Wednesday, 25 March 2009

Huu Ndio Wakati Muafaka wa Kumiliki gari la Waziri wa SMZ


Mara kadhaa nimewahi kuandika juu ya ubabe wa SMZ dhidi ya Mahkama za Zenj, zaidi ya SMZ hata wananchi wakati mwingine wamekuwa na ubabe dhidi ya maamuzi ya Mahkama za Zenj. Kumekuwepo na hukumu mbalimbali kila siku, ila zinazonipa mashaka ni zile hukumu za kesi za madai. SMZ kama mhimili wa Mahkama imekuwa kwa mara kadhaa ikishitakiwa katika kesi za madai kutoka na ubabe wake wa kushindwa kufuata sheria zake.

Kesi nyingi ambazo SMZ na asasi zake zimekuwa zikijikuta matatani zinatokana na matatizo ya ardhi na madeni yanayotokana na huduma mbalimbali wanazoomba kufanyiwa na hatimae kushindwa kulizipia. Mwaka 2006 niliwahi kuandika jinsi gani Mahakama za Zenj zinapoonja ubabe wa SMZ na wananchi wake kiasi cha mtu kujiuliza iwapo utakuwa na matatizo ambayo yanahitaji haki kutendeka utakimbilia wapi!

Mwaka huo wa 2006 kulikuwa na kesi mbili za muda mrefu ambazo zilipata hukumu yake, lakini zikakutana na ubabe wakati wa utekelezaji wake, kama inavyoelezwa kwa kirefu chini ya bandiko la "Mahakama za Zenj na Matatizo ya Ubabe"

SMZ kwa kujua au kwa makusudi kabisa imekuwa ikipuuza madai mengi ya wananchi wake dhidi ya asasi yake. Nakumbuka kesi nyingi katika hili lakini moja iliyonivutia ni ile ya asasi moja ya SMZ kuibeza amri ya Mahkama kuhusu uvunjaji wa mabanda ya biashara ili kupisha ujenzi wa soko katika eneo la Mwanakwerekwe.

Wengi wa wananchi wamekuwa na madai mbalimbali na wanapokimbilia katika vyombo vya SMZ ili kupata suluhisho, uvunjika moyo jinsi wanavyosumbuliwa na inahitaji moyo wa ziada kwenda Mahakamani ambako ni sawa na kumpa Nyani kesi ya Ngedere. Binafsi nimekuwa nikipigwa tarehe zaidi ya miaka tisa kwa madai ya haki yangu ambayo niliingia mkataba na SMZ.

Hatua ya Mahakama Kuu kupiga mnada magari ya SMZ kwa kushindwa kulipa deni lake la matengenezo ya ikulu ndogo huko Pemba ni ya kuungwa mkono sana. Amri hii iwapo itafanikiwa itakuwa ya kuigwa na kupigiwa mfano. Moja ya mali ambayo inaweza kupigwa mnada ni gari la Mh. Waziri ambae wizara yake inahusika moja kwa moja na kushindwa kufuata taratibu za kuheshimu mikataba. Nategemea jeshi la polisi visiwani humo kusimamia vizuri ushikwaji wa mali hizo za SMZ na hatimae kupigwa mnada. Hii inaweza kuondoa usingizi mzito kwa watendaji wa SMZ kuhusu kuheshimu mikataba wanayoingia.

Tuesday, 24 March 2009

Agha Khan na Mji Mkongwe....

Agha Khan Development Network kwa zaidi ya miaka kumi sasa imekuwa ikifanya ukarabati mkubwa katika baadhi ya Majengo ya Mji Mkongwe wa Zanzibar. Na hivi karibuni walikuwa katika hatua za mwisho mwisho za kukamilisha ukarabati wa Forodhani Park.
Leo nitaangalia majengo mawili, nikianzia na Stone Town Culture Centre maarufu kama Old Dispensary ambalo ni mojawapo ya majengo yaliyofanyiwa ukarabati na AKDN baada ya kutupwa na SMZ. Aidha jengo lingine lililolembewa na SMZ ni Extelcom, ambalo leo hii kuingia ndani ya jengo hilo inabidi uwe nazo mfukoni.

Old Dispensary.

Jengo hili ujenzi wake ulikamilika mwaka 1894 chini ya ushauri wa kihandisi toka Uingereza. Michoro na mafundi wa jengo hili ni kutoka India ambako ndipo alipotoka mwenye jengo Bw. Tharia Topan ingawa hakuweza kuona kukamilika kwa ujenzi wa jengo hilo.

Mjane wa Topan aliweza kuendeleza ujenzi na baadae kuliuza. Lengo la Topan lilikuwa kujenga shule na zahanati, ambapo mmiliki wa mwisho wa jengo hilo aliweza kufanya sehemu ya chini ya jengo hilo kuwa zahanati na sehemu ya juu kuwa sehemu ya makaazi yake. Huu ndio ukawa mwanzo wa jina maarufu la Old Dispensary.

Miaka 70 baadae jengo hilo likawa tupu, na kuendelea kuwa tupu huku likiendelea kuchakaa na kuharibika ni hadi pale Agha Khan walipopewa ruhusa ya kulifanyia ukarabati ili kunusuru ufundi mkubwa uliotumika katika ujenzi huo kupotea na hasa nakshi zake za kihindi.


Miaka 100 baadae Agha Khan waliweza kupata kibali cha ukarabati wa jengo hilo, zaidi walipewa mkataba mpya wa kukodishwa jengo hilo na SMZ chini ya muda maalumu. Pichani hapo juu ni old dispensary baada ya kufanyiwa ukarabati mkubwa .


Extelcom
Jengo lingine ambalo lilikuwa chini ya SMZ na kuachwa bila aina yoyote ile ya usimamizi hadi pale walipotokea tena agha khan na kuamua kuligeuza toka ofisi hadi kuwa hoteli ya kitalii. Sasa jengo hili linajulikana kama Serena Inn

Thursday, 19 March 2009

Movie...Hobbie iliyokwisha huko Zenj


Jengo hili sasa halitumiki tena kama jumba la Sinema..!

Wednesday, 18 March 2009

Amin Salmin Amour, aonja tamu ya siasa

Ni baada ya kushindwa kutamba kwenye kura za awali za kumtafuta mgombea kwa tiketi ya CCM katika jimbo la Magogoni huko Zenj. Amin ambaye ni mtoto wa rais mstaafu wa Zenj Salmin Amour maarufu kama Komandoo, alikuwa ni miongoni wa wagombea 10 wa CCM waliojitokeza kuwania nafasi hiyo.

Umaarufu wa Amin unakwenda nyuma zaidi kipindi cha kwanza cha Komandoo Salmin alipokuwa madarakani,umaarufu wake ulijengeka kwa kuwa mjasirimali zaidi ya siasa na kwa kujaribu kila aina ya biashara za muda mfupi! Hatua yake ya kuingia kwenye siasa kwa wengi ilikuwa ni karata yake muhimu ya kujinyanyua tena baada ya kushindwa kudumu katika sekta ya biashara.

Kwa habari zaidi tembelea hapa

Sunday, 8 March 2009

Nani Mjinga Hapa?


Pichani ni mwanamke wa kizenj akiwa katika pilika pilika zake ufukweni, na pembeni kushoto ni mtalii akicheza na maji.

Jaribu kuangalia tofauti ya mavazi kati ya wanawake hawa wawili, halafu jaribu kufikilia hali ya hewa ya Zanzibar, bila kusahau udhaifu wa ngozi za watalii dhidi ya jua kali la ikweta.

Je unafikili kati ya hawa wanawake ni nani mjinga kutokana na aina ya mavazi yake?

Friday, 6 March 2009

Maji ya Karume Bai bai, Karibu maji ya Japan



Kwa muda mrefu kisiwa cha Zanzibar kimekuwa kikipata huduma ya maji bure, hatua ambayo ilitokana na mapinduzi ya mwaka 1964. Huduma hiyo muhimu kabisa katika maisha ya kila siku ya binadamu ilibatizwa jina na kuitwa maji ya Karume. Hata hivyo jina hilo halikuja burebure tu! kuna sababu kadhaa ambazo zilisababisha maji hayo yaitwe ya Karume. Moja ya sababu kubwa ilikuwa ni upungufu wa maji na hasa katika halmashauri ya manispaa ya Zanzibar,ambapo wananchi wengi walijikuta wakitafuta maji sehemu mbalimbali za manispaa hiyo. Usumbufu wa upatikanaji wa maji ulisababisha maji hayo kuitwa Maji ya Karume ambayo yalikuwa ni bure lakini shida kupatikana.

Maendeleo yote yaliyotokana na mapinduzi yaligeuka kuwa adha na kero baada ya maji kupungua katika manispaa, Majengo kama ya Mjeru pale Kikwajuni ambayo yalikuwa yakipata maji muda wote yalijikuta yakikosa maji muda mwingi wa mchana na maji yaliweza kutoka usiku tu, na ni usiku wa manane, hivyo kuwafanya wakaazi wake kubadilisha ratiba ya kulala ili waweze kukinga maji. Hali hii ilikuwepo kwa maeneo ya Kilimani, Michenzani na sehemu kadha wa kadha katika manispaa hiyo.

Ukosefu wa maji ya kutosha katika maeneo hayo ambayo yalikuwa na nyumba za ghorofa kulisababisha kubadilika kwa sura za majumba hayo kwa uwekaji wa pump za maji,nyingi katiya hizo kufungwa kienyeji tu na kuendelea kuwa kero kwa wananchi hao. Aidha uchimbaji wa makaro makubwa ya kuhifadhia maji chini ardhi ulishamiri na kupunguza upatikanaji wa maji hayo machache/kidogo kwa wakaazi wengine. Uchimbaji wa visima vile vile ulishamiri kando kando ya manispaa hiyo. Hii yote ilitokana na upungufu mkubwa wa maji ya Karume.

SMZ kwa upande wake walijitahidi kuona kero hiyo inaondoka, lakini mara zote miradi ya maji yenye nia ya kuwa endelevu ilishindwa kuendelea kutokana na SMZ kuendelea kupendelea kuwa na Maji ya Karume.

Wananchi kwa upande wao walikuwa tayali kulipia huduma za maji,hii inaonyeshwa na mifao kadhaa ya baadhi ya wananchi walioamua kutafuta njia za kudumu za upatikanaji wa maji katika maeneo yao. Miradi mingi midogo midogo ya maji iliyowashirikisha wananchi ilifunguliwa na mingi katika hiyo ilitumika kama mifano katika hatua za awali za semina mbalimbali za kubadili msimamo wa serikali na maji yao ya Karume.

Maji ya Karume yalianza kuaagwa rasmi tokea mwaka jana, hata hivyo sio wananchi wote ambao wameweza kupata maji ya Japan licha ya Idara ya maji kuwatumia ankara za maji. Hii kwa upande mmoja inaonyesha kuwa Idara ya Maji bado haijawa makini katika kuona kuwa maji yanalipiwa na yule tu ambae mfereji wake haukauki maji, na sio wale wenye mifereji iliyokauka au ile yenye kupiga filimbi kama maji yanakuja kumbe la..!

Udhaifu huu unathibitishwa na Waziri wa Maji, Ujenzi, Nishati na Ardhi,Bw, Mansour Yussuf Himid katika kauli yake aliyoitoa hivi majuzi wakati wa kusaini awamu ya pili ya maji ya Japan

``Napenda kutoa wito kwa wale wanaopata huduma ya maji kukubali kuchangia na wale wasiopata hawatatozwa fedha hadi hapo watakapoanza kupata maji ya uhakika,``

Tuesday, 3 March 2009

Bwejuu Zenj, ina beach nzuri kabisa hapo Afrika Mashariki

Inashikilia rekodi hiyo kwa miaka miwili sasa...
Ni kivutio kikubwa cha watalii katika Zanzibar




Ever wanted to feel like a castaway in a warm, secluded oasis of tranquility and beauty? Conde Nast Traveler has scoured the globe to find the best island beaches.
Following is a list of their top 10 choices:
1. Shipwreck Beach, Zakynthos, Greece -- This is an idyllic, isolated beach scooped out of a vertical wall of white rock.

2. Cumberland Island, Georgia -- With only 300 visitors allowed per day it equates to about 18 tourists per mile of beach.

3. Anse Victorin, Fregate Island, Seychelles -- Almost deserted, the crescent-shaped beach has soft sand, clear, tranquil water and a backdrop of palms and cliffs.
4. Lido, Venice, Italy -- The ultimate seaside resort made famous by author Thomas Mann in Death in Venice.

5. 7-Mile Beach, Negril, Jamaica --The right mix of white sand, tranquil water and enough beach life to keep anyone from getting bored.

6. Gibson Beach, Sagaponack, New York -- With no amenities of any kind, this wild swath of dunes, surf and fabulously wealthy homes is a beach that attracts Manhattan's beautiful people. With minimal parking, cycling is a preferred transport.

7. Cocoa Island, Maldives -- Tiny Cocoa Island is virtually all beach.

8. Bwejuu, Zanzibar, Tanzania -- It's one of the most exotic of Africa's islands and Bwejuu is its wide and blindingly white beach.

9. Kamala Beach, Phuket, Thailand -- The western shores are thick with beaches, and many of those beaches are bustling with commercial activity including food vendors, gift shops, bars and other distractions. Kamala is the antidote. Kamala Bay's main street is a convivial integration of seafood restaurants, shops, and bars that are notably tamer.

10. Waikiki, Oahu, Hawaii -- There's no such thing as boredom in Waikiki. The shops, restaurants and parks of Honolulu are just a block away.

Wednesday, 25 February 2009

Wikipedia ya Kiswahili

Watanzania wote wanakaribishwa kuchangia habari za mahali wanapoishi au wanapotoka katika wikipedia ya Kiswahili! (sw.wikipedia.com) Ijulikane ya kwamba wikipedia ni mradi mkubwa wa elimu unaojengwa na wachangiaji wanaojitolea bila malipo yoyote. Kila mtu anakaribishwa kuchangia!

Kwa sasa tumeanzisha makala fupi za kila kata kwenye mikoa ya Arusha, Dar es Salaam, Dodoma, Iringa, Kilimanjaro, Kigoma, Lindi, Mara, Mwanza, Mbeya, Manyara, Morogoro, Mtwara, Pwani na Tanga.

Angalia mfano huu: sw.wikipedia.org/wiki/Mkoa_wa_Mjini_Magharibi_Unguja

Chini kuna sanduku inayoonyesha mikoa yote. Ukiingia katika mkoa fulani unapata majina ya wilaya. Kila safari ukibonyeza kwenye neno lenye rangi ya buluu unapelekwa kwenye makala mpya. Ukifika kwenye wilaya utaona sanduku lenye majina ya kata za eneo hili. Makala mengi yana habari fupi tu kama "ABC ni kata ya wilaya DEF katika Mkoa wa XYZ. Idadi ya wakazi wake ilihesabiwa kuwa xxxxx katika sensa ya 2002". Kila mtu yuko huru kubonyeza kwenye sehemu ya "hariri" juu ya makala na kuongeza habari.

Baada ya kuongeza habari unabonyeza sehemu ya "Hifadhi ukurasa" iliyoko chini.


Taarifa hii imeletwa kwenu kwa hisani kubwa ya Bw. Kipala anayesimamia kamusi hiyo

Tuesday, 24 February 2009

Zanzibar Hakuna Sheria za Ujenzi?

Zanzibar kama nchi, mji mkuu wake ni Zanzibar ambao unaundwa na Mji Mkongwe na Ng'ambo, kiutawala upo katika mkoa wa Mjini Magharibi. Mji wa Zanzibar unapata huduma zake kupitia Halmashauri ya Manispaa ya Zanzibar na Mamlaka ya Hifadhi na Uendelezaji wa Mji Mkongwe.

Halmashauri ya Manispaa kama halmashauri zingine duniani imepitia katika mabadiliko mengi ya kiutawala na sheria za kuongoza mji huo na hasa katika suala zima la ardhi na maendeleo yake kwa kushirikiana na idara zingine kama ofisi ya Mkuu wa wilaya, ofisi ya Mkuu wa Mkoa, Kamisheni ya Ardhi na baadae Idara ya Mipango Miji na Idara ya Ardhi.

Masterplan ya kwanza kabisa ya mji wa Zanzibar ilitolewa mwaka 1923 chini ya sheria ya mji(Town Decree Cap 79). Master plan ilitolewa kutatua matatizo ya ukuaji wa mji kiholela, kupanua wigo wa miundo mbinu na kurahisisha mizunguko katika mji huo ambao ulikuwa na watu 35000 huku asilimia 30 ya watu hao wakiishi Mji Mkongwe na asilimia 70 wakiishi Ng'ambo sehemu iliyokithiri kwa ujenzi holela.

Mwaka 1958 kulifanyika mabadiliko katika Master plan kwa kuingizwa kwa "Town Scheme" chini ya sheria ya mwaka 1955- "Town and Country Planning Decree" ambapo lengo lilikuwa kuandaa rasimu ya usafirishaji/usafiri katika mji mkongwe na kuendeleza maeneo ya wakaazi yaliyopimwa chini ya viwango huko Ng'ambo (semmi planned settlements)

Master plan ya pili "The Town Master Plan -1968" ilifanywa na Wajerumani, ikiwa na lengo la kuboresha zaidi maeneo ya Ng'ambo ambayo yalikuwa yakipanuka kwa kasi, huku umuhimu mkubwa ukiwekwa kwenye upatikanaji wa huduma muhimu kama vile mifereji, taa za kwenye mitaa na misingi ya maji taka.
Mafanikio yake ni pamoja na Majumba ya Mjeru pale Kikwajunina Majumba ya Kilimani.

Master plan kubwa na ya mwisho ilitolewa mwaka 1982 na wataalmu kutoka China. Pamoja na mabo mengine, master plan hiyo iliangalia zaidi kupanuliwa kwa mji wa Zanzibar kwa kupima maeneo mengine mapya ili kuruhusu nafasi kubwa zaidi kwa ya asilimia 68 ya wazenj waliokuwa wamebanana kupatiwa maeneo ya ujenzi huku wengi wakiishi katika maeneo yasiopimwa kisheria, aidha kutoa nafasi kubwa zaidi ya ujenzi kuanzia nyumba za kuishi shule na maeneo ya biashara, ilitizama vilevile kupunguza umwagaji wa maji taka baharini na kuzuia tabia iliyoanza ya kujenga nyumba katika maeneo yenye mafuriko.

Tokea master plan hiyo ya wachina kumekuwepo na nyongeza mbili moja ikiwa ni ya mwaka 1996 The Tourism Zoning Plan ambayo iliingizwa kwenye Master plan kukidhi mahitaji ya mahoteli na maeneo ya kitalii. Ya pili ni pendekezo la kuimarisha na kuanzisha miundo mbinu hasa katika maeneo ya Ng'ambo iliyopendekezwa na Zanzibar Sustainable Programm (ZSP) mwaka 1998.

Kwa nyakati tofauti maendeleo ya ujenzi na udhibiti wake yalikuwa yakisimamiwa na Joint Building Authority (JBA)ambayo ilianzishwa chini ya sheria ya Town and Country Planning Decree (cap 85) ya mwaka 1955, ikiwa na wajumbe watatu toka ambao ni Mkuu wa Afya, Mkuu wa Wilaya na Building Inspector. Kazi zao kubwa ilikuwa ni kutoa vibali vya ujenzi wa aina zote ndani ya mji wa Zanzibar na kudhiti ujenzi ndani ya mji huo kwa mujibu wa sheria ya mji. "Town Decree Cap 79 Subsidiary"

Mwaka 1969 SMZ ilizivunja Halmshauri za Miji na hivyo ukawa mwisho wa awamu ya kwanza ya JBA. Awamu ya pili ya JBA ilianza tena mwaka 1986 baada ya kurejeshwa kwa serikali za mitaa katika ikiwa na wajumbe wengi zaidi huku mkuu wa mkoa akiwa ndie mwenyekiti wake. Wajumbe wengi walitoka baraza la Manispaa, wakifuatiwa na wajumbe toka idara ya Ardhi, idara ya Upimaji na Mhandisi wa ujenzi. Kazi za JBA ziliendelea kufanyika chini ya sheria na taratibu za ujenzi kama zinavyooneshwa katika Cap 79 Subsidiary. Kati ya Mwaka 1969 na 1986 shughuli za ujenzi zilikuwa zikisimamiwa na serikali za majimbo, pasipo kufuata sheria yoyote za ujenzi zaidi ya uzoefu uliopatikana katika Cap 79 ya Town Decree.

Mwaka 1994 Sheria ya uendelezaji na uhifadhi wa Mji Mkongwe ilianza kufanya kazi, hivyo kuitoa JBA kama mdhibiti wa ujenzi katika eneo la Mji Mkongwe. JBA iliendelea kufanya kazi kufuata mipaka ya Master plan ya mwaka 1982 nje ya Mji mkongwe hadi mwaka 1995 ambapo kulitokea tena mgongano wa sheria. Mwaka 1995 ilianzishwa sheria mpya ya halmashauri za Miji Zanzibar, ikichukua sehemu kubwa za sheria za Town decree na kupunguza ukubwa wa Manispaa ya Zanzibar hali kadhalika kuibana zaidi JBA katika utendaji wake.

Kufikia hapa kazi za JBA ziliendelea kufanyika ila ni kwa ubabe tu, kwani chini ya sheria ya mwaka 1995 ya Manispaa ilionekana wazi kuwa JBA haikuwa na nafasi ya utendaji katika manispaa yenyewe na wilaya ya Magharibi. Ikiwa chini ya Mkuu wa Mkoa kama mwenyekiti na Baraza la Manispaa kama katibu, JBA iliendelea kufanya kazi huku ikijua inafanya hivyo kinyume na sheria na taratibu. Udhaifu wa Halmashauri ya wilaya ya Magharibi, nguvu ya kisheria ya Idara ya Ardhi na Idara ya Upimaji iliipa uhai kidogo JBA kutokana na kuwa na wajumbe toka katika Idara hizo.

Mwaka 2000 JBA ilivunjwa rasmi na moja ya sababu kubwa ya uvunjwaji wake ilikuwa ni zoezi la uvunjaji wa nyumba katika mitaa kadhaa ya Mkoa wa Mjini Magharibi iliyofanyika katika mwaka 1996, katika vyanzo vya maji, karibu na njia ya grid ya umeme wa Kidatu na maeneo mengine yaliyovamiwa, ambapo ilionekana zoezi zima limefanyika kisiasa zaidi kuliko kufuata taratibu. Manispaa kwa upande mwingine chini ya sheria ya mwaka 1995 waliona kuwa JBA ni mzigo kwao na walitaka ichukuliwe na asasi nyingine yoyote ya serikali. Kuvunjwa kwa JBA kulitoa nafasi ya kuanzishwa kwa UDCA (Urban Development Control Authority)ambayo ilianzishwa chini ya sheria ya 1955 ya Town and Country Planning decree ambayo ipo chini ya Wizara ya Ardhi na Upimaji. Safari hii Mwenyekiti wake akiwa ni Mkurugenzi wa Manispaa na katibu akiwa ni Town Planner wa Manispaa na wajumbe wengine 10 toka katika asasi zingine zinazohusika na ujenzi. Kwa ufupi UDCA ipo lakini haina nguvu kisheria kutokana na kuwepo kwa sheria ya Halmashauri ya Manispaa ya Mwaka 1995. Aidha sheria iliyotumika na Waziri huyo haina nafasi katika Halmashauri ya Manispaa, kwani Mkurugenzi wa Halmshauri anawajibika kwa Waziri wa Tawala za Mikoa na si venginevyo. UDCA inaendelea kufanya kazi kutokana na mazoea ya kuwepo na kitengo kama hicho katika miaka iliyopita.

Tukio lililotokea hivi karibuni la uvunjaji wa nyumba na misingi ya nyumba katika shehia ya Tomondo lililo fanyika chini ya amri ya Mkuu wa Mkoa wa Mjini Magharibi, Mhe. Abdallah Mwinyi, licha ya kuwa ni la kinyama halikufuata utaratibu wowote wa kisheria, zaidi limenikumbusha mojawapo ya sababu ya kumwondoa Mkuu wa Mkoa katika kudhibiti ujenzi visiwani humo. Aidha limenikumbusha kuwa Zanzibar Mjini hakuna sheria ya Ujenzi na kuna asasi nne zote hizo zikidai kuhusika na maendeleo ya ardhi katika mji huo na kufanya kuwepo na vurugu tupu katika kusimamia masuala ya ujenzi katika Mkoa huo wa Mjini Magharibi.

Aidha kuna umuhimu mkubwa kuona kuwa migongano ndani ya Mipaka ya Master plan ya mwaka 1982 inakwisha na kuna umuhimu mkubwa kuona kuwa Idara ya Upimaji, Idara ya Ardhi, Mamlaka ya Hifadhi na Uendelezaji Mji Mkongwe, Halmshauri ya Manispaa ya Zanzibar, Halmashauri ya Magharibi, Ofisi ya Mkuu wa Mkoa na Ofisi ya Mkuu wa wilaya ya magharibi pamoja na ofisi ya Mwanasheria mkuu wa serikali wanakaa pamoja na kuamua ni sheria gani ya ujenzi itumike katika eneo la master plan ya mwaka 1982. Kwani kwa sasa hakuna sheria inayotumika zaidi ya wizi mtupu. Yaani inatia aibu kwa wizi huu wa mchana kweupe, huku wanaoumia ni wananchi wasio jua wafuate sheria gani kupata kibali halali cha ujenzi wa nyumba zao.

Wednesday, 18 February 2009

E-governance for African Municipalities...Ni Wizi Mtupu....!


Zenj mara nyingi imekuwa ikiingia kwenye rekodi mbalimbali barani Afrika na Duniani kutokana na matukio ya maisha maendeleo na teknologia. Rekodi kadhaa zimeandikwa ndani ya visiwa hivyo, hivyo kuongeza umaarufu wake na wakati huo huo kuboresha huduma mbalimbali kwa wananchi wake.

Zanzibar inaendelea kujivunia rekodi zake mbalimbali hadi wakati huu ingawa zingine zilishindwa kuendelezwa na hivyo kubakia kwenye kumbukumbu tu na kuwa hadithi kwa vijana kutambiana na hasa wanapokuwa katika ubishi na wenzao wa bara. Mapema mwaka huu Zenj iliibuka tena na kujiwekea rekodi nyingine mpya katika Afrika ya Mashariki, na iwapo rekodi hii itakuwa na mafanikio hapana shaka itaanza kusambaa taratibu kwa nchi zote za jirani. Safari hii rekodi hiyo haikupokelewa vizuri na nchi jirani, hata hivyo nina hakika baada ya muda wataifuata tu. Hii ni rekodi ya kuwa nchi ya kwanza katika Afrika ya Mashariki kutoa leseni ya udereva yenye kumbukumbu zote muhimu za mwenye leseni pamoja na namba yake ya ulipaji kodi. Hii ni hatua nzuri na kubwa kwa nchi zenye matatizo ya ukusanyaji wa kodi.

Mafanikio haya yote siku zote yanakuwa na lengo moja kubwa la urahisishaji wa utendaji na uongezaji wa ufanisi katika utoajo wa huduma, ambapo ni hatua muhimu ya kuondokana na ukiritimba ambao umekuwa ukichangia kwa asilimia kubwa kuwepo na rushwa na hatimae ufisadi.

Hata hivyo sio mambo yote ambayo yamekusudiwa kufanikisha na kurahisisha utoaji huduma katika Zanzibar yamefanikiwa. Ni watu wachache ambao watakumbuka kuwepo na mradi wa E-governance for African Municipalities kwa Manispaa tano tu barani Afrika ikiwemo Zanzibar, Manispaa zingine zilikuwa ni Bamako (Mali), Maputo (Mozambique), Niamey (Niger) na Lusaka (Zambia). Lengo la mradi huu ambao ulianza mwaka 2001 ilikuwa ni kuziunganisha Manispaa hizo tano katika mtandao mmoja aidha kuwezesha Manispaa hizo kuwa karibu na wananchi wake kwa utoaji wa huduma ya habari kwa njia ya mtandao. Kwa Manispaa ya Zanzibar kupitia mtandao uliofungwa katika Idara zake zote ilikusudiwa kurahisisha ubadirishanaji wa habari za kiutendaji katika idara hizo kwa njia ya umeme(electronically). Zaidi ilikusudiwa kutoa habari juu upatakanaji wa leseni mbalimbali kwa wananchi wake kupitia kwenye tovuti yake, pamoja na wananchi hao kupata nafasi ya kutumia mtandao huo bure katika sehemu maalumu kwa ajili ya kupata habari juu ya sheria ndogo ndogo mpya, muhtasari wa vikao vya kamati za Manispaa na Baraza Kuu, ukusanyaji wa mapato na matumizi yake na kuweza kujionea bajeti ya Manispaa hiyo ndani ya mtandao.

Mradi huu ambao ulikuwa unadhaminiwa na DANIDA/UNESCO, ulikamilika mwaka 2003, ambapo pamoja na Manispaa kupatiwa vitendea kazi vyote na taaluma kwa watendaji wake, wadhamini hao waligharamia na uanzishaji wa tovuti ya manispaa hiyo, ambayo tokea mwaka 2003 hadi leo hii imedumaa. Huu ni wizi mtupu.

Mradi huu ulikuwa wa thamani ya dola za kimarekani elfu arobaini haukuweza kuendelea kama ilivyokusudiwa kwa sababu zisizo na msingi zaidi ya kuendeleza tabia za ukiritimba ndani ya vyombo vya utoaji wa huduma ambapo ni wizi mtupu.

Madiwani ambao kwa namna moja ama nyingine ndio wanao wawakilisha wananchi wao katika Manispaa, ilitegemewa wawe mstali wa mbele kuona huduma hii muhimu iliyokuwa inaweza kuwapunguzia bughuza za waombaji wa fomu kugonga milango ya nyumba zao alfajili, kuwabana wahusika kuikamilisha tovuti hiyo ili kuwezesha wananchi kujaza fomu online walikaa kimya na kufumbia macho kudumaa kwa mradi huu ili waweze kuendelea kuwazungusha wananchi wao juu ya upatikanaji wa fomu mablimbali... Huu ni wizi mtupu!

Mkurugenzi wa Manispaa ama kwa kutojua ama kushindwa kwenda na mabadiliko katika utoaji wa huduma nae alishindwa kuendeleza mradi huu. Kwa nafasi yake angeweza kuhakikisha kuwa kila Idara inapeleka taarifa zake za mapato katika tovuti hiyo na kila idara inaweka fomu za maombi katika tovuti hiyo na hivyo kupunguza ama kuondoa foleni zisizo na ulazima wowote katika Ofisi ya manipaa hiyo. Hata hivyo kwa miaka saba sasa amekaa kimya tokea alipoweka ada za kupaki magari mwaka 2003... Wizi mtupu!

Mstaki Meya ambae huwa anaalikwa kwenye matukio muhimu yote yanayofanyika katika Manispaa yake nae ameshindwa kumbana afisa uhusiano kuona kuwa Matukio muhimu yote yanawekwa katika tovuti hiyo, hii ingekuwa ni njia mojawapo ya kuelekea kuweka hata matangazo ya matukio kwa njia ya kulipia hivyo kuifanya tovuti hiyo kuingiza mapato. Nae kama wengine ameamua kukaa kimya... Ni wizi mtupu!

Tovuti ya Baraza la Manispaa ilifanyiwa marekebisho kwa mara ya mwisho mwaka 2003, na hata yale ambayo yamo katika tovuti hiyo yanatia kichefuchefu. Yaliyoandikwa humo yana uhusiano mdogo kabisa na shughuli za Manispaa hiyo huu ni wizi mtupu. Hata design na layout ya tovuti hiyo ni vichekesho vitupu... Yaaaani ni Wizi mtupu!

Thursday, 12 February 2009

Ni wiki ya Sauti za Busara (Sounds of Wisdom) huko Zanzibar



Tamasha la sita la Sauti za Busara limeshaanza rasmi siku ya Jana kwa maanandamo ya ufunguzi wa tamasha hilo ambalo sasa ni mojawapo ya tamasha kubwa kabisa barani Afrika. Tamasha hili litadumu kwa muda wa siku sita(12-18/02/2009)na tokea kuanza kwake limekuwa likifanyika katika wiki ya pili ya mwezi wa pili.

Tamasha la mwaka huu litatumbuizwa na wasanii maarufu toka karibu pande zote nne za Afrika, kwa mjibu wa tovuti ya sauti za busara wasanii ambao wana washabiki wengi kwa mwaka huu ni Bi Kidude, Culture Musical Club, DJ Yusuf, Samba Mapangala & Orchestre Virunga, Jagwa Music, Best of WaPi, Iddi Achien'g, Natacha Atlas, Segere Original na Joh Makini

Kwa habari zaidi tembelea hapa chini