Wednesday, 18 February 2009

E-governance for African Municipalities...Ni Wizi Mtupu....!


Zenj mara nyingi imekuwa ikiingia kwenye rekodi mbalimbali barani Afrika na Duniani kutokana na matukio ya maisha maendeleo na teknologia. Rekodi kadhaa zimeandikwa ndani ya visiwa hivyo, hivyo kuongeza umaarufu wake na wakati huo huo kuboresha huduma mbalimbali kwa wananchi wake.

Zanzibar inaendelea kujivunia rekodi zake mbalimbali hadi wakati huu ingawa zingine zilishindwa kuendelezwa na hivyo kubakia kwenye kumbukumbu tu na kuwa hadithi kwa vijana kutambiana na hasa wanapokuwa katika ubishi na wenzao wa bara. Mapema mwaka huu Zenj iliibuka tena na kujiwekea rekodi nyingine mpya katika Afrika ya Mashariki, na iwapo rekodi hii itakuwa na mafanikio hapana shaka itaanza kusambaa taratibu kwa nchi zote za jirani. Safari hii rekodi hiyo haikupokelewa vizuri na nchi jirani, hata hivyo nina hakika baada ya muda wataifuata tu. Hii ni rekodi ya kuwa nchi ya kwanza katika Afrika ya Mashariki kutoa leseni ya udereva yenye kumbukumbu zote muhimu za mwenye leseni pamoja na namba yake ya ulipaji kodi. Hii ni hatua nzuri na kubwa kwa nchi zenye matatizo ya ukusanyaji wa kodi.

Mafanikio haya yote siku zote yanakuwa na lengo moja kubwa la urahisishaji wa utendaji na uongezaji wa ufanisi katika utoajo wa huduma, ambapo ni hatua muhimu ya kuondokana na ukiritimba ambao umekuwa ukichangia kwa asilimia kubwa kuwepo na rushwa na hatimae ufisadi.

Hata hivyo sio mambo yote ambayo yamekusudiwa kufanikisha na kurahisisha utoaji huduma katika Zanzibar yamefanikiwa. Ni watu wachache ambao watakumbuka kuwepo na mradi wa E-governance for African Municipalities kwa Manispaa tano tu barani Afrika ikiwemo Zanzibar, Manispaa zingine zilikuwa ni Bamako (Mali), Maputo (Mozambique), Niamey (Niger) na Lusaka (Zambia). Lengo la mradi huu ambao ulianza mwaka 2001 ilikuwa ni kuziunganisha Manispaa hizo tano katika mtandao mmoja aidha kuwezesha Manispaa hizo kuwa karibu na wananchi wake kwa utoaji wa huduma ya habari kwa njia ya mtandao. Kwa Manispaa ya Zanzibar kupitia mtandao uliofungwa katika Idara zake zote ilikusudiwa kurahisisha ubadirishanaji wa habari za kiutendaji katika idara hizo kwa njia ya umeme(electronically). Zaidi ilikusudiwa kutoa habari juu upatakanaji wa leseni mbalimbali kwa wananchi wake kupitia kwenye tovuti yake, pamoja na wananchi hao kupata nafasi ya kutumia mtandao huo bure katika sehemu maalumu kwa ajili ya kupata habari juu ya sheria ndogo ndogo mpya, muhtasari wa vikao vya kamati za Manispaa na Baraza Kuu, ukusanyaji wa mapato na matumizi yake na kuweza kujionea bajeti ya Manispaa hiyo ndani ya mtandao.

Mradi huu ambao ulikuwa unadhaminiwa na DANIDA/UNESCO, ulikamilika mwaka 2003, ambapo pamoja na Manispaa kupatiwa vitendea kazi vyote na taaluma kwa watendaji wake, wadhamini hao waligharamia na uanzishaji wa tovuti ya manispaa hiyo, ambayo tokea mwaka 2003 hadi leo hii imedumaa. Huu ni wizi mtupu.

Mradi huu ulikuwa wa thamani ya dola za kimarekani elfu arobaini haukuweza kuendelea kama ilivyokusudiwa kwa sababu zisizo na msingi zaidi ya kuendeleza tabia za ukiritimba ndani ya vyombo vya utoaji wa huduma ambapo ni wizi mtupu.

Madiwani ambao kwa namna moja ama nyingine ndio wanao wawakilisha wananchi wao katika Manispaa, ilitegemewa wawe mstali wa mbele kuona huduma hii muhimu iliyokuwa inaweza kuwapunguzia bughuza za waombaji wa fomu kugonga milango ya nyumba zao alfajili, kuwabana wahusika kuikamilisha tovuti hiyo ili kuwezesha wananchi kujaza fomu online walikaa kimya na kufumbia macho kudumaa kwa mradi huu ili waweze kuendelea kuwazungusha wananchi wao juu ya upatikanaji wa fomu mablimbali... Huu ni wizi mtupu!

Mkurugenzi wa Manispaa ama kwa kutojua ama kushindwa kwenda na mabadiliko katika utoaji wa huduma nae alishindwa kuendeleza mradi huu. Kwa nafasi yake angeweza kuhakikisha kuwa kila Idara inapeleka taarifa zake za mapato katika tovuti hiyo na kila idara inaweka fomu za maombi katika tovuti hiyo na hivyo kupunguza ama kuondoa foleni zisizo na ulazima wowote katika Ofisi ya manipaa hiyo. Hata hivyo kwa miaka saba sasa amekaa kimya tokea alipoweka ada za kupaki magari mwaka 2003... Wizi mtupu!

Mstaki Meya ambae huwa anaalikwa kwenye matukio muhimu yote yanayofanyika katika Manispaa yake nae ameshindwa kumbana afisa uhusiano kuona kuwa Matukio muhimu yote yanawekwa katika tovuti hiyo, hii ingekuwa ni njia mojawapo ya kuelekea kuweka hata matangazo ya matukio kwa njia ya kulipia hivyo kuifanya tovuti hiyo kuingiza mapato. Nae kama wengine ameamua kukaa kimya... Ni wizi mtupu!

Tovuti ya Baraza la Manispaa ilifanyiwa marekebisho kwa mara ya mwisho mwaka 2003, na hata yale ambayo yamo katika tovuti hiyo yanatia kichefuchefu. Yaliyoandikwa humo yana uhusiano mdogo kabisa na shughuli za Manispaa hiyo huu ni wizi mtupu. Hata design na layout ya tovuti hiyo ni vichekesho vitupu... Yaaaani ni Wizi mtupu!

Thursday, 12 February 2009

Ni wiki ya Sauti za Busara (Sounds of Wisdom) huko Zanzibar



Tamasha la sita la Sauti za Busara limeshaanza rasmi siku ya Jana kwa maanandamo ya ufunguzi wa tamasha hilo ambalo sasa ni mojawapo ya tamasha kubwa kabisa barani Afrika. Tamasha hili litadumu kwa muda wa siku sita(12-18/02/2009)na tokea kuanza kwake limekuwa likifanyika katika wiki ya pili ya mwezi wa pili.

Tamasha la mwaka huu litatumbuizwa na wasanii maarufu toka karibu pande zote nne za Afrika, kwa mjibu wa tovuti ya sauti za busara wasanii ambao wana washabiki wengi kwa mwaka huu ni Bi Kidude, Culture Musical Club, DJ Yusuf, Samba Mapangala & Orchestre Virunga, Jagwa Music, Best of WaPi, Iddi Achien'g, Natacha Atlas, Segere Original na Joh Makini

Kwa habari zaidi tembelea hapa chini

Tuesday, 10 February 2009

Kichekesho kingine toka kwa Shamsi Vuai Nahodha



Mwishoni mwa mwezi Januari mwaka huu, Waziri Kiongozi wa Serikali ya Mapinduzi alinifanya nicheke kwa kauli yake ya kuamua kushika fagio na kuanza kufagia barabara za Zenj kutokana na barabara hizo kujaa michanga na vumbi kiasi cha kutojulikana kama ni za kiwango cha lami au la. Hii si mara ya kwanza kwa Mh. Nahodha kujitolea kusafisha Halmashauri ya Manispaa ya Zanzibar. Hata hivyo pamoja na juhudi zake hizo kwa Halmashauri hiyo ambayo kipindi fulani kupitia kwa Mkurugenzi wake Mr Mabrouk Makame Jabu ilikuwa ikidai kupewa hadhi ya Jiji(Sina hakika kama tayali ombi hili limeshakubaliwa)bado mji huo umeendelea kuwa mchafu.

Juhudi zote za Waziri Kiongozi zimekuwa na mafanikio ya muda mfupi, kwani huwa zinafanyika katika mtindo wa Operation ambao siku zote huwa hauna uendelevu wa aina yoyote, kwani operation inapokwisha shughuli nzima uwekwa kando na watu wakaendelea na shughuli zao zingine, huku wakisubiri kutokea kwa operation mpya. Watendaji wengi na hasa wa kimacha chini upenda aina hii ya utendaji kwani ndio wakati wao wa kuwa na kipato zaidi kutokana na overtime. Kwa Waziri Kiongozi ambae mara kwa mara amekuwa akisisitiza kuwepo na utendaji wa uendelevu katika shughuli za serikali, kilimo na biashara huku akiongoza kufanya operation za usafi ni kichekesho kitupu. Inakuaje unahutubia kila siku mambo ya uendelevu huku kazi unafanya za kizima moto kama sio vituko vitupu!

Moja ya barabara ambao siku zote huwa inajaa michanga na kusababisha vumbi la kuweza kusababisha chafya kila baada ya sekunde kadhaa, na hatari ya kupata kikohozi kikali ni barabara ya Benjamin Mkapa(zamani creek road). Barabara hii ndio inatenganisha Mji Mkongwe na Ng'ambo, ni moja ya barabara yenye pilika kubwa kabisa katika Zenj ikipitiwa na magari mengi zaidi, itumiwayo na wapanda baiskeli wengi zaidi na wapanda vespa,huku wakipigana vikumbo na mamia ya watembeao kwa miguu. Ndio barabara pekee visiwani humo yenye taa za kuongozea magari, kwa ufupi ndio barabara maarufu kabisa visiwani humo.

Kwa miaka nenda rudi barabara hiyo imekuwa ikifagiliwa pasipo kutakata na sasa naona imeshakuwa sugu, na kama hakuna mipango ya kuweza kujua ni kwa nini barabara hiyo haikosi vumbi licha ya kuwa ndio picha ya mji wa Zenj, kamwe haitokuja kuwa safi na ni wazi kuwa vumbi litaendelea kuwepo tu, licha ya ombi la watendaji wa Halmshauri hiyo kununuliwa gari la kufagia barabara hivi karibuni.


Barabara hiyo pamoja na kupita katika bustani za Mnazi Mmoja, Jamhuri, Donge na viwanja vya Malindi, haikupaswa kabisa kuwa na vumbi. Lakini kutokana na sababu za kutokuwa na mipangilio mizuri vumbi limeendelea kuwepo licha ya ufagiaji wa kila siku. Kitu cha kwanza ambacho kina kasoro kubwa katika barabara hiyo ni kukosekana kwa njia ya watembeao kwa miguu. Kama kungekuwa na njia hiyo ingetumika vile vile kama buffer ya kutenganisha barabara na sehemu zinazoingiza michanga barabarani na kusababisha vumbi. Aidha aina za kuegesha magari na hasa teski katika barabara hiyo unachangia kuingia kwa michanga barabarani, kuna maegesho ya magari ya mizigo na haya uegeshwa karibu kabisa na barabara hiyo, hivyo uchangia kuingia kwa michanga barabarani.Kwa upande mwingine Feeder road zinazo ingia katika barabara hiyo vile vile uchangia kuingiza michanga.

Ili kumfanya Waziri Kiongozi aendelee kufanya kazi zake za kawaida, badala ya kutafuta fagio, upo umuhimu wa lazima kuona kuwa barabara ya Benjamin Mkapa inafanyiwa mabadiliko makubwa ili kukidhi mahitaji ya watumiao barabara hiyo ambao ni maelfu. Kuna umuhimu wa kuweka njia kwa watembeao kwa miguu ambayo iwe inafanya kazi ya kuzuia kuingia kwa michanga katika barabara hiyo. Kuboresha maegesho ya teski na magari ya mizigo kama kituo cha daladala kilivyoboreshwa, kufanyia matengenezo feeder roads ambazo huingiza michanga kwa wingi na hasa wakati wa masika. Kuangalia tena eneo la Darajani kwani nalo linachangia sana katika uchafuzi wa barabara hiyo. Maeneo mengine kama Mkunazi,Donge, Ben Bella na Ofisi za Zec zinatakiwa kuangaliwa kwa vizuri zaidi.

Kwa utengenezaji wa njia ya wapita kwa miguu, Halmashauri ya Manispaa ya Zenj, inaweza kufanya kazi hiyo kwa kutumia mitambo yake mikubwa ya kutengeneza vigae, kwa kuweka vigae pembeni ya barabara hiyo. Hizo milioni 135,000,000 ambazo Manispaa wanahitaji kwa ununuzi wa mashine ya kusafisha barabara mnaweza kuwapa japo nusu yake ili waweze kutumia kwa utengenezaji wa vigae.

Friday, 6 February 2009

Athari za Utalii kwa Mazingira ya Zanzibar




Moja ya masharti wanayopewa watalii mara waingiapo Zenj, ni juu ya uvaaji wa nguo ambazo hazistiri mwili mzima, yaani uvaaji wa suruali kipande, vichupi, ama kutembea vifua wazi ni sawa na kwenda uchi ndani ya Zenj. Hivyo watalii uambiwa wavae nguo zinazofunika mwili wote wakati wao wote watakapo kuwepo visiwani humo. Kwa watalii sharti hili ulipokea kwa shingo upande kwani wanapotoka ni sehemu za baridi na kwa muda mrefu wanakuwa wakivaa nuo nyingi kujikinga na baridi, na hivyo wanapotalii katika nchi za joto hupenda kuipa nafasi miili yao kufaidi joto hilo ambalo kwao ni adimu.

Hata hivyo linapokuja suala la ujenzi wa hoteli za kitalii Masharti na Taratibu zake hazijulikana kabisa, kwani vyombo vinavyosimamia ujenzi huo havina ushirikiano wa moja kwa moja na Idara ya Mazingira ambayo ipo kisheria kusimamia mazingira ya Visiwa hivyo chini ya sheria ya mwaka 1996.

Utalii katika visiwa vya Zanzibar sasa umeshapanuka sana na visiwa hivyo vimeshashuhudia mambo mengi yaliyokuja na utalii, ikiwa ni pamoja na ujenzi wa hoteli nyingi za kitalii karibu kwa fukwe zote visiwani humo pamoja na visiwa vidogo dogo, ongezeko la wageni wahamiaji kwa ajili ya kazi za kitalii, ongezeko la uvuvi kwa ajili ya vyakula vya watalii, ongezeko la safari za anga na ardhini, ongezeko la maduka rasmi kwa ajili ya watalii na mambo mengine mengi yanayoendana na utalii kwa ujumla.

Mengi katika haya yalikuja pasipo kwa wenyeji wengi kujiandaa na sasa inakaribia miaka ishirini tokea mfumuko wa utalii visiwani kuanza, na kumekuwepo na malalamiko mengi toka ndani ya visiwa hivyo na nje ya visiwa hivyo kwa jinsi suala zima la utalii lilivyobadili mambo mengi visiwani humo. Wenyeji wengi wanalalamikia sehemu kubwa ya ajila kushikwa na wageni, ongezeko la bei kwa vyakula vya baharini, kupigwa marufuku kutembea ama kuvua katika baadhi ya hoteli hizo. Huku asasi za kimataifa zikipigia kelele uharibifu wa mazingira kutokana na aina za ujenzi wa baadhi za hoteli visiwani humo, uharibifu wa coral reef kutokana na uvuvi uliokithiri, kutokuwepo na miundo mbinu ya kutosha kwa ajili ya kuhifadhi maji taka na utupaji holela wa taka toka mahotelini humo.

Hadi kufikia mwaka 2003 takwimu za ZIPA zinaonyesha kuwa, jumla ya miradi 242 ilidhinishwa yenye thamani ya jumla ya dola za kimarekani milioni 403. Mwaka 2001 Zanzibar iliingiza dola za kimarekani milioni 46 kutokana na utalii pekee ikiwa ni asilimia 15 ya GDP. Makisio yanaonyesha kuwa kutakuwa na ongezeko la asilimia 21 la GDP kufikia mwaka 2012 na kufanya mgawanyo wa mapato kufikia million 116(makadirio haya yalifanyika kabla ya Global recessionya mwaka huu).

Ripoti ya maendeleo ya utalii ya Zanzibar iliyoandaliwa na na UNDP inaonyesha kuwa katika mwaka 1983 kulikuwa na sehemu kumi tu za malazi visiwani humo zenye vyumba 215 na jumla ya vitanda 467 ambazo hazikuwa kwenye daraja la aina yoyote(utalii au malazi ya wageni wa kawaida). Leo hii sekta ya utalii visiwani humo ina sehemu zaidi ya 180 za malazi, zenye zaidi ya vyumba 3160 na zaidi ya vitanda 6490.

Kufikia mwishoni mwa mwaka 2006, ripoti ya Umoja wa Mataifa(UN) ilionya kuwa Zanzibar imekuwa mojawapo ya nchi duniani inayoongoza kwa uchafuzi wa mazingira ya baharini kutokana na umwagaji wa maji taka katika bahari ya Hindi pamoja na uharibifu wa vyanzo vya maji. Mtafiti Stefan Gossling toka Sweden, yeye alionya kuwepo na uharibifu mkubwa wa coral reef kwa lengo la uuzaji wa viumbe vyake kwa watalii. Maeneo yenye uharibifu mkubwa wa mazingira kutokana na utalii visiwani humo ni ya Kaskazini na yale ya Mashariki.

Ukuaji wa utalii, licha ya kuendelea kuharibu mazingira umesababisha kuwepo na ushirikiano mdogo kati ya serikali na wananchi wake. Kwa upande wa mazingira wananchi wengi wanalalamikia hatua kadhaa za wenye hotel kuwanyima sehemu zao za uvuvi, ulimaji(seaweeds), minazi na hata kutembea karibu na hotel hizo. Mwaka 2002 wananchi wenye hasira katika kijiji cha Kendwa walichoma moto hoteli ya kitalii kwa madai ya hoteli hiyo kuharibu coral reef, tabia hii ilisambaa kwa baaadhi ya vijiji vya Nungwi.

Baadhi ya hotel( Fundu lagoon, Matemwe Bungalow, Blue Bay, Mnemba Island na Chumbe) zimeonyesha kujali athari ambazo zinatokana na ujenzi wa hoteli zao kwa mazingira. Wamejitahidi kufuata aina za ujenzi usio tumia resources kwa wingi, aidha wamejitahidi kufuata aina ya ujenzi wa nyumba za vijiji zinavyowazunguka. Hivyo kupunguza uharibifu wa maji safi na bahari.

Serikali kwa upande wake imeendelea kutoa vibali vya ujenzi pasi kuzingatia uharibifu wa mazingira au namna ya kujenga pasipo kuwepo na uharibifu wa mazingira. Hoteli zinaendelea kujengwa pasipo kuwepo na mfumo unaotambulika wa ukusanyaji na usafishaji wa maji taka, ukusanyaji na utupaji wa taka ngumu na utunzaji wa vyanzo vya maji. Aidha hakuna taratibu zozote ambazo zinatolewa kwa kutumia materials ambazo zinaendana na mazingira ya fukwe zinazojengwa.

Na kama kawaida yao, mambo yanapokwenda kombo, viongozi huja na amri kede kede. Nakumbuka miaka miwili iliyopita Mh. Mansour Yussuf Himid alinukuliwa akisema;
“Serikali imegundua ukiukwaji wa taratibu za utunzaji wa mazingira katika ukanda wa fukwe”
Aidha alikubali kuwa sekta ya utalii ndio inaongoza katika uchafuzi wa mazingira visiwani humo na kuzitaka Idara zinazohusika kujipanga kukabiliana na tatizo hilo hilo, huku Ofisi ya Mwanasheria Mkuu ikisema kuwa yeyote ambae atakiuka taratibu za Mazingira ataburuzwa mahakamani na kupigwa faini ya Sh million 2 ama kwenda Chuo cha Mafunzo kwa kipindi cha miezi sita.