eneo hilo linafaa kwa kujengwa kwa Vibanda na Viduka vya biashara hivyo walikuwa wanasita kutoa ruhusa ya matengenezo ya ukuta. Na hata walipotoa ruhusa hiyo eneo lilikuwa karibu na shule hiyo halikupewa ruhusa ya ukarabati.
Sasa eneo hilo limejengwa Vibanda vya biashara, na litaendelea kujengwa licha ya maombi ya kanisa hilo kurejeshewa umiliki wa shule hiyo.
Hivi ni nini nafasi ya kuwa na mamlaka ya hifadhi na uendelezaji wa mji mkongwe, iwapo sehemu ambazo zinahitaji kupatiwa hifadhi kutokana na umuhimu wake wa kihistoria, zinashindwa kuhifadhiwa? Kanisa la Anglikana ni muhimu kabisa katika historia ya Zanzibar. Hivyo linatakiwa lipewe nafasi ya ya kuhifadhiwa chini ya Sheria za Mamlaka ya Hifadhi na Uendelezaji Mji Mkongwe.
Posted by Kibunango at 13:06 2 comments
Thursday 15 February 2007
Sasa ni Disco...!
Katikati ya mwaka jana(2006)SMZ ilipigia marufuku matumizi ya simu za mkononi kwa wanafunzi wote wa shule za Msingi na Sekondari kwa madai kuwa, simu hizo zinachangia kwa kiasi kikubwa kwa wanafunzi kushiriki katika vitendo vya ngono, aidha wanafunzi hao wamekuwa wakipoteza muda mrefu kuandika meseji na kupokea simu wawapo darasani na katika maeneo ya shule.
Sasa SMZ imenyoshea mkono Disco kuwa imesababisha kwa wanafunzi wengi kufeli mtihani wa kidato nne wa mwaka jana. Hivyo ni marufuku kwa mwanafunzi yoyote wa shule ya msingi na sekondari kwenda Disco!
Hatua ya kupiga marufuku kwa wanafunzi kwenda kwenye madisco na kumbi za starehe zimepokelewa kwa mitazamo tofauti na waakazi wa visiwa hivyo, ambapo Disco na mojawapo ya sehemu ndogo tu ya Starehe zinazopatina kwenye visiwa hivyo.
Wanafunzi wengi wanakwenda katika madisco wakati wa sikukuu za Idd ambazo huwa ni mara mbili kwa mwaka, Madisco mengine yanayovuta wanafunzi wengi ni kama tamasha la Mwaka Kogwa ambalo hufanyika mara moja kwa mwaka na Tamasha la nchi za Majahazi. Zaidi wanafunzi huonekana kwenye maonyesho ya Muziki wa Kizazi Kipya. Madisco yote haya hufanyika kuanzia saa za maghalibi hadi usiku wa saa nne.
Katika kuona kuwa wanafunzi wa Visiwa hivyo wanafanya vizuri SMZ imo katika mipango ya kutenganisha wanafunzi kwa kuweka shule za jinsia moja tu. Mpango huu umeshaanzishwa kwa baadhi ya shule visiwani humo kwa lengo la kuwafanya wanafunzi hao wasome na kufaulu na sio kutongozana.
Mwaka jana Visiwa hivyo vilishuhudia amri ya kuwataka wanafunzi wa chuo cha "Zanzibar University College" kutochanganyikana(wanaume na wanawake) wakati wa kujisomea usiku, kwa madai kuwa chuo kimezagaa na kondomu zilizotumika!
Hatua za SMZ kutaka kuona kunakuwepo na matokeo mazuri ya mitihani kwa wanafunzi wake zichukuliwe kufuatana na mapendekezo kadhaa yaliyokwisha kutolewa huko nyuma. Kwanza SMZ imekwisha shauriwa mara kadhaa kuhusu kubadilisha mitaala yake ili iendane na ya Tanzania bara. Hata hivyo hadi sasa SMZ wanaonekana kuwa bado kuwa tayali kufuta pendekezo hilo, licha ya kujua manufaa yake kwa wanafunzi na wanakisiwa hicho kwa ujumla. Kinacho zuia kutofuatwa kwa pendekezo hilo hadi leo hakijulikani. Zaidi ni kwa serikali hiyo kuibuka na viamri vya ajabu ajabu kila kukicha! Kitendo cha kupiga marufuku marufuku hizi husababisha kuwafanya wanafunzi kuwa watukutu zaidi.
Kwa upande mwingine Wazazi nao wanapaswa kushirikishwa katika kila hatua ya maendeleo ya wanafunzi wanapokuwa shuleni na majumbani. SMZ inapaswa kushirikiana na wazazi kuona ni kwa kiwango gani wataweza kuongeza bidii ya wanafunzi katika masomo yao. Malezi bora kwa mwanafunzi husaidia kwa kiasi kikubwa kwa mwanafunzi kuwa na bidii katika masomo yake.
UNCEF wanathibitisha hilo kwa kuwa hata nchi zenye utajili mkubwa iwapo wanafunzi wake wanakosa malezi bora matokeo ni kufanya vibaya shuleni.
http://news.bbc.co.uk/2/hi/uk_news/6359363.stm
Posted by Kibunango at 15:52 6 comments
Tuesday 23 January 2007
Nungwi : Ukahaba, Nguo fupi na Ulevi hauna nafasi..
Posted by Kibunango at 19:15 10 comments
Sunday 21 January 2007
Mstakabala wa Soko la Usiku....
Posted by Kibunango at 22:32 0 comments
Thursday 18 January 2007
SMZ yafanya kweli
Posted by Kibunango at 21:41 8 comments
Tuesday 9 January 2007
Alijenga Baba na kamalizia Mtoto
Leo Wazenj na Watz wanasherekea siku ya Mapinduzi ya Zanzibar ukiwa ni mwaka wa 43. Mapinduzi hayo ambayo lengo lake kubwa ilikuwa kuwapa weusi wengi madaraka ya kujitalawa.
Tokea Mapinduzi kumeshapita awamu zaidi ya sita za uongozi wa ngazi ya juu kabisa visiwani humo, nikiwa na maana marais wa serikali ya mapinduzi, maarufu kama SMZ. Kila awamu iliingia na mambo yake waliyoona ni muhimu kwa wakati wao, zaidi kila awamu inakumbukwa kwa mazuri na mabaya waliyofanya.
Awamu ya kwanza ilikuwa na lengo la kuwawezesha wananchi walio wengi kuwa na maisha bora. Na hii ilithibitishwa na ujenzi wa nyumba bora katika kila pande ya kisiwa hicho. Juhudi za ujenzi huo zilifanyika kwa pamoja kati ya serikali na wananchi. Yaani wote walishiriki kikamilifu katika ujenzi wa nyumba tena wakitumia kila kitu katika kufanikisha azma ya serikali kuwapatia maakazi bora. Utaratibu uliotumika ni kuvunja nyumba ndogo ndogo zilizojengwa kiholela na kujenga nyumba kubwa za ghorofa. Mfano ni majengo ya Forodhani. Kwa upande mwingine nchi za ulaya nazo hazikuwa nyuma kuona wakaazi wa kisiwa hicho wananufaika, Ujerumani nao wakajenga nyumba za maendeleo katika mtaa wa Kikwajuni ambazo zilikuwa na kila kitu ambacho kinahitajika kwa maisha bora.
Awamu iliyofuata ikaona ni vema kuwa na nyumba nzuri vijijini vilevile, hivyo nayo ikajikita katika kujenga nyumba za vijiji huku wao wakitoa mafundi na vifaa vya ujenzi na wananchi wakifyatua matofali. Vijiji vikajengwa na wananchi wakahamia.
Awamu mbili zikapita pasipo kujishughulisha kabisa na masuala ya ujenzi wa nyumba, licha ya kuwepo na matatizo na kasoro nyingi katika ujenzi wa nyumba katika awamu zilizopita. Mojawapo ya matatizo ni kutomalizika kwa ujenzi wa Nyumba za Michenzani na baadhi ya nyumba za vijiji kukosa wakaazi. Aidha matatizo mabaya ya matumizi ya nyumba hizo na uchakavu wa nyumba. Mbaya zaidi ni kwa wale ambao walivunjiwa vibanda vyao kupisha majengo hayo waliendelea kusota pasipo kujua ni lini watanufaika na nyumba bora.
Awamu ya tano iliingia na aina mpya ya ujenzi wa nyumba, ambao uliitwa nyumba za mkopo nafuu, lengo likiwa ni ujenzi wa nyumba za kisasa kwa kuwauzia wananchi hasa wafanyakazi wa SMZ ambao wengi wao walikuwa hawana nyumba. Serikali ya Uchina ikajitutumua na kujenga nyumba za mkopo nafuu. Kasheshe ikaanza wakati wa ugawaji wa nyumba hizo, malengo yakapindishwa na waliopata wakapata na waliokosa wakakosa, malalamiko yakazidi na serikali kama kawaida yake ikaendelea kutoa ahadi kuwa zitajengwa zingine. Zaidi awamu hii ikachungulia na kule kwenye mabaki ya ujenzi wa nyumba za Michenzani. Wakajipanga na kumalizia block moja, wanainchi wakapata nyumba, kama vile haitoshi kukawepo na malalamiko kuwa nyumba nyingi wamepewa watu toka kisiwa cha pili.
Kuingia kwa awamu ya sita kukabadili kidogo sura ya ujenzi wa nyumba, wao wakaona ni bora kumalizia majengo ya Michenzani na kuwapa wale waliovunjiwa nyumba zao karibu miaka therathini na ushee! Wakawata watu hao kuwa wavumilivu kwani serikali haina fedha za kutosha ila nyumba zitamaliziwa.
Hapa sio kama zamani ambapo wananchi walishiriki ujenzi wa nyumba hizo. Sasa ikawa ni kazi ya serikali pekee kumalizia nyumba hizo. Pengine wananchi walishachoka kuisaidia serikali yao. Sijui.
Umaliziaji wa nyumba za Michenzani utakuwa ni furaha ya pekee kwa Rais Aman Abeid Karume. Kwani nyumba hizo zilijengwa na baba yake ambae alikuwa ndio rais wa kwanza wa SMZ. Pengine Karume ameshawishika kumalizia nyumba hizo ili kukamilisha ndoto za baba yake ambae alitaka kuona kuwa wananchi wake wanaishi katika nyumba zilizo bora kabisa. Aidha ni kuondoa kero za wale ambao walivunjiwa nyumba zao kwa mategemo ya kuishi kwenye nyumba bora, na kujikuta wakisubiri kwa zaidi ya miaka arobaini.
Mwisho napenda kuipongeza SMZ kwa kufikisha miaka 43.
Posted by Kibunango at 18:16 0 comments